WAZIRI MKUU ASEMA RAIS DKT.SAMIA ANATEKELEZA ILANI KWA VITENDO

NA MWANDISHI WETU

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuwatumikia wananchi na kwamba ilani ya uchaguzi ya 2020 inatekelezwa.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa akizungumza katika Maadhimisho ya Miaka 46 ya CCM yaliyofanyika kimkoa kwenye uwanja wa Umoja uliopo Kasulu Mkoani Kigoma, Februari 4, 2023. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

“Chama kipo imara na kinaendelea kuwatumikia wananchi kupitia ilani ya uchaguzi ambayo inatekelezwa kwa mafanikio makubwa, hivyo kila Mkuu wa Idara aone kilichoandikwa kuhusu eneo lake na atengeneze mpango kazi wa kuyatekeleza yaliyoahidiwa kwenye ilani hiyo.”

Mheshimiwa Majaliwa ameyasema hayo leo Februari 4, 2023 wakati wa maadhimisho ya Sherehe za Miaka 46 ya CCM Mkoa wa Kigoma. Maadhimisho hayo kimkoa yamefanyika katika Uwanja wa Umoja wilayani Kasulu.

Amesema katika kipindi cha miaka miwili ya Serikali ya awamu ya sita, Mheshimiwa Rais Samia na Mwenyekiti wa CCM Taifa amefanikiwa kuboresha sekta mbalimbali zikiwemo uchumi, elimu, afya, maji, miundombinu, nishati, utalii pamoja na kuimarisha ushirikiano wa Kimataifa.

Pia, Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini na kuwa kivutio cha wawekezaji kutoka mataifa mbalimbali, ambapo amesema namna pekee ambayo Watanzania wanaweza kumuunga mkono Mheshimiwa Rais Dkt. Samia ni kufanya kazi kwa bidii, weledi na uaminifu.

Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa amesema mbali na kuimarisha sekta hizo, Mheshimiwa Rais Samia anaendelea kuimarisha Muungano pamoja na kuboresha maslahi ya watumishi wa umma nchini ili waendelee kuwatumikia wananchi katika maeneo yote.

Awali, Mheshimiwa Waziri Mkuu alizindua ugawaji wa kadi za kielektroniki kwa mkoa wa Kigoma kwa kugawa kadi hizo kwa wanachama wapya 400 wa CCM wa wilaya ya Kasulu. Katika maadhimisho hayo Mkoa umefanikiwa kupata wananchama wapya 2,162 waliojiunga na Chama hicho.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Kigoma, Jamal Tamim alisema CCM imefanya mambo mengi tangu kuanzishwa kwake ikiwemo utoaji wa elimu ambapo awali elimu ya sekondari ilikuwa changamoto kwa watu wengi kutokana na uhaba wa madarasa licha ya kufaulu elimu ya msingi. “Kwa sasa shule ni nyingi ila nashangaa kwa nini wazazi hawapeleki watoto shule.”

Naye, Mbunge Kasulu Mjini na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Profesa Joyce Ndalichako amemshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia kwa kusimamia vyema utekelezaji wa Ilani na jimbo la Kasulu limefanikiwa kupata miradi mbalimbali ya elimu, afya, maji, barabara na kilimo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news