SIMULIZI YA KUTISHA KATIKA MAISHA-30

NA WILLIAM BOMBOM

Ilipoishia...wachawi hao walikuwa wakifanya zindiko la mwisho ili kumchukua mtu mmoja, waliyekuwa wamemloga mtaa huo. Ndugu msomaji unaposikia mbwa wengi wakilia kwa sauti ya kupokezana, kama sauti zao zitakuwa ziki...

Endelea

Zikipanda na kushuka kwa kubembeleza zaidi, tambua hao siyo mbwa wa kawaida ni wachawi. Hili hufanyika katika kukamilisha miiko ya kichawi kabla ya kumchukua mtu huyo.

Pia unapaswa kufahamu kuwa siyo kila mtu anapochukuliwa msukule ni lazima mbwa hao walie namna hiyo, unaposikia kilio cha namna hiyo tambua kuwa ni ishara ya kichawi.

Ishara hiyo huonesha kuwa katika mtaa huo, kuna watu wengi zaidi watachukuliwa muda si mrefu. Ndugu msomaji jaribu kuchunguza kwa kina iwapo mbwa watalia sauti hizo mtaani kwako, kisha subiri siku tatu au nne utajionea mwenyewe.

Vifo hivyo huwa ni vya rika moja au jinsi moja. Kama atakayeanza kufariki atakuwa mtoto basi ndani ya majuma mawili watafariki idadi kubwa ya watoto wa rika hilo.

Iwapo atakayeanza kufariki ni mwanamke wa makamo, basi watakaofuatia wote watakuwa ni wa umri na jinsi hiyo hiyo. Endapo atakayeanza kufariki ni kijana basi watakaofuata watakuwa ni vijana wa rika hilo hilo.

Ninaamini ndani ya jamii mambo hayo huwa mnayaona, jaribu kuchunguza kabla ya mfululizo wa vifo hivyo utabaini mbwa hao walilia kwa sauti za kusikitisha.

Mtoto THE BOMBOM na kundi lake la wachawi walikuwa na uwezo wa kuwaona wachawi hao, lakini wachawi hao hawakuwa na uwezo wa kuwaona.

Waliendelea kubweka mithili ya mbwa koko, wakati huo wakazi wa mtaa wa Ushashini walikuwa wametopea kwenye lindi la usingizi mzito.

Mtoto THE BOMBOM na kundi lake walipita karibu kabisa na wachawi hao, kisha wakaendelea na safari yao. Waliachana na kijinjia kinachonyoosha hadi soko la chini la Igoma, wakafuata barabara hiyo ya mawe hadi kituo cha magari madogo kinachoitwa Ndama.

Kituo hicho kipo karibu na kiwanda cha utengenezaji wa soda huko Nyanza. Ni barabara kuu itokayo Mwanza mjini kuelekea Musoma. Tayari ilikuwa imetimia saa nane na dakika arobaini na tano usiku, wakati huo fisi wengi walikuwa wakipita barabarani hapo wakitoka kuwanga na mabwana wao.

Wakiwa bado wanaendelea na safari yao eneo hilo, walisikia mlio wa basi lililokuwa likija maeneo hayo likitokea Mwanza mjini.

Waliposikiliza kwa makini walibaini aina ya gari hilo wakaamua kulisubiria, kituoni hapo pasi na shaka. Basi lilivuka kituo cha Kijereshi, kiwanda cha bia cha Serengeti, Coca Cola na hatimaye likafika kituo cha Ndama.

Lilisimama kidogo abiria kumi na mbili wakapanda waliokuwa kituoni hapo. Kulingana na uwezo wa mtoto THE BOMBOM, tayari alikuwa amegundua kuwa mwisho wa basi hilo ilikuwa mji wa Nyanguge baada ya kuvuka mji wa Bukandwe.

Milango ya gari ilifungwa dereva akachomeka gia kisha akakanyaga mafuta mwendo ukaongezeka. Ndani ya gari hilo watu walikuwa uchi wa mnyama, hivyo mtoto THE BOMBOM na kundi lake hawakuwa wakionekana machoni mwao.

Pale kituoni abiria kumi na mbili waliopanda, baina yao wanne walikuwa ni wachawi wale wanane walikuwa ni abiria wa kawaida.

