Dawa za kulevya haziwezi kukuacha salama-Dkt.Mfisi

NA GODFREY NNKO

KAMISHNA wa Kinga na Tiba kutoka Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Dkt. Peter Mfisi amesema, moja wapo ya sababu ya wanaosafirisha dawa za kulevya kukamatwa nchi nyingine na sio Tanzania wanapoanzia safari ni kutokana na kutaka kupata taarifa za kina kuhusu anayepelekewa.

Dkt.Mfisi ameyasema hayo leo Mei 29, 2023 wakati akifanya mahojiano maalum na UTV ya jijini Dar es Salaam kutokea jijini Dodoma.

"Si wote wanaomeza hapa wanatoka, wanapakiwa kutoka nje kuna wengi tu tunawakamata hapa na pale Airport tuna kitengo kabisa cha kudhibiti dawa za kulevya ambapo kiasi kikubwa tu wanakamatwa na hawafanikiwi kuzipeleka huko nje.

"Lakini wakati mwingine unaweza ukakuta kabisa tunajua kuwa huyu mtu kabeba dawa za kulevya, lakini tunataka kujua anampelekea nani huko nje hizo dawa. Kuna kitu kinaitwa 'Control Delivery' kwa hiyo ninyi mnajua, mkishajua mnawapigia wenzenu huko nje.

"Kwa mfano, anakwenda India, Hongkong mnawaambia kuna mtu huyu amebeba dawa, lakini tunachotaka kujua sisi tunataka kujua anampelekea nani. Kwa hiyo wale kule Airport wanamuona wanaanza kumfuatilia, kwa hiyo anakutwa na huyo anayepokea hizo dawa wanakamatwa kwa pamoja wote.

"Kule sisi tunawasiliana tunaacha afike kule kama alivyokuwa anasema Marwa wanasafiri kilomita 40 ili waanze kuzitoa zote zile dawa sasa anakamatiwa kule na yule anayepokea hizo dawa,"amefafanua Dkt.Mfisi.

Wakati huo huo, Dkt.Mfisi amebainisha kuwa, ingawa ni changamoto kubwa kumbaini mtu aliyebeba dawa za kulevya, mamlaka hiyo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wanashirikiana kuhakikisha hakuna anayefanikiwa kupitisha au kuingiza dawa hizo hapa nchini.

"Lakini suala la kumjua mtu amebeba dawa za kulevya sio rahisi sana, kwa sababu kuweza kuanza kum-suspect na kum-subject kwenye X-ray kila mtu anayepita Airport. Lazima muwe na taarifa za kiintelejensia na mmemhisi mtu kwa kiasi kikubwa ndio mnaweza mkam-suspect, mkamsubject kwenye X-ray na kumkamata.

"Lakini tunahitaji taarifa zaidi za kiintelejensia kujua kama mtu fulani au watu fulani wamebeba dawa za kulevya. Lakini sio kila msafiri aende apigwe x-ray inaweza kuwa ngumu.

"Kwa sababu ili uweze kusafirisha kwa mfano unatoka Dar es Salaam unakwenda Australia unaweza ukakuta safari ukiunganisha inachukua masaa (saa) 20. Sasa kwa masaa hayo hutatakiwa kwenda haja kubwa kwa sababu utazipoteza hizo dawa."

Aidha, Dkt.Mfisi anasema, wasafirishaji wote wa dawa za kulevya kwa njia za kumeza huwa wanakuwa waraibu kwa baadae.

"Wanalazimika kulamba dawa kidogo kwa sababu ukitumia hiyo dawa ya kulevya hasa heroine huwa inakufanya mtu ufunge choo, kwa hiyo wanalamba dawa ili kutoenda choo kusudi wafikishe hiyo dawa wanakopeleka.

"Kwa hiyo, muda mwingi walio wengi wanabadilika wanakuwa watumiaji na waraibu na kupelekea ndoto zao zote zinakwisha. Haya yote hawaambiwi,lakini wanapokuwa wanatengenezwa hawaambiwi kabisa kwamba watakuwa waraibu.

"Sisi (DCEA) tunajitahidi sana kwenye kinga, tunatoa elimu kama sasa hivi tunapenda kutoa elimu kwenye level (ngazi) za chini kabisa katika shule za msingi na sekondari.Tunataka mpango wa kuanzisha klabu kwenye shule zote za msingi na sekondari na vyuo hapa Tanzania.

