HEBU NIACHE NIBEBWE

NA LWAGA MWAMBANDE

WATAALAM wa malezi wanathibitisha kuwa,malezi ni mchakato wa maandalizi ya mtoto utakaomwezesha kukua, kukubalika na kushiriki katika shughuli za kijamii na kiutamaduni kwa kumlinda, kumjamiisha na kumpatia mahitaji na huduma za msingi kwa wakati.

Malezi bora. (Picha na Solbelearning).

Aidha, iwapo malezi ni mchakato wa maandalizi ya mtoto basi shurti iwepo mipango toka kwa wazazi ili kufanikisha hili.

Hivyo, baada ya kuzaa yafaa kuwekeza muda na nguvu katika kulea, kulea ni pamoja na kuwekeza katika mahitaji muhimu kama vile lishe bora, afya, elimu, ulinzi na hata maji safi na salama kwa watoto.

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasisitiza kuwa, ili kumwezesha mtoto kukua mathalani kiakili ili kimo na weledi wa mambo vikue sambamba basi wazazi hawana budi kuwekeza muda wao katika malezi bora ya watoto. Endelea;


1.Mtoto sina mikono,
Wazazi ndiyo mikono,
Mwendo wangu konokono,
Kufika hadi nibebwe.

2.Huko nasema nyumbani,
Ni kwa wazazi nyumbani,
Najilaza kitandani,
Kuishi hadi nibebwe.

3.Kama nimeshikwa njaa,
Chakula hakijajaa,
Wazazi wanaandaa,
Kula ni hadi nibebwe.

4.Sifikirii chochote,
Nyumbani napata vyote,
Vinginevyo hali tete,
Hebu niache nibebwe.

5.Shule zikifunguliwa,
Mahitaji nagawiwa,
Bila hata kuchelewa,
Hebu niache nibebwe.

6.Sare zote ninapewa,
Jinsi ninafikiriwa,
Vizuri naandaliwa,
Hebu niache nibebwe.

7.Mimi ninafurahia,
Mungu anifikiria,
Maisha nafurahia,
Hebu niache nibebwe.

8.Wako wenzangu walia,
Jinsi walivyofulia,
Nani awasaidia?
Hebu niache nibebwe.

9.Wengine walizaliwa,
Kisha ndipo liambiwa,
Wazazi likatiliwa,
Hebu niache nibebwe.

10.Wengine wanakumbuka,
Kwa wazazi walideka,
Na mara wakaondoka,
Hebu niache nibebwe.

11.Tena watoto wengine,
Maisha ni kivingine,
Hebu waache wanune,
Huku na mimi nibebwe.

12.Kweli kwetu ni neema,
Ambayo inasimama,
Kupata baba na mama,
Hebu tuache tubebwe.

13.Wazazi wanapendana,
Wanacheka tunaona,
Hakuna kuvurugana,
Hebu tuache tubebwe.

14.Wengine tunasikia,
Jinsi chozi wanalia,
Amani imeishia,
Hebu niache nibebwe.

15.Watoto kwetu Amani,
Nyumbani hata shuleni,
Yazidi yote madini,
Hebu niache nibebwe.

16.Kupigwapigwa hapana,
Hatutaki kutesana,
Inakuwa raha sana,
Hebu niache nibebwe.

17.Sasa na mimi mtoto,
Naushika ule wito,
Nizidi kupata joto,
Hebu niache nibebwe.

18.Wazazi walezi pia,
Sisi twawafurahia,
Tena tunajivunia,
Hebu tuache tubebwe.

19.Jinsi mwatuangalia,
Na kutushughulikia,
Kweli tunafurahia,
Hebu tuache tubebwe.

20.Yetu mnafwatilia,
Pia kutusaidia,
Maisha twafurahia,
Hebu tuache tubebwe.

21.Mungu wetu wa mbinguni,
Azidi wapa Amani,
Nyumbani pia kazini,
Sisi tuache tubebwe.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news