NA DIRAMAKINI
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt.Hussein Ali Mwinyi amewataka Wazanzibari wote kujitokeza kuhesabiwa katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi 2022, linalotarajiwa kufanyika Agosti 23, 2022.

Dkt.Mwinyi ametoa wito huo katika hafla ya makabidhiano ya Anuani za Makazi, hafla iliofanyika katika makazi ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Migombani, Mkoa Mjini Magharibi.
Amesema, Serikali imefikia uamuzi wa kuifanya Agosti 23, 2020 kuwa ya mapumziko ili kutoa fursa kwa wananchi wote kuweza kushiki kikamilifu katika zoezi hilo litakalofanyika nchini kote.
Amesema, ana furaha kubwa kupokea anuani hiyo na kufanikisha mchakato huo kwa wakati kabla ya zoezi la sensa na makaazi 2022 kuanza kama ilivyoelekezwa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan.

Naye Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Dkt.Khalid Salum Mohamed amesema, hadi kufikia sasa wizara hiyo kwa ushirikiano wa karibu na Shirika la Posta Tanzania imefanikiwa kuweka Anuani za Makaazi zipatazo 451,128 Unguja na Pemba, ikiwa ni zaidi ya malengo yaliowekwa.
Amesema, hatua hiyo ni ya mafanikio kwa kuzingatia kuwa utekelezaji wake umekwenda sambamba na muongozo wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania,Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alielekeza zoezi hilo liwe limekamilika kabla ya zoezi la Sensa ya Watu na Makazi kuanza.
Alieleza kuwa, kazi iliobaki ni ya uwekaji wa vibati katika baadhi ya Nyumba na Majengo, na akabainisha zoezi linaloendelea la uwekaji wa nguzo ambapo nguzo 17,000 zinatarajiwa kuwekwa katika mitaa mbalimbali Unguja na Pemba.
