'Jukumu la Wizara ya Madini ni kuunda na kusimamia Sera ya Madini'

NA TITO MSELLEM-WM

JUKUMU la Wizara ya Madini ni kuunda Sera na kusimamia Sheria ya Sekta ya Madini sambamba na utoaji wa mafunzo ya kitaalamu ya uendeshaji wa shughuli za madini ikiwa ni pamoja na kusimamia taasisi zilizo chini ya wizara.
Hayo yamebainishwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo wakati akifungua Semina ya Wachimbaji Wadogo wa Madini uliyofanyika katika ukumbi wa EPZ uliopo katika viwanja vya Bombambili mkoani Geita.

Mbibo amesema lengo la semina hiyo ni kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata elimu na ujuzi wa namna bora ya utafiti, uchukuaji wa sampuli, uchimbaji na uchenjuaji wa madini.
Aidha, Mbibo amesema Sekta ya Madini ni sekta muhimu kwenye uchumi wa Taifa, hivyo Tanzania haina sababu ya kuto kupiga hatua ya maendeleo kutokana na rasilimali za madini zilizopo nchini.

"Ili Sekta ya Madini iweze kutunufaisha ipasavyo, lazima tuyafanye kwa uzuri na kwa utaratibu ikiwemo kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu," amesema Mbibo.
Pamoja na mambo mengine, Mbibo ametoa wito kwa wachimbaji wadogo kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika semina hiyo kwa lengo la kujipatia elimu na ujuzi wa namna bora ya uendeshaji wa shughuli zao.

Pia, Mbibo ameiagiza Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) pamoja na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kuendelea kutoa elimu ya namna ya kufanya tafiti na uchukuaji wa sampuli.

Sambamba na hayo , Mbibo ameupongeza mkoa na wilaya ya Geita kwa kuendesha zoezi la uandaaji wa Maonesho ya 5 ya Teknolojia ya Madini 2022.
Katika hatua nyingine, Mbibo ametembelea maandalizi ya Maonesho ya 5 ya Teknolojia ya Madini katika mabanda yote yanayoendelea mkoani Geita.
Naye, Mkuu wa Wilaya ya Geita Shimo William amempongeza Mbibo kwa kukubali kufungua semina hiyo na kuahidi kuendelea kuwalea na kuwasimamia vyema wachimbaji wadogo wa mkoa huo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news