Mchakato wa Katiba Mpya wabisha hodi, Rais Dkt.Samia atoa maelekezo

NA DIRAMAKINI

RAIS wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan amemuagiza Msajili wa Vyama vya Siasa Jaji Francis Mutungi, kuitisha kikao maalum cha Baraza la Vyama vya Siasa.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan akiongoza Kikao cha Viongozi mbalimbali wa Serikali kinachohusu kuanza kwa Mchakato wa Katiba mpya, kilichofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 6 Mei ,2023. (Picha na Ikulu).

Lengo ni kuwashirikisha wadau katika kutathmini utekelezaji wa mapendekezo ya Kikosi Kazi kilichokuwa kikiratibu maoni ya watu kuhusu demokrasia ya vyama vingi vya siasa nchini.

Rais Dkt.Samia ametoa maelekezo hayo wakati wa kikao kilichofanyika Ikulu ya Chamwino, kilichohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali kuhusu kuanza kwa mchakato wa Katiba mpya.

Kikao hicho kimejadili namna ya kushirikisha wadau mbalimbali na hasa ushirikishwaji wa wananchi katika mchakato huo kutoka pande zote mbili Tanzania Bara na Zanzibar.

Mbali na mchakato huo wa Katiba mpya, masuala mengine yanayotarajiwa kushughulikiwa ni marekebisho ya sheria mbalimbali zinazohusiana na uchaguzi; zikiwemo Sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi na Sheria ya Vyama vya Siasa.

Miongoni mwa viongozi waliohudhuria kikao hicho ni pamoja na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge) Mhe. Jenista Mhagama, Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro na watendaji wa taasisi mbalimbali.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news