Wabaini vitendo vya ulawiti, usagaji na ubakaji shuleni, RC afunguka mazito

NA MWANDISHI WETU

MKUU wa Mkoa wa Katavi, Mhe. Mwanamvua Mrindoko ametoa wito kwa wananchi wote katika mkoa wake kujitokeza kukemea na kulaani vitendo vya ukatili vinavyofanywa na baadhi ya watu dhidi wanafunzi wa shule katika Wilaya ya Mpanda.

Amesema hayo kufuatia uchunguzi wa awali uilofanywa na vyombo vya usalama kuwa kuna ufanyikaji wa mapenzi kinyume na maumbile yaani ulawiti, usagaji na ubakaji katika baadhi ya shule za msingi na sekondari, vituo vya shule ya awali na vya kulelea watoto yatima katika wilaya hiyo.

Mheshimiwa Mrindoko amefafanua kuwa, mapenzi hayo yanawahusisha wanafunzi kwa wanafunzi, baadhi ya walimu na wafanyakazi wanafanya na wanafunzi, baadhi ya watu wazima waliopo mtaani wanafanya mapenzi ya aina hiyo na wanafunzi.

Kwa masikitiko makubwa, Mhe. Mrindoko amesema, katika uchunguzi huo ipo orodha ndefu inayoonyesha kuwa kuna ukiukwaji mkubwa wa maadili ndani ya taasisi zake ambazo jamii ina tegemea kuwafundishia watoto wake.

Amesema, imebainika kuwa kuna mabweni bubu na shule za msingi binafsi na vituo vya kulelea watoto ambavyo havina vibali na ameagiza kufungwa shule hizo.

Mhe. Mrindoko ameitaka jamii, wazazi au walezi na wananchi wote mkoani kwake kupaza sauti ‘kukataa ulawiti, usagaji na ubakaji katika mkoa wake.

"Tusipokemea haya watoto wetu wataendelea kuharibiwa na ukatili utaenea katika mkoa wetu. Tushirikiane kukemea na kuwaelimisha watoto na vijana wetu kwamba mambo hayo siyo utamadauni wetu wala maelekezo ya mwenyezi mungu na hayapo sehemu yoyote duniani na hayana uhalali wowote ule.

Jambo lolote la namna hiyo likitokea sisi wananchi katika ngazi ya familia/ukoo, tusinyamaze, tusikae kimya, tulifikishe kwenye vyombo vya sheria na hatua zichukuliwe dhidi ya watu wote wanaojihusisha na uhalifu huo.

Viongozi wa dini tuwatangazie waumini kuhusu maovu hayo na madhara yake kwa jamii nao pia wayakemee kwa nguvu zote.

Ukaguzi wa shule ufanyike mara kwa mara na hatua zichuliwe dhidi ya shule zinazokiuka maadili na sheria za sekta ya elimu nchini. Tume ya utumishi wa walimu ifanye uchunguzi wa kina kuhusu walimu wanaojihusisha na utovu wa nidhamu mashuleni na kuwachulia hatua za kinidhamu.

Jeshi la Polisi katika Mkoa wa Katavi liimarishe madawati ya wanawake na watoto na kuwachukulia hatua za kisheria watu wote wanaojihusisha na vitendo vya ukatili dhidi ya watoto au wananfunzi,"amefafanua.

Mhe.Mrindoko ameyasema hayo katika Wiki ya maandalizi kuadhimisha siku ya wanawake inayotarajiwa kuadhimishwa katika viwanja vya Mpanda ndogo wilayani Tanganyika.

Miongoni mwa shughuli zinazoendelea kufanyika kabla ya kilele cha maadhimsho hayo, ni pamoja na kutoa elimu ya lishe, rushwa na kupinga ukatili, kupanda miti, kutembelea vituo vya yatima na kutoa misaada, kuendesha kongamano,maonyesho na mabonanza

Kauli mbiu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani 2023 ni ‘Mawazo ya ujasiri yenye kuleta teknolojia jumuishi,ubunifu, elimu inayoweza kupambana na ubaguzi na kutengwa kwa wanawake duniani kote'.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news