Wahitimu vyuo vikuu wafundwa,vituo vyote vya Chuo Kikuu Huria kuunganishwa na Mkongo wa Taifa

NA MWANDISHI WETU

WAHITIMU mbalimbali wa vyuo vikuu nchini wameaswa kutumia vema elimu wanayopata ili kuleta tija kwa Taifa.
Hayo yamesemwa jijini Mwanza na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Phillip Mpango wakati wa mahafali ya 41 ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT).
Aidha, Mhe. Mpango ameagiza Wizara ya Elimu kuhakikisha vituo vyote vya chuo hicho vinaunganishwa na mkongo wa Taifa ili kuwezesha matumizi ya TEHAMA na kupunguza gharama za uendeshaji .

"Vituo vyote vya Chuo Kikuu Huria vitaunganishwa na mkongo wa Taifa na hili naagiza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kuhakikisha linafanyika mara moja ili kupunguza gharama za uendeshaji," ameongeza Mhe. Mpango
Awali akiongea katika mahafali hayo, Mhe. Prof. Adolf Mkenda, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia amesema Chuo Kikuu Huria kimetengewa fedha kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) kwa ajili ya ujenzi wa miundo mbinu, kusomesha wahadhiri na miradi mingine.
"Serikali kwa kutambua mchango wa Chuo Kikuu Huria katika kupeleka elimu kwa jamii kupitia mradi wa HEET tutajenga maabara saba katika mikoa ya Njombe, Arusha, Dodoma, Mwanza, Kigoma, Mtwara na Pwani ambazo zitajikita katika tafiti za kisayansi kulingana na shughuli na mahitaji muhimu ya eneo husika," amefafanua Waziri Mkenda.

Waziri Mkenda ameongeza kuwa Serikali imetoa zaidi ya Shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya kujenga vituo vya Chuo Kikuu Huria katika mikoa ya Geita, Kigoma, Lindi, Simiyu na Manyara ambao mikoa hii ilikuwa ikitumia majengo ya kukodi kwa gharama kubwa.
Zaidi ya Wahitimu 4,000 wametunukiwa Shahada mbalimbali zikiwemo Shahada za Umahiri na Uzamivu wakiwemo wanafunzi kutoka nchi jirani za Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Ghana, Malawi, Zambia, Congo, Namibia na Ethiopia.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news