Waliokata mkono wa Albino na kukimbia nao wadakwa

NA DIRAMAKINI

WATU watano wamekamatwa wakituhumiwa kuhusika na kifo cha kikatili cha Joseph Mathias (28) kilichotokea usiku wa Novemba 2, 2022 kwa kukatwa mkono wa kulia na kusababisha kifo chake katika Kijiji cha Ngulla wilayani Kwimba mkoani Mwanza.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Adam Malima ameyabainisha hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maendeleo ya kuwasaka watuhumiwa wa sakata hilo ambao wamekamatwa wilayani Misungwi.

"Wiki iliyopita yalitokea mauaji mabaya sana na nilitoa maagizo kwa Jeshi la Polisi na vyombo vingine vinavyohusika na uchunguzi kuhakikisha wanawakamata watu wote waliohusika na tukio hilo na juzi wamewakamata wahalifu hao, kwa kweli nawapongeza sana Jeshi la Polisi na wananchi wote waliotoa ushirikiano,"amesema Mhe.Malima.

Amefafanua kuwa, marehemu Mathias alifikwa na umaiti kutokana na kupoteza damu nyingi, kwani pale nyumbani kwake alikatwa mkono kwa kutumia kitu kikali na marehemu alibaki akihangaikabila msaada huku akiendelea kupoteza damu.

Vilevile, ametoa agizo kwa vyombo vinavyohusika na uchunguzi kuendelea kufuatilia mwenendo mzima wa uovu huo ili asibaki hata mtu mmoja aliyehusika bila kukamatwa aidha awe aliyetekeleza mauaji, aliyetengeneza mazingira, mwendesha bodaboda aliyewabeba, mganga wa kienyeji au hata mwanasiasa yeyote kama alihusika.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, SACP Wilbroad Mtafungwa amefafanua kuwa, marehemu Joseph Mathias aliuawa usiku wa Novemba 2, 2022 na watu waliofika nyumbani kwake na kumuita atoke nje na alipotoka alishambuliwa na takribani watu wapatao watano na kumkata mkono na kuondoka nao, hivyo kusababisha kifo chake kwa kupoteza damu.

Ameongeza kuwa Jeshi la Polisi limefanya msako mkali kwenye maeneo mbalimbali wilayani Kwimba na siku ya Novemba 6, 2022 walifanikiwa kumkamata mtu mmoja aliyebeba begi jeusi na baada ya upekuzi alikutwa na mkono wa binadamu na mtuhumiwa alikiri kuhusika kwa kushirikiana na wenzake kufanikisha uovu huo.

"Baada ya uchunguzi wa kitaalamu imebainika ya kwamba mkono ule ni wa marehemu Joseph Mathias na Mtuhumiwa huyo pamoja na wenzake tunaendelea kuwahoji na kwa hakika msako mkali unaendelea na hatabaki mtu hata mmoja ambaye amehusika na mauaji hayo na baadae watafikishwa mahakamani,"amesema Kamanda Mtafungwa.

Kamanda Mtafungwa ametoa wito kwa wananchi kuendelea kuliamini Jeshi la Polisi na kusaidia kufanikisha kuwakamata wahalifu na pia ametoa onyo kali kwa jamii kuacha mara moja kufanya vitendo vya kihalifu, kwani watakaokaidi agizo hilo watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news