Waziri Mkuu amwakilisha Rais Samia mazishi ya Shinzo Abe

NA MWANDISHI WETU

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameungana na wakuu wa nchi na viongozi mbalimbali 700 kutoka nchi 195 na mashirika ya kimataifa 23 kuweka mashada kwenye mazishi ya kitaifa ya Waziri Mkuu mstaafu wa Japan, Bw. Shinzo Abe.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwa ameongozana na mkewe Mery Majaliwa wakimpa mkono wa pole Waziri Mkuu wa Japan Fumio Kishida, kwenye Kasri la Kifalme la Akasaka, jijini Tokyo Japan, Septemba 27.2022. Baada ya kutoa heshima za mwisho kwa Waziri Mkuu mstaafu wa nchi hiyo, Bw. Shinzo Abe. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Waziri Mkuu ambaye yuko Tokyo, Japan akimwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan, ametoa heshima hizo za mwisho leo Jumanne, Septemba 27, 2022 kwenye ukumbi wa Nippon Budokan akiwa ameambatana na mkewe Mary Majaliwa, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassoro Mbarouk, Balozi wa Tanzania nchini Japan, Balozi Baraka Luvanda na mkewe Consolata Luvanda.

Baada ya kutoa heshima za mwisho, Waziri Mkuu alikwenda kwenye Kasri la Kifalme la Akasaka, jijini Tokyo ambako hufanyika shughuli zote za Kiserikali ili kumfariji Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Fumio Kishida pamoja na mjane wa Bw. Shinzo Abe, Bibi Akie Abe. Alikuwa miongoni mwa viongozi wengine wa kitaifa 40 ambao walipata fursa hiyo.

Viongozi wengine wa kitaifa walioshiriki mazishi hayo ni Marais kutoka Vietnam, Sri Lanka, Makamu wa Rais kutoka Indonesia, Marekani, Ufilipino, Marais wastaafu wa Ufaransa, Ujerumani na Mfalme wa Falme za Kiarabu, mtawala wa Qatar na Amiri wa Kuwait. Mawaziri Wakuu 16 walihudhuria mazishi hayo.

Miongoni mwa mawaziri wakuu waliokuwepo ni Narendra Modi (India), Justin Trudeau (Canada), Han Duck-soo (Korea Kusini) na Antony Albanese (Australia). Wengine ni Mawaziri Wakuu wastaafu, Maspika, Majaji, wakuu wa mashirika ya Umoja wa Mataifa na mabalozi. Baadhi ya nchi na taasisi zilizowasilisha salamu za rambirambi, zilisomwa majina yao.

Mapema asubuhi, wakazi wa Japan walijipanga kwenye misururu mirefu ili kupata fursa ya kutoa heshima zao za mwisho kwa kuweka mashada ya maua kwenye eneo maalum lililoandaliwa katika bustani nje ya ukumbi huo. Ukumbini kulikuwa na watu zaidi ya 4,300.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news