UTAJUA UMEOA:Mwanaume ukioa, wewe oa kwelikweli

NA LWAGA MWAMBANDE

KILA mmoja wetu anatambua kuwa, ndoa ni muungano kati ya mwanamke na mwanamume kuishi pamoja kama mume na mke muda wote wa maisha yao kulingana na Kifungu cha 9 (1) cha Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971.

Aidha, kulingana na Kifungu cha 10 cha Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971, kuna aina mbili za ndoa, mosi ni ndoa ya mke mmoja, hii ni ndoa ambapo mwanaume ana mke mmoja tu, mfano ndoa za Kikristo.

Pia, kuna ndoa ya wake wengi, hii ni ndoa ambayo mwanaume ana wake zaidi ya mmoja, mfano ndoa za Kiislamu na kimila.

Ndoa hizo zinaweza kufungwa kwa kufuata taratibu za kidini, kiserikali au kimila. Utaratibu huo utafuata au kuzingatia kama wanandoa ni waumini wa dhehebu au la. Kulingana na Kifungu cha 25 cha Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971, kuna aina tatu za ufungaji wa ndoa.

Mosi,ndoa ya kidini, hii hufungwa kwa mujibu wa taratibu ya dini husika kama ni Kikristo, Kiislamu au dhehebu la wahusika katika ndoa.

Jambo la msingi ni lazima masharti yote yatimizwe kisheria na taarifa ya nia ya kufunga ndoa itolewe na ndoa ifungiwe mahali pa wazi panapokubalika kisheria na mfungishaji awe na mamlaka hayo kisheria.

Pili,ndoa ya kiserikali,hii hufungwa mbele ya mkuu wa wilaya ambaye ndiye Msajili wa Ndoa na wanandoa wanaokusudia kuwa na ndoa ya kiserikali. Ndoa itafungiwa katika Ofisi ya Msajili (mara nyingi hufungwa bomani kwa mkuu wa wilaya) au mahali pengine popote palipotajwa katika leseni yake ya kufungisha ndoa.

Tatu ni ndoa ya kimila,hii inaweza kufungwa kimila iwapo mmoja wa wafunga ndoa au wote wawili wanafuata sheria za mila za kabila fulani.

Aidha, mwandishi wa ndoa za kimila ni Katibu Tarafa (Afisa Tarafa) wa eneo husika ambako ndoa ya kimila inakwenda kufungishwa.

Ndoa ya kimila hufungishwa na mtu anayetambulika kimila kuwa ana uwezo huo. Ni muhimu sana Katibu Tarafa kuhudhuria kwenye ufungishaji huo wa ndoa, kwani ndiye atakayehusika na kupeleka vyeti vya ndoa kutoka kwa msajili.

Wakati huo huo, ukipitia katika Sheria ya Ndoa mwaka 1971 kifungu cha 9.Wanaooana wawe wamekubaliana pasipo kulazimishwa na mtu. Ndoa ni ya mwanamke na mwanamume, ni ndoa ya kudumu maishani.

Vivyo hivyo, mpango na utaratibu wa Mungu kwa wanandoa umewekwa wazi, rejea Biblia Takatifu kitabu cha Mwanzo 2:18, " “Bwana Mungu akasema si vema mtu huyu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufafana naye”.

Pia, rejea Mathayo 19:3-6...3-"Basi Mafarisayo wakamwendea, wakamjaribu, wakimwambia, Je! Ni halali mtu kumwacha mkewe kwa kila sababu?.

4-Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke,
5-akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja?.

6-Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe." Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasisitiza kuwa, mwanaume ukioa, wewe oa kweli kweli. Endelea;


1.Mwanaume ukioa, wewe oa kwelikweli,
Kile kiapo cha ndoa, kiwe kamilikamili,
Wakati wa mambo poa, na hata hali dhalili,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

2.Ni baba wa kwenye ndoa, ndiye amenena hili,
Ni wakati anatoa, shukrani kwa Jalali,
Mungu alivyomwokoa, kwenye ugonjwa wa mwili,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

3.Ni mgonjwa ameoa, imekuwa mbaya hali,
Mke aliyemuoa, yuko naye kila hali,
Ndio hapo akatoa, neno kwa wake halali,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

4.Kama vema umeoa, mke aliye kamili,
Nenda shukrani toa, jambo kubwa sana hili,
Kwa sababu hiyo ndoa, una amani ya kweli,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

5.Kuwe heri kwenye ndoa, huwezi ona dalili,
Hakuna kujiondoa, mwafaidi vya halali,
Kunapotokea doa, hapo utajua kweli,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

6.Wanaume kwenye ndoa, huweza gundua hili,
Kwamba wake zao poa, au sawa na mbigili,
Wale wanajiondoa, shida kwao siyo dili,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

7.Hapo jua umeoa, ni maumivu makali,
Utashindwa kusogoa, unaishi na jangili,
Ni jicho umechongoa, nyumbani ni shida kweli,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

8.Ila yupo kwenye ndoa, ni mwanawake kamili,
Hata kutokee doa, anabaki wa ukweli,
Shida raha yuko poa, anaijulia hali,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

9.Unapotaka kuoa, kijana omba Mungu kweli,
Huyo utakayeoa, awe mke kwelikweli,
Mambo poa na madoa, mshikane mkisali,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

10.Binti anayekuoa, ni mtu siyo kamili,
Anayo madoadoa, mepesi hata aghali,
Jitoe ya kujitoa, mengine nenda na hali,
Changamoto ikifika, utajua umeoa.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news