Waziri Dkt.Mabula:Mnapanga nini? Hii haiwezekani,ni marufuku kwa halmashauri zote

NA MUNIR SHEMWETA-WANMM

WAZIRI wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt.Angeline Mabula amepiga marufuku ubadilishaji matumizi katika halmashauri nchini usio na tija.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt.Angeline Mabula akioneshwa ramani ya lililokuwa shamba la NARCO Gezaulole Kata ya Somangila Manispaa ya Kigamboni jijini Dar es Salaam alipofanya ziara katika eneo hilo Februari 14, 2023. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni Halima Bulembo.

Dkt.Mabula alipiga marufuku hiyo alipotembelea eneo lenye mgogoro lililokuwa shamba la NARCO Gezaulole Kata ya Somangila Manispaa ya Kigamboni jijini Dar es Salaam tarehe 14 Februari 2023.

Amesema, kumekuwa na tabia ya kubadilisha matumizi usio na tija alioueleza kuwa unaharibu miji na mipango inayowekwa na halmashauri kupitia mipango kabambe pamoja na yeye kulipiga marufuku mara kwa mara.

Kwa mujibu wa Dkt.Mabula, ubadilishaji matumizi kwenye maeneo unafanywa na halmashauri husika na utaratibu wowote wa kubadilisha matumizi usiozingatia taratibu unaenda kinyume na mipango miji sambamba na kuharibu miji.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt.Angeline Mabula akiingia kwenye moja ya eneo lenye mgogoro lililokuwa shamba NARCO Gezaulole Kata ya Somangila Manispaa ya Kigamboni jijini Dar es Salaam alipofanya ziara kwenye eneo hilo tarehe 14 Februari 2023. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Halima Bulembo.

Akitolea mfano wa Manispaa Kigamboni. Dkt.Mabula alisema manispaa hiyo inao mpango kabambe ambapo mipango yote katika halmashauri hiyo inatakiwa kuzingatiwa ama kutekelezwa na kushangazwa kabla ya kutekelezwa mpango huo matumizi yanaanza kubadilishwa.

‘’Hapa mnayo master plan inayotakiwa kutekelezwa na haijaanza katika utekelezaji, lakini mnaaza kubadilisha matumizi maana yake katika uandaaji hamkuwa na uhakika mnapanga nini, hii haiwezekani,’’amesema Dkt.Mabula.
Ametaka matumizi ya ardhi katika Manispaa ya Kigamboni kubaki kama yalivyopangwa na kama kuna uhitaji wowote wa lazima basi ni lazima ufahamike kama ni wa mamlaka au ni wa mtu binafsi.

Awali Mbunge wa Jimbo la Kigamboni, Dkt.Faustine Ndugulile alimueleza Waziri wa Ardhi Dkt.Angeline Mabula kuwa, katika jimbo lake kumekuwa na tabia ya ubadilishaji matumizi usio na tija alioueleza kuwa, kwa kiasi kikubwa unachangiwa na baadhi ya watendaji wa sekta ya ardhi.

‘’Hapa Kigamboni kumekuwa na ubadilishaji matumizi na watu wanavamia mpaka maeneo ya public na hili linachangiwa na baadhi ya watendaji wa sekta ya ardhi hili nakuomba Mheshimiwa Waziri ulipige marufuku,"amesema Dkt Ndugulile.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt.Angeline Mabula akisisitiza jambo kwa viongozi wa Wilaya ya Kigamboni mara baada ya kumaliza kutembelea eneo lililokuwa shamba NARCO Gezaulole tarehe 14 Februari 2023. Wa pili Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Halima Bulembo na kulia ni Mbunge wa Kigamboni, Dkt.Faustine Ndugulile. (Picha na WANMM).

Dkt.Mabula alitembelea eneo ya lililokuwa shamba la NAFCO Gezaulole Kata ya Somangila Manispaa ya Kigamboni baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi wa eneo hilo kuwa, eneo hilo limeingia mgogoro na baadhi ya wananchi kwa madai kumiliki kihalali eneo hilo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news