BUNDI WA GAMBOSHI SEHEMU YA 41

NA WILLIAM BOMBOM

ILIPOISHIA... Nilipomfikisha kwenye eneo alilopaswa kuchinjwa, nilichukua nondo nikaishusha kwa nguvu kichogoni mwake.
Damu zikachuruzika mithili ya bomba la umma litoalo maji. Akayatoa macho yake makubwa mithili ya mjusi aliyebanwa na mlango wa choo. Nikamsindikiza kwa teke la tumbo akajikunja kama jongoo...

Endelea;

Niliutumia muda huo kumsogeza karibu na eneo la msingi wa jengo, nikachukua jisu langu la jambia nikatenganisha kichwa chake bila huruma.

Damu zikaruka mfano wa mbuzi aliyechinjwa kwa ajili ya kafara. Tuliendelea na utaratibu wa kuwachinja abiria hao huku tukinyunyuzia damu eneo maalumu lililokuwa limepangwa kwa ajili ya ujenzi wa GAMBOSHI MPYA.

Eneo lote lilitapakaa damu mfano wa bwawa la tope, vichwa vya watu hao tulivichimbia kila kona ya eneo tulilofikiria kujenga majengo.

Baada ya kumaliza kazi hiyo, tulijipongeza kwa kunywa damu ya binadamu tuliyokuwa tumeijaza kwenye mitungi.

Ndugu msomaji tambua kuwa hakuna mchawi ambaye hapendi kunywa damu za binadamu. Ni muhimu kwa mchawi kunywa damu ya binadamu ili kutunza maagano ya kichawi baina yake na mkuu wake.

Ukichunguza ndani ya jamii yako utagundua mara nyingi wachawi huwa wanaishi miaka miaka mingi endapo watafuata utaratibu wa sheria za kichawi.

Hii yote husababishwa na uhai wa binadamu wengine ambao hupatikana ndani ya damu mbichi, ambayo sisi wachawi huwa tunakunywa.

Baada ya kukamilisha shughuli zetu kwa siku hiyo, tuliamua kurudi kwenye kambi yetu. Kwa kuwa kambini ilikuwa karibu na eneo hilo tuliamua kutembea kwa miguu, tulipita nyuma ya jengo la shule ya Msingi Airport tukatokeza mbele yake.

Wanafunzi walikuwa shuleni wakiendelea na ratiba za masomo, kwa nje tuliwaona wanafunzi wachache waliokuwa wakipewa adhabu na mwalimu wao.

Mwalimu huyu alikuwa ni miongoni mwa walimu waliokuwa wakiogopwa sana na wanafunzi kulingana na ukali wake.

Alikuwa mkali zaidi ya pilipili kichaa, alikuwa akiwashikisha adabu wanafunzi watovu wa nidhamu huku wazazi baadhi wakilaani.

Alipewa jina la utani kuwa mwalimu Mboko, unajua wanafunzi huwaita walimu wao majina ya utani kulingana na sifa zao.

Jina hili aliitwa kulingana na kauli yake aliyokuwa akiitumia sana wakati anatoa adhabu, alipenda kusema "Shika hapo mboko ipenye" wanafunzi wakaamua kumpa jina la Mboko.

Tulisogea karibu na eneo alilokuwa akitoa adhabu mwalimu huyo, tulipofika karibu zaidi tulikuta anamchapa kijana mmoja aliyekuwa amelala chini.

Nilipomtazama kwa makini mwanafunzi huyo nikamtambua, alikuwa ni mjukuu wa miongoni mwa wachawi walionisaliti na kukimbilia kambi ya Padri Jonasi Chambilacho Muzungu.

Nikamuagiza mchawi mmoja kufanya jambo, alichukua nondo yake akasogea mkabala na yule mwalimu.

Wakati mwalimu anashusha kiboko matakoni mwa mwanafunzi huyo, mchawi huyo alishusha nondo kichwani mwa mwanafunzi huyo.

Lilikuwa ni pigo takatifu lililochukua uhai wa kijana huyo, baada ya kufanya kitendo hicho tuliondoka tukamuacha mwalimu akiwa katika hali ya kupigwa butwaa.

