SIMULIZI YA KUTISHA KATIKA MAISHA-4

NA WILLIAM BOMBOM

Ilipoishia... Kwa umri huo alikuwa na uwezo wa kusonta kitu kikabadilika katika umbo alilolitaka. Mtoto huyo alikuwa na nguvu za ajabu japo walimu na jamii hawakulijua hilo.

Endelea

"Habari za mchana bwana THE BOMBOM? Mazungumzo yao yalianza kwa salamu huku mzungu huyo akitumia lugha fasaha ya Kiswahili. "Salama kidogo" lilikuwa jibu fupi kutoka kwa mtoto THE BOMBOM huku akiwa amejaa hasira na kisirani.

"Kwa nini iwe salama kidogo badala ya salama kabisa?" Mzungu yule aliongeza swali akiwa amekusudia kuandeleza maongezi na mtoto huyo. "Natumaini unajua kwa nini ni salama kidogo" mtoto huyo alijibu swali hilo la mzungu kwa mkato zaidi.

Wahenga walisema "Nyota njema huonekana asubuhi" kwa hili hawakukosea hata kidogo. Namna maongeze yalivyoanza, tayari yule mzungu alikuwa ameshabaini kuwa maongezi yao yasingefika mbali maana mtoto THE BOMBOM alionekana kuwa na hasira.

Kupitia muda mfupi huo, mzungu alikuwa amebaini pia nguvu za ziada zilizokuwa mwilini mwa mtoto THE BOMBOM.

Kimya kirefu kilipita wakiwa kimya, haikuwa kawaida kwa mtoto huyo kuwa katika hali aliyokuwa nayo kwa siku hiyo.

Siku zote alionekana mchangamfu, mcheshi na mwenye furaha awapo na wageni waliokuja kumhoja. Kumbe alikuwa ameshabaini jambo kwa mzungu huyo kupitia nguvu alizokuwa nazo mtoto huyo.

Kho! Kho! Khooooo! Alikohoa kidogo mtoto huyo kisha akaanza kuzungumza. "Nawachukia sana ninyi wazungu kwa unafiki mnaoufanya Afrika. Hivi Waafrika tumewakosea nini? Kwa nini mnatufanyia unyama wa namna hiyo?.

Yalikuwa ni maswali mazito yaliyotoka kwa mtoto huyo mwenye umri wa miaka minne aliyekuwa akisoma darasa la sita.

Alichokuwa akiuliza mtoto THE BOMBOM yule mzungu alikuwa akikifahamu vyema, akaamua kukwepa kujibu "Hakika sifahamu kitu chochote unachotulaumu sisi wazungu, mbona tumewafanyia mambo mengi Waafrika!. 

Tumetumwa na Mungu kueneza imani yetu dunia nzima ili watu wamujue kisha waenende kwenye njia bora!. Ni mambo yapi mabaya ambayo tumewafanyia? Unafiki wetu uko wapi?" Alihitimisha maongezi yake kwa kumtupia maswali mtoto THE BOMBOM.

Kwa wakati huo macho ya yule mtoto yalikuwa yamebadilika rangi na kuwa mekundu mithili ya pilipili kichaa. "Wewe si Padri bali ni mchawi mkubwa, unautumia Upadri kufichia mambo yako. Mmeshiriki kwa kiasi kikubwa kuua dini za kiafrika ambazo zilikuwa za kweli na haki.

Kwa nini mlibadili dini za kweli za pale Kemet na kuzifanya za kwenu? Utatu mtakatifu, Mungu baba, Mungu mmoja, Bikra Maria asili yake ilikuwa wapi? Siyo Kemet? Nakuuliza siyo Kemet?.

Wakati mtoto huyo akizungumza ghafla kulitokea kimbunga kikubwa kilichokuwa kikizunguka maeneo ya shule. Haikujulikana ni wapi kimbunga hicho kulitokea, maeneo yote ya shule yalifunikwa na upepo.

Mabati ya shule yalisukwasukwa kwa nguvu, uchafu na makaratasi yalipeperushwa juu. Ikawa hekaheka kwa muda wa dakika kadhaa, upepo huo haukuja kwa bahati mbaya bali ulikusudiwa.

Hapa nizungumze kidogo, ndugu msomaji siyo kila mzungu anayehubiri neno la Mungu ni muumini wa neno hilo. Wengi wao wana shughuli ama binafsi au wametumwa na taasisi toka nchini mwao.

Wapo wanaofanya biashara za dawa Za kulevya, wapo wanaochunguza madini yetu, wengine wanashiriki kueneza tamaduni zao za kishenzi kama ushoga na usagaji kwa mgongo wa dini.

Wengi wao huja Afrika kujifunza uchawi wetu kisha kuutumia kwao, wengine wanafanya biashara za viungo vya binadamu kwa njia za kishirikina wakiwa wamejifichia kwenye dini.

Hata huyu mzungu alikuwa ni mshirikina mkubwa aliyetoka nchini kwao kuja kujifunza uchawi wa Afrika upande wa kabila la Wasukuma.

