RC Rashid, DC Mkasaba wasema wapo tayari kuhesabiwa, wafurahishwa na utayari wa wananchi Kusini Unguja

NA DIRAMAKINI

MKUU wa Mkoa wa Kusini Unguja, Rashid Hadid Rashid amewasisitiza wananchi wa Wilaya ya Kusini kutoa ushirikiano mkubwa kwa makarani wa Sensa siku ya zoezi la Sensa ya Watu na Makazi itakapofika ili lengo lililokusudiwa liweze kufikiwa.
RC Rashid ameyasema hayo katika Bonanza la kuhamasisha Sensa ya Watu na Makazi lililofanyika huko katika uwanja wa Jamhuri Makunduchi Wilaya ya Kusini Mkoa wa Kusini Unguja lililoandaliwa na uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya kwa ushirikiano na Ofisi ya Wilaya ya Kusini.

Katika maelezo yake, Mkuu wa Mkoa huyo alisema kuwa tayari wananchi walio wengi wamepata mwamko juu ya zoezi hilo linalotarajiwa kufanyika Agosti 23, 2022 na kusema kwamba kwa wilaya hiyo pamoja na mkoa wake ana matumaini makubwa kwamba zoezi hilo litafanyika vizuri.

Alieleza kwamba kwa vile tayari siku ya tarehe 23 imeshatangazwa rasmi kwamba ni siku ya mapumziko hivyo ni vyema wananchi wakaitumia vizuri siku hiyo ili zoezi hilo liweze kufanikiwa kwa kiasi kikubwa.

Mapema Mkuu wa Wilaya ya Kusini Rajab Yussuf Mkasaba aliwasisitiza wananchi wa Wilaya hiyo kutofanya makosa na badala yake washiriki vyema katika zoezi hilo muhimu kwa maendeleo ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa sahihi kwa makarani wa Sensa.

Alieleza kwamba, zoezi la Sensa lina umuhimu mkubwa kwani litatoa fursa kwa Serikali kupanga na kupeleka maendeleo zikiwemo huduma za kijamii kwa wananchi wake.

Mkasaba alieleza matumaini yake kwamba zoezi hilo kwa wilaya hiyo litafanikiwa kwani tayari maandalizi mazuri yanaendelea kufanyika na kutoa pongezi kwa wananchi mbalimbali waliojitokeza katika Bonanza hilo ambalo lilifana.

Nao viongozi wa CCM wa wilaya hiyo waliwasihi wananchi kuhakikisha wanahesabiwa siku itakapofika ili kuweza kuisaidia Serikali kufanya shughuli zake kwa ustadi zaidi ikiwemo kuwapelekea maendeleo endelevu wananchi popote pale walipo.

Mapema katika bonanza hilo michezo mbalimbali ilifanyika ikiwa ni pamoja na mashindano ya kufua na kukuna nazi, mbio za magunia, mashindano ya kibuli, mchezo wa kuigiza ulioongozwa na msanii mahiri maarufu Makombora, uvutaji kamba, nage pamoja na pambano la mpira wa miguu kati ya Jimbo la Paje na Makunduchi.

Baada ya kumalizika kwa mashindano hayo mgeni rasmi alitoa zawadi kwa washindi ikiwemo timu ya Paje ambayo iliifunga Makunduchi mabao mawili kwa moja.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news