Hapa niseme kidogo, mara nyingi kuna vifo hutokea kwenye jamii pasipo kutegemewa. Unaposikia baba kampiga mwanae mpaka kamuua kwa ajili ya sigara hapa jifikirie mara mbili mbili.

Unaposikia mama kamuua mwanae wa kuzaa kisa kaiba mboga tambua kuna nguvu za ziada. Matukio mengi ya ajabu ndani ya jamii huwa yana nguvu za ziada nyuma ya pazia, tukio la mwalimu kumuua mwanafunzi lilitapakaa ndani ya jamii.

Raia wa mji wa majengo walimiminika shuleni hapo wakiwa na hasira, walitaka kujichukulia sheria mkononi dhidi ya mwalimu Mboko.

Kiuhalisia mwalimu hakuwa ameua, kilochomponza ilikuwa ni sifa yake ya ukali. Ukali wake tuliutumia kutengeneza skendo kubwa ndani ya jamii, kitendo cha kumuua mwanafunzi yule kisingetia shaka kwa jamii maana toka mwanzo mwalimu alijulikana kwa ukali wake.

Hakuna mtu ambaye angefikiria nje ya boksi, watu wote waliamini kuwa mwalimu alikuwa kaua.

Tukaachana na skendo za mwalimu Mboko, tulivuka barabara ya lami kisha tukatokeza upande wa pili, tilivuka mashine ya kusaga nafaka kisha tukapinda kulia tukaifuata barabara inayoelekea kambini kwetu.

Njia tulikutana na watu kibao wakielekea shuleni wengine wakielekea eneo la ajali pale Mganza. Hakuna aliyekuwa akituona kwa kuwa ilihitaji sayansi ya hali ya juu kutuona, kulitakiwa macho ya pili jambo ambalo ni gumu sana.

Tulifika kambini tukawakuta wachawi wengine wakiendelea na shughu zao, kwa kawaida pale kambini kulikuwa na zamu za wachawi kusimamia mambo mbalimbali.

Hata hivyo kila kitengo kilikuwa kikiongozwa na wachawi viongozi, wachawi wa zamu alikusanya taarifa kwa siku kupitia viongozi wa kila kada kisha kuwasilisha makao makuu. Kambi ilikuwa salama salimini, misukule walikuwa wakiendelea na shughuli zao kama ilivyo ada.

Niliwaruhusu wachawi wenzangu wakaao nje ya kambi kurudi makwao. Hapa niseme kidogo, wachawi hufanya kazi zao katika makundi mbalimbali kulingana na nguvu za uchawi walizo nazo.

Wapo ambao hufanya uchawi mchana na usiku, wapo ambao huloga usiku mnene, wengine huloga usiku wa mwanzo.

Utofauti wa wachawi hawa huamuliwa na nguvu za madawa wanayoyamiliki. Kwa kuwa kambi yetu ilikuwa ni kubwa, wachawi wa sehemu mbalimbali kijijini waliweza kujiunga. Madawa tuliyokuwa tukiyamiliki yalikuwa ni ya kiwango cha juu, ndiyo maana tuliweza kuloga mchana, usiku na muda wowote tuliojisikia.

Zipo njia mbalimbali za mchawi wa mchana kuwazubaisha familia yake pindi anapokwenda mchana kuwanga.

Njia ya kwanza ni huyo mchawi kuwaambia familia yake anajipumzisha hivyo hataki usumbufu, kabla ya kuondoka ataacha mnyama au gogo kitandani kwake lenye picha yake.

Njia ya pili hutengenezwa dawa za kusahau, yaani familia nzima na watu wengine huwa wanasahaulishwa uwepo wa muhusika.

Watafanya shughuli zao zote huku hawakumbuki kama katika familia hiyo kuna mtu wa aina hiyo. Mpaka mchawi huyo atakaporudi ndipo fikra za watu nazo hurudi.

Njia ya tatu ni kutengeneza msukule mwenye picha ya mchawi, msukule huyo mtazungumza naye na kufanya mambo yote sawa na muhusika.

