TWASHEREHEKA UHURU-1:Nyerere alitamani, mengi tuweze yapata

NA LWAGA MWAMBANDE

KATIKA kipindi cha miaka 61 ya Uhuru wa Tanganyika, ambayo mwaka 1964 ilibadilika jina kuwa Tanzania kufuatia Muungano na Zanzibar, kumekuwa na jumla ya marais sita ambao wameongoza nchi hii.

Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wakati wa kupata Uhuru wa Tanganyika. (Picha na Gettyimages).

Kila mmoja wa marais hao alitutumikia na kufanya vitu vya aina yake ambavyo vinafanya kila wakati tuendelee kuwakumbuka na kuwaenzi.

Katika mfululizo wa mashairi sita,mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anaelezea kwa njia ya ushairi baadhi ya mambo ambayo kila Rais katika awamu yake alifanya kama sehemu ya kuadhimisha Sikukuu ya Uhuru wa Tanzania, pamoja na kuweka kumbukumbu ya viongozi wetu hao, endelea;


1:Siti na moja miaka, tuna marais sita,
Ni vitabu vyafunguka, kwa kila anayepita,
Tunasoma twaridhika, nchi Yazidi kupeta,
Twashereheka uhuru, pia na maendeleo.

2:Nyerere wetu mwasisi, changamoto alipata,
Kututoa kwenye hasi, uhuru tukaupata,
Hakuwa na ukakasi, Muungano tukapata,
Twashereheka uhuru, pia na maendeleo.

3:Umoja lisisitiza, ukabila akafuta,
Kiswahili kukikuza, kote sasa kinapeta,
Kuondoka kaongoza, bila ya kusitasita,
Twashereheka uhuru, pia na maendeleo.

4:Kuulizana kabila, huwezi kuona hata,
Kwa pamoja tulikula, na elimu tukapata,
Wa Serengeti na Kyela, hakukuwa na ukuta,
Twashereheka uhuru, pia na maendeleo.

5:Nyerere alitamani, mengi tuweze yapata,
Kutoa umaskini, ujinga uliopita,
Na maradhi ya mwilini, afya bora weze pata,
Twashereheka uhuru, pia na maendeleo.

6:Uchumi weze jengeka, na kuombaomba hata,
Litaka tukajengeka, Ujamaa akaleta,
Kwa sehemu tulivuka, vya kuokotaokota,
Twashereheka uhuru, pia na maendeleo.

7:Ukombozi Afrika, wakoloni liipata,
Aliongoza hakika, uhuru tukaupata,
Nchi zinahesabika, ubwanyenye kuufuta,
Twashereheka uhuru, pia na maendeleo.

8:Na yule Idd amin, kwetu alipitapita,
Kutuvuruga amani, kwa kutuletea vita,
Nyerere litudhamini, Amini kazi mfuta,
Twashereheka Uhuru, pia na maendeleo.

9:Peke yake liamua, kwamba urais hata,
Kweli alisisimua, urais kumpita,
Mfano alizindua, marais tukipata,
Twashereheka uhuru, pia na maendeleo.

10:Yake Nyerere ni mengi, kwingine utayapata,
Kama kuupiga mwingi, kwa kweli alitakata,
Aliujenga msingi, ndimo humo tunapita,
Twashereheka uhuru, pia na maendeleo.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news