Simba SC yawapigisha kwata Polisi Tanzania yaondoka na 3-1

NA DIRAMAKINI

POLISI Tanzania wamepigishwa kwata na wageni wao Simba SC ya jijini Dar es Salaam huku ikijizolea alama zote tatu zikisindikizwa na mabao 3-1.

Ni kupitia mtanange wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara ambao umepigwa leo Novemba 27, 2022 katika dimba la Ushirika mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.

Nahodha John Bocco dakika ya 32 na Mzambia, Moses Phiri mawili, dakika ya 43 na 53 ndiyo walioharibu mipango ya Polisi Tanzania na kuifanya Simba SC kung'ara.

Aidha,bao la kufutia machozi la Polisi Tanzania limefungwa na Zuberi Mbogo dakika ya 90 wakati mtanange huo ukielekea ukingoni.

Matokeo hayo yanaifanya Simba SC kufikisha alama 31 katika mchezo wa 14 na kubakia nafasi ya tatu ikizidiwa pointi moja tu na mabingwa watetezi, Yanga ambao wana mechi mbili mkononi.

Aidha, kwa upande wao, Polisi Tanzania baada ya kichapo hicho wanabaki na alama zao tisa za mechi 14 huku nafasi yao ikiwa 14 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara.

Katika mtanange huo,Kocha Juma Mgunda alifanya mabadiliko ya kuwatoa Gadiel Michael na Bocco na kuwaingiza Kennedy Juma na Kibu Denis.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news