Hizi ni baadhi ya njia zinazotumiwa na wachawi wa mchana kuwahadaa watu pindi wanapokuwa wamekwenda kuloga mchana.

Ndugu msomaji, dunia imejaa vitimbwi. Hasa katika dunia hii ya giza imefunikwa na mambo mazito, mengine ni vigumu kuyasimulia kulingana na sheria zake.

Yapo mambo ya ajabu yanayotendeka, mengine hufanywa na wale tunaowaita wapendwa wetu. Mfano asilimia mia moja ya watu waliooa wachawi au waliona wapenzi wachawi wamewahi kufanya mapenzi na mbwa au fisi.

Wanyama hawa kwa kiasi kikubwa hutumiwa na wachawi kama mbadala wao usiku wanapokwenda kufanya kazi zao.

Pia nyani au kondoo nao hutumiwa pamoja na misukule, hutegemea na namna mchawi atakavyokuwa ameamua kumuacha nani kama mbadala wake.

Wanaume mmefanya mapenzi sana na hao wanyama, kama mke wako ni mchawi hilo haliepukiki. Mbaya zaidi ukikutana na msukule ambaye ana muda mrefu hajafanya tendo la ndoa, siku hiyo unaweza ukafikiri mke wake au mpenzi wako alikukumbuka sana kumbe hapana. Ni msukule au fisi aliyekuwa na ashiki za ngono kwa muda mrefu.

Baada ya baadhi ya wachawi kurudi makwao huku wengine wakiendelea na shughuli zao kambini hapo, niliamua kujipumzisha kulingana na uchovu niliokuwa nao.

Pia usiku wake tulikuwa na mkutano mkuu wa kambi yetu, kwa namna hiyo THE BOMBOM nilipaswa kupata muda mkubwa wa kupumzika.

Jioni yake tulikutana kwenye kikao kama kawaida, kikao kilikuwa kinahusu namna ya kupata misukule watakaojenga majengo ya GAMBOSHI MPYA.

Pia tulifikilia namna ya kupata chakula kitakachowalisha misukule hao watakaokuwa wakijenga majengo hayo.

Mchawi wa kwanza alishauri tusiue watu, bali tutafute mafundi washi wazuri katika mji wa Nguruka, Majengo, Mlyabibi, Mganza, Bweru na Itebula.

Katika miji hiyo kulikuwa na mafundi zaidi ya Elfu mbili, hawa wangetumika katika ujenzi wa GAMBOSHI MPYA pasipo hata kuwaua.

Aliongeza kwa kusema kuwa iwapo hawatatosha basi tunaweza kuongezea mafundi katika miji mingine kama Kigoma, Kasulu, Tabora, Urambo na Kaliua.

Kwa namna hiyo itatuwia rahisi kukamilisha ujenzi wa *GAMBOSHI MPYA* pasipo kumwaga damu za binadamu, wazo la mjumbe lilikuwa zuri lililovutia kwa idadi kubwa ya wachawi.

Mjumbe wa pili alishauri kuwa, wazo la mjumbe wa kwanza ni zuri isipokuwa linatakiwa liongezewe nyama.

Yeye alisema kulingana na michoro na ramani za majengo hayo tulipaswa kupata mafundi waliobobea, yeye akashauri ni vyema tuwaue wachina watano waliokuwa wakisimamia barabara ya Uvinza kwenda Mpanda kupitia Sumbawanga.

Hawa ndiyo watasimamia ujenzi huo na ujenzi mwingine wakiwa kama misukule wetu. Mbija, vifijo na nderemo zililipuka, kila mchawi alionekana kuunga mkono wazo hilo.

Ndugu msomaji mambo ndiyo yameanza kuiva, unadhani kikao hicho kitamalizika salama? Je, wachina hao wataingia kwenye mikono ya wachawi? Endelea kufuatilia kisa hiki cha kusisimua.

WABONYE?
THE BOMBOM

Ukihitaji kisa hiki sehemu ya kwanza hadi ya 40 usisite kutujulisha

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news