TWASHEREHEKA UHURU-2: Na Ali Hassan Mwinyi,Tena akaona mbali, uchumi ukafunguliwa

NA LWAGA MWAMBANDE

MHESHIMIWA Alhaj Ali Hassan Mwinyi aliyeongoza Serikali ya Awamu ya Pili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliingia madarakani rasmi Novemba 5,1985 hadi Novemba 23,1995.

Ikumbukwe kuwa, wakati wa uongozi wake, Mheshimiwa Mwinyi alifungua milango ya sera za soko huria kutoka Ujamaa.

Hivyo, masharti ya kuingiza bidhaa kutoka nchi za nje yalipunguzwa na uanzishaji wa biashara ya watu binafsi ulihamasishwa.

Mwaka wa 1991, Mheshimiwa Mwinyi alianzisha Tume ya Nyalali iliyopendekeza kuanzisha mfumo wa vyama vingi nchini. Wakati wa awamu yake kwenye mwaka 1995 ulitokea uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi vya kisiasa nchini Tanzania.

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema, tunaposherehekea miaka 61 ya Uhuru, Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi watanzania wataendelea kumpa heshima ya kipekee kutokana na uongozi wake ambao ulifungua milango ya kiuchumi na mfumo wa vyama vingi nchini, endelea;

1:Huyu asherehekewa, huyu anashangiliwa,
Na wengi afurahiwa, yake yanakumbatiwa,
Na Mungu livyotumiwa, milango kufunguliwa,
Twashereheka Uhuru, Na Ali Hassan Mwinyi.

2:Huyu Rais wa pili, tayari umetajiwa,
Alituliza akili, nafasi lipopatiwa,
Tena akaona mbali, uchumi kufunguliwa,
Twashereheka Uhuru, na Ali Hassan Mwinyi.

3:Huyu ni Mzee wetu, sana wa kuheshimiwa,
Likuta uchumi wetu, kwa vita mebomolewa,
Na hata watesi wetu, kwa sana twasumbuliwa,
Twashereheka Uhuru, na Ali Hassan Mwinyi.

4:Huyu ni Mzee Ruksa, uhuru tulipatiwa,
Ni wakati wake hasa, siasa kutanuliwa,
Vyama vipya vya siasa, ndiko vilianzishiwa,
Twashereheka Uhuru, na Ali Hassan Mwinyi.

5:Huyu alisemwasemwa, kiasi kusingiziwa,
Na watu waliotumwa, na wengine kutumiwa,
Lakini hawakuzimwa, Ruksa walipatiwa,
Twashereheka Uhuru, na Ali Hassan Mwinyi.

6:Lile fagio la chuma, kwake lilianzishiwa,
Wala rushwa walogoma, mbali walifagiliwa,
Mengi yaliyosimama, yalianza inuliwa,
Twashereheka Uhuru, na Ali Hassan Mwinyi.

7:Tunaye mzee wetu, hekima tunapatiwa,
Ni baba na babu yetu, kumwona twafurahiwa,
Alifanya mema kwetu, anazidi kuenziwa,
Twashereheka Uhuru, na Ali Hassan Mwinyi.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news