WAZIRI MKUU:MRADI WA SGR UTAKAMILIKA KAMA ULIVYOPANGWA

NA MWANDISHI WETU

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema ameridhishwa na maendeleo ya mradi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) na kwamba Serikali itaendelea kuhakikisha mradi huo unajengwa kwa viwango na kukamilika kama ilivyobainishwa kwenye mkataba.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa (katikati) na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TRC, Profesa John Kondoro (kulia) wakati alipokagua ujenzi wa Stesheni Kuu ya Reli ya Kisasa (SGR) katika eneo la Mkonze jijini Dodoma, Novemba 24, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Amesema kuwa ujenzi wa reli hiyo unaendelea vizuri katika vipande vyote na kwamba Serikali itahakikisha mradi huo haukwami na itakabiliana na viashiria vyote vinavyoweza kukwamisha utekelezaji wake.

Ameyasema hayo leo Novemba 24, 2022 wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa stesheni kuu ya Dodoma katika eneo la Mkonze, jijini Dodoma.
Akizungumza baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa stesheni hiyo, Mheshimiwa Majaliwa amewataka Watanzania wanaoshiriki katika ujenzi wa mradi huo wasimamie usalama wa mradi na wawe walinzi ili ukamilike kama ilivyokusudiwa.

Aidha, Waziri Mkuu amesema kuwa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassam inaendelea kufanya maboresho kwenye sekta mbalimbali ikiwemo ya usafirishaji.

“Rais Samia anaendelea na mkakati wake wa ujenzi wa reli, endeleeni kuwa na imani na Serikali yenu, lengo lake ni kuhakikisha anainua uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla”.

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amemtaka Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma kuwa na mkakati wa maeneo ya uwekezaji kutokana na fursa ya ujenzi wa reli hiyo ikiwemo ujenzi wa kituo cha mabasi jirani na stesheni hiyo.

Kwa upande wake, Mkurgenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC) Masanja Kadogosa amesema kuwa Shirika hilo lipo kwenye mpango wa ununuzi wa vichwa vya treni na mabehewa ya mizigo. “Hadi sasa TRC imesaini mkataba wa ununuzi wa vichwa vya treni vya umeme 19, seti za treni 10 zenye uniti 80.”

Amesema pia shirika hilo itanunua mabehewa ya kawaida ya abiria 89, mabehewa ya ghorofa 30 ambayo yanakuja, mabehewa ya mizigo 1,430 na vifaa vya matengenezo 26.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news