UAE yatoa dola milioni 100 kusaidia maafa ya tetemeko Syria na Uturuki

ABU DHABI-Umoja wa Falme za Kiarabu umeahidi kutoa dola milioni 100 kwa Syria na Uturuki, ikiwa ni kiasi kikubwa cha fedha ambazo zitatolewa kufuatia tetemeko kubwa la ardhi lililoua zaidi ya watu 5,400 katika nchi zote mbili.

Picha na thehill.

Taifa hilo lenye utajiri mkubwa wa mafuta eneo la Ghuba ambalo tayari lilikuwa limeahidi dola milioni 13.6 kwa Syria linaongoza juhudi za kikanda za misaada, baada ya kutuma ndege kwa nchi zote mbili, misaada na timu za uokoaji kufuatia tetemeko lenye ukubwa wa vipimo vya Ritcher 7.8 lililotokea mapema Jumatatu.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Emirates, siku ya Jumanne, Rais wa Emarati, Sheikh Mohamed bin Zayed Al-Nahyan aliamuru kutolewa kwa dola milioni 100 kwa ajili ya kuwaokoa walioathirika katika mataifa hayo mawili.

Kiasi hicho kitagawanywa kwa usawa kati ya Syria na Uturuki, huku kila moja ikipata dola milioni 50, kulingana na shirika hilo la habari.

Haijabainika mara moja ikiwa fedha za Syria zilijumuisha dola milioni 13.6 zilizotangazwa hapo awali. Meja Jenerali Saleh Al-Ameri, kamanda wa operesheni za pamoja katika Wizara ya Ulinzi ya UAE, alisema Jumanne kwamba ndege tatu za kijeshi zilitumwa Uturuki, zikiwa na timu za utafutaji na uokoaji ambazo zimeanza operesheni.

"Jumla ya safari saba za ndege zimepangwa kuelekea nchi zilizokumbwa na tetemeko hilo, zikiwemo mbili za kuelekea mji mkuu wa Syria wa Damascus,"Meja Jenerali huyo aliviambia vyombo vya habari vya ndani.

Shirika rasmi la habari la Syria la SANA lilisema Jumanne kwamba, ndege ya Emarati iliyobeba tani 10 za chakula iliwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Damascus.

UAE ilifungua tena ubalozi wake katika mji mkuu wa Syria mnamo Desemba 2018.
 
Mwezi Machi mwaka jana, Rais wa Syria,Bashar Hafez al-Assad alifanya ziara UAE ikiwa ni mara yake ya kwanza katika taifa la Kiarabu katika zaidi ya muongo mmoja wa vita ambavyo vinatajwa vya kikatili vya wenyewe kwa wenyewe.(DIRAMAKINI)

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news