UNACHOFANYA SAMIA, KOFIA TWAKUVULIA

NA LWAGA MWAMBANDE

LEO Machi 8, 2023 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mheshimiwa Dkt.Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mkutano wa Baraza la Wanawake wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo-CHADEMA (BAWACHA) ikiwa ni Siku ya Wanawake Duniani.

Hayo yalibainishwa hivi karibuni na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa, Mheshimiwa Freeman Mbowe alipofanya mahojiano na mwandishi wa Habarileo, akieleza kuwa alimuomba Rais Dkt.Samia naye ameridhia ombi hilo.

“Siku zote anawasikiliza wakina mama wa chama chake, tulimuomba aje awaone atambue kazi kubwa inayofanywa na akina mama wa CHADEMA, kwa hiyo Rais atakuwa mgeni rasmi katika tukio letu na mimi nitakuwepo kumpokea,” alisema Mbowe.

Mheshimiwa Mbowe alieleza kuwa, mkutano huo utafanyika mkoani Kilimanjaro na kuhudhuriwa na wanawake wa vyama mbalimbali vya siasa nchini.

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema, hatua hizi za Mheshimiwa Rais Dkt.Samia zinadhirisha ni kiongozi mwenye kujali watu wake, mlezi na mshauri mwema ambaye anaamini zaidi katika umoja, mshikamano na maridhiano kwa ustawi bora wa Taifa. Endelea;


1.Kwamba mbele ya BAVICHA, mgeni Mama Samia,
Tanzania kumekucha, siasa zake Samia,
Rais wetu ni kocha, wa siasa Tanzania,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

2.Siasa tunazipiga, twabaki Watanzania,
Hata zikituvuruga, hapahapa twasalia,
Hizi za Samia swaga, twapaswa kushangilia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

3.Yeye Mgeni Rasmi, kwa wapinzani wa nia,
Walokuwa hawasemi, ngumu ngumu wajitia,
Sasa aenda kitemi, katikati aingia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

4.Hii miaka miwili, kafanya mengi Samia,
Kutoka dhofli hali, watu wanafurahia,
Lakini hili ni ghali, ni raha kulisikia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

5.Tangu alipoingia, kama Rais Samia,
Pazuri alianzia, nchi kutufungulia,
Ni ndani alianzia, hadi nje kafikia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

6.Wale waliotitia, yeye liwafungulia,
Mikutano kuzuia, amekwishafungulia,
Hao awaangalia, huko akiwafikia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

7.Wapinzani angalia, Mama wamfurahia,
Mengi anawafanyia, yale yaliyofifia,
Bavicha kawasikia, aenda wasalimia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

8.Hata waliokimbia, hatari lizowajia,
Wamekwishajirudia, siasa wajifanyia,
Kafanikisha Samia, heko tunammwagia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

9.Hongera Mama Samia, Rais wa Tanzania,
Sasa twakuaminia, pazuri tunafikia,
Bavicha kuwafikia, wapate kushangilia?
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

10.Tusichukulie poa, anayofanya Samia,
Yanatufuta madoa, nchi yetu Tanzania,
Uhasama yaondoa, sote ni Watanzania,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

11.Sasa tunasubiria, tupate kumsikia,
Atakayotuambia, atapotuhutubia,
Kombe tunampatia, mchezo kajishindia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

12.Ni siku ya wanawake, macho yote kwa Samia,
Ni Rais mwanamke, wa kwanza kwa Tanzania,
Acha alama aweke, tutazidi simulia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

13.Rais Samia heko, unavyotuhudumia,
Tulio huku na huko, sote twakufurahia,
Kwa vile huko uliko, nasi watuangalia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

14.Karibu Kilimanjaro, huko twakusubiria,
Na walio Kilombero, wote takufwatilia,
Sema uondoe kero, zile zinatuzidia,
Unachofanya Samia, kofia twakuvulia.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news