"Mei 26, 2023 tulifanya mkataba na wenzetu wa TAKUKURU (Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU) kwamba Klabu zilizokuwa zinaitwa Klabu za Kuzuia Rushwa zitaitwa Klabu za Kuzuia Rushwa na Dawa za Kulevya. Tutakuwa tunatoa elimu kwenye shule zote za msingi na sekondari, hatua hiyo tunaamini itaweza kuwafikia Watanzania wengi zaidi.

"Kwa sababu zaidi ya asilimia 98 ya Watanzania wanapitia kwenye hizi hatua za elimu msingi na sekondari, pia tunatumia socila media kutoa elimu na Tv, Radio kutoa hii elimu. Jamii isijihusishe na hii biashara ya dawa za kulevya na kutumia kwa sababu biashara na matumizi ya dawa za kulevya haijawahi kumuacha mtu salama. mwisho wake ni kupata matatizo makubwa.

"Tunapaswa tuelewe kwamba hao watu wanaouza dawa za kulevya wanakuwa na mkakati wa muda mrefu. Kwa mfano umemsikia Marwa anameza chapati kiasi kikubwa namna hiyo, kwa hiyo wanakuwa wanajua Marwa tumbo lake ni kubwa anaweza akameza kiasi kikubwa cha dawa.

"Ndio maana hata alipokamatwa, wenzake walikuwa wanamlaumu yeye anabeba kiasi kikubwa cha dawa kuliko wenzake. Kwa hiyo yeye tayari walishamfanyia mazoezi na hata alipochukuliwa kwenda kwenye shamba la ng'ombe walikuwa wanampa chakula kingi zaidi bila yeye kujua. Lakini lengo awe na tumbo kubwa atakapokuwa anasafirisha aweze kusafirisha kwa kiwango kikubwa wapate faida kubwa.

"Jinsi gani tunaweza kuwalinda watoto, tunatakiwa sisi wazazi tuwe tunawatahadharisha watoto hata wanapokwenda kwenye michezo kwa mafano mwingine anakwambia anaenda kwenye mpira nchi fulani, lakini huko unaona huwa wanabebeshwa dawa za kulevya tumeshawahi kuona hapa nchini watu walikuwa wanakwenda kwenye mchezo wa ngumi watu wakakamatwa wamebeba dawa.

"Nafikiri kitu cha maana ni kutoa elimu kwa jamii, wewe kama ni mchezaji umeteuliwa kwa ajili ya kucheza usifanye kingine ukifanya kingine ni rahisi kukamatwa. Ukajikuta kabisa unapoteza ndoto zako sisi tunazidi kutoa elimu kwa jamii kuhakikisha kwamba kubeba dawa za kulevya kwa njia yoyoye ile adhabu yake ni kali na watu wasifanye hivyo.

"Kuna baadhi ya nchi zinanyonga, zingine zinafunga maisha kwa mfano hapa Tanzania tunafunga maisha. Sisi tunatoa elimu mtu hata kama anadanganywa inakuwa rahisi kushituka. Kwamba mimi mchezaji wa mpira au ngumi nikisafirisha dawa hizo nikikamatwa nitapoteza ndoto zangu kabisa na sisi rai yetu waache kabisa kufanya hivyo.

"Na kwenye huu ukanda wa Afrika Mashariki dawa zinapita, zinatengenezwa Afghanistan zinapita Pakistan au Iran ambapo sisi tunapakana nao kwa njia ya moja kwa moja ya Bahari ya Hindi. Kwa hiyo dawa zinasafirishwa kutoka Pakistan au Iran kuja mpaka Tanzania, Kenya kwenye hii Pwani ya Afrika Mashariki.

"Zikifika zinapakiwa ndio kina Marwa wanapatikana wanameza wanapeleka Australia, Marekani,Hongkong, Taiwan, kwa hiyo ni kitu cha kweli, lakini tatizo moja hao watu wanaowatengeneza kina Marwa huwa hawawaambii kwamba unaweza ukakamatwa.

"Wakati mwingine dawa zinapasuka tumboni wanakufa na wakati mwingine unaweza wakiwa kwenye hizo nchi kama Marwa alivyosema wenzake walinyongwa na kweli wengine kufungwa kifungo cha maisha.

"Lakini wanaowatengeneza huwa hawawaambii wanawaambia tu wewe tutakukatia tiketi ya ndege, VISA, passport ukifika kule tutakupa pesa. Lakini ukweli wengine wanapata madhara makubwa sana kama kifo zile kete zinapopasuka tumboni,"amesema Dkt.Mfisi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news