Waziri Mkuu:Serikali ipo imara na inaendelea kuwahudumia wananchi

NA MWANDISHI WETU

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ipo imara na itaendelea kuhakikisha huduma mbalimbali za kijamii zinawafikia wananchi kwa ukaribu karibu.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua ujenzi wa Kituo cha Afya Nangurugai akiwa katika ziara wilayani Ruangwa, Novemba 18, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Amesema hayo leo Novemba 18, 2022 alipofanya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, wilayani Ruangwa, Lindi

Amesema kuwa Serikali ya awamu ya sita itaendelea kuipa kipaumbele sekta ya afya kwa kuimarisha utoaji wa huduma na ujenzi wa zahanati, vituo vya afya na hospitali nchini lengo likiwa ni kusogeza huduma hizo karibu na wannachi.

“Kituo cha afya cha Rais Samia kinakuwa na huduma zote muhimu zikiwemo za upasuaji, wodi ya wanawake na watoto, wodi za akinababa na akinamama, magonjwa mchanganyiko. Hii ndio dhamira yetu.”

Pia, Waziri Mkuu amesema ukarabati wa miundombinu ya kutolea huduma za afya unaoendelea nchini unahusisha hospitali za rufaa za kanda, hospitali za rufaa za mikoa, hospitali za halmashauri, vituo vya afya na zahanati.

Akizungumzia kuhusu usambazaji wa umeme vijijini, Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Serikali imesambaza wakandarasi wa umeme nchi nzima ikiwemo kwenye vijiji vya wilaya ya Ruangwa ili kuhakikisha huduma hiyo inawafikia wananchi wote.

Katika hatua nyungine, Waziri Mkuu amewataka viongozi wa mikoa wahakikishe wanabainisha wafugaji katika vijiji vyao ili kuwatambua pamoja na mifugo yao ikiwa ni mkakati wa kukabiliana na migogoro ya wakulima na wafugaji.

Waziri Mkuu ametoa wito kwa wafugaji nchini kuweka utaratibu wa kufuga mifugo ambayo anaweza kuihudumia. “Hakuna mwenye haki zaidi ya mwenzake, ukiamua kufuga fuga mifugo ambayo unaweza kuihudumia, usilishe kwenye mashamba ya watu, kufanya hivyo mkono wa sheria utakufuata.”

Kadhalika, Waziri Mkuu amezitaka Serikali za vijiji kuhakikisha wanasimamia sheria ya kutolima ndani ya mita 60 kutoka kwenye mito na vyanzo vingine vya maji ili kuhufadhi vyanzo hivyo.

Akizungumza na wananchi wakati alipokagua ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Mbwemkuru, Mheshimiwa Majaliwa amekipongeza kikundi cha vijana cha UKAJE UJENZI kwa kuamua kuanzisha umoja huo na kufanya kandarasi mbalimbali za Serikali.

Akizungumza kwa niaba ya Vijana wenzake, Mwenyekiti wa kikundi hicho amemshukuru Rais Samia kwa uamuzi wake wa kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo imekuwa fursa kwao ya kujipatia kipato na kujikwamua kiuchumi.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wakazi wa vijiji vya Nangurugai, Mbwemkuru na Narung’ombe wamemshukuru Rais Samia kwa fedha anazozitoa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo afya na elimu.

Mapema, Waziri Mkuu alitembelea familia zilizopoteza ndugu zao kutokana na tukio la wakulima na wafugaji kwenye kijiji cha Nambilanje. “Serikili itachukua hatua za kisheria kwa wote waliohusika na tukio hilo, tuendelee kuwaombea ndugu zetu, Serikali inatoa pole kwa familia zote zilizopoteza ndugu zao.”

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news