Tayari mtoto THE BOMBOM kwa kuwa alikuwa ni mchawi mkubwa aliyekuwa ametabiriwa katika vitabu mbalimbali vya dini za kichawi, haikumuwia vigumu kumtambua mzungu huyo.

Katika dini zote za kichawi utabiri juu ya kuzaliwa kiongozi mkubwa wa kichawi ulifahamika, mbaya zaidi kiongozi huyo alitabiriwa kuzaliwa eneo la Afrika.

Hii kidogo iliwaumiza wazungu, wachawi wa kichina na mataifa mengine. Kwao haikuwa taarifa nzuri hata kidogo, walitaka mambo yote mazuri yatokee kwenye nchi zao.

Waliweka ajenda ya kumuua mtoto huyo pindi atakapozaliwa. THE BOMBOM alikuwa kazaliwa katika jamii ya kifugaji, tena nchi ya Tanzania mkoa wa Mwaza katika wilaya ya Magu.

Sifa za mtoto huyo zilikuwa zimeanza kueneo ndani na nje ya nchi, wawakilishi mbalimbali wa makampuni ya kichawi walianza kumiminika Tanzania kutaka kuhakikisha utabiri huo. Kupitia mazungumzo hayo, yule mzungu alikuwa ameamua kuleta kimbunga ili ampime mtoto huyo.

Ndani ya kimbunga hicho kulikuwa na wachawi waliokuwa wameitwa na Padri huyo kuja kufanya shughuli maalumu. Yule mtoto alibaini hilo kisha akashika kidole chake kidogo cha kulia harafu akaking'ata.

Wale wachawi waliokuwa ndani ya kimbunga walidondoka chini wakiwa uchi wa mnyama. Walikuwa ni Waafrika halisi wakishirikiana na mzungu huyu katika uchawi wao. Lengo lao ilikuwa ni kumuua yule mtoto kulingana na namna walivyoelekezwa na Padri ili kuzima ndoto za Afrika.

Bila kupoteza muda yule mtoto alitema mate ardhini, kile kimbunga kikatulia kukawa kama ilivyokuwa awali. Wale wachawi wanane waliokuwa wamekuja na kimbunga waliendelea kugalagala pale chini wakiwa hoi, hawakuwa na namna ya kujinasu kutoka kwenye ile dhahama.

Pale shuleni walimu na wanafunzi hawakutambua kilichokuwa kikiendelea, wao waliona kimbunga kile kilikuwa cha kawaida.

Hata wale wachawi wanane waliokuwa wameanguka pale chini hawakuonekana kwa macho ya kawaida. Walionekana katika umbo la karatasi kama karatasi zingine zilizokuwa zimeletwa na kimbunga.

Kitendo cha kimbunga kukoma na wale wachawi kudondoka chini, kilimfanya yule mzungu kuanza kutetemeka. Yule mtoto THE BOMBOM alimuamuru mzungu huyo kuondoka haraka eneo hilo.

Mzungu aliamka na kuanza kutembea haraka huku akiwa kashikilia vifaa vyake. Hakupata hata muda wa kuwaaga walimu, aliondoka haraka haraka kwa mwendo ulioleta shaka kwa kila mmoja pale shuleni.

Baada ya mtoto THE BOMBOM kuona yule mzungu ameondoka, alisimama kisha akaziokota zile karatasi na kuzitia mfukoni mwake.

Hakuna hata mtu mmoja aliyebaini kuwa karatasi zile walikuwa ni binadamu katika maumbo hayo. Aliingia darasani kwake na kuwakuta wanafunzi wengi wakimsubiria kwa hamu.

Mashikolo alikuwa ni rafiki mkubwa wa THE BOMBOM, baada ya kumuona rafiki yake alimkimbilia na kumkumbatia kisha wakaenda kukaa nyuma kabisa ya darasa. Masomo yaliendelea mpaka muda wa saa nane kamili, baada ya hapo wanafunzi walitawanyika na kurejea makwao.

Kutoka shuleni kuelekea nyumbani kwao mtoto huyo, kulikuwa na umbali kidogo. Ilikuwa ni lazima akatishe barabara iendayo Musoma kisha aifuate barabara iendayo Kijiji cha Inala.

Kutoka barabarani hadi kwao kulikuwa na mbuga na vichaka kadhaa. Kwa mwanafunzi wa umri wake ilikuwa ni hatari sana kupita maeneo hayo.

Nyuma ya pazia hakuna hata mtu mmoja aliyekuwa akijia mtoto huyo alikuwa akipita namna gani maeneo hayo na kufika nyumbani kwao.

Alianza safari ya kurejea kwao, mara nyingi huwa anajibadili na kuwa upepo. Lakini kwa siku hiyo aliamua kutembea kwa miguu akiwa kwenye uhalisia wake.

Mfukoni alikuwa amewabeba wale wachawi. Alipotokeza kwenye uanda aliwaona kundi la wachawi wakiwa wamesimama na Padri yule mzungu.

Ndugu msomaji unadhani nini kitampata mtoto THE BOMBOM? Mambo ndiyo yanaanza kuiva, usikose kusoma sehemu inayofuata.

YA WIZA HENE?

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news