Abiria hao walikuwa wamedamka asubuhi na mapema kufuata biashara, wengi wao walikuwa wakifuata matunda, nyanya na mboga za majani mji wa Isangejo.

Pale kituo cha magari walikutana na wachawi wanne, ambao waliwahadaa kwa madawa na kuonekana kama abiria wanaosubiri usafiri kumbe ni wachawi. Kumbuka basi hilo lilikuwa la kichawi, lilikuwa likifanya kazi ya kuwakusanya wachawi wa kambi yao.

Wakati huo gari lilikuwa limeongeza mwendo jambo ambalo lisingekuwa rahisi kwa wale abiria kuruka nje hata baada ya kugundua hawakuwa salama.

Wale wachawi walikuwa uchi wa mnyama kuanzia dereva, kondakta na abiria isipokuwa wale abiria wanane tu. Hali haikuwa rafiki hata kidogo kwa wale abiria wa kawaida, hawakuamini kwa kile walichokuwa wakiona ndani ya basi hilo.

Kwa upande wa wachawi kila mmoja alikuwa na shughuli zake, wapo waliokuwa wakiahangaika na kula nyama za binadamu.

Wengine walikuwa wakitikisa vichwa vyao wakifanya mawasiliano ya kichawi na wachawi wenzao. Wachawi wote walikuwa wamekaa kwenye viti vyao, viti vya gari hilo vilikuwa ni vichwa vya binadamu vilivyokuwa ni mafuvu.
Kwa upande wa kiti cha dereva yeye kilikuwa kimetengenezwa kwa muundo wa viti vya jadi vya ngozi, lakini chenyewe kilikuwa kimetengenezwa kwa mifupa ya binadamu.

Taa za ndani za gari hilo zilikuwa ni macho ya watu wenye ulemavu wa ngozi yaani albino. Hapa niseme kidogo, kwa kiasi kikubwa watu wenye ulemavu wa ngozi huonewa sana katika ulimwengu wa giza.

Miguu yao hutumiwa kuunda matairi ya magari ya kichawi, mifupa yao hutumika pia katika utengenezaji wa madawa mbalimbali na viti vya ndege zao.

Nywele na kucha zao pia hutumika katika kutengeneza aina mbalimbali za madawa ya kichawi, kila unachokiona kwenye mwili wa albino katika ulimwengu wa giza hutumika tena kina thamani kubwa.

Macho ya albino hutumiwa kama taa za ndani za gari zao, huchanganywa na madawa mengine ili kutoa mwanga huo. Kumbuka kuwa viganjwa vya vya binadamu ndivyo hutumika kama taa za nje za magari hayo ya kichawi na shughuli zingine zinazohitaji mwanga.

Wale abiria walikuwa katika wakati mgumu, hali waliyokuwa wakiishuhudia ndani ya gari hilo iliwatia wasiwasi mkubwa.

Baadhi ya wachawi walikuwa wameshika vichwa vya watoto wachanga, huku wakiendelea kuvitafuna mithili ya mkate wa kuchomwa.

Damu zilikuwa zimewatapakaa mwili mzima, lakini hawakujali hilo wao waliendelea kula. Wachawi wengine walikuwa wakitafuna nyeti za kiume, haikujulikana nyeti hizo walikuwa wamezitoa wapi.

Nyeti zenyewe zilikuwa zimevimba mfano wa zile za punda, rangi yake pekee ya nyeti hizo ilidhihirisha hazikuwa za Waafrika bali zilikuwa za Waasia au Wazungu.

Namna wachawi hao walivyokuwa wakizishughulikia ungedhani ni nyama za kuku, kila mmoja hakujishughulisha na mwenzake zaidi ya kuendelea na mambo yake.

Mara mchawi mmoja aliyeonekana kuwa kiongozi ndani ya gari hilo aliwafuata wale abiria wanane. Mkononi alikuwa kashikilia kibuyu kilichokuwa kimejaa damu, haikujulikana damu hiyo ilikuwa ya mnyama gani.

Lakini kwa namna mazingira yalivyokuwa ndani ya basi hilo, ni dhahiri kabisa kuwa damu hiyo ilikuwa ya binadamu. Aliwasogelea abiria hao huku akiwa kimya, alipofika kwa abiria wa kwanza alimkabidhi kile kibuyu na kumtaka kunywa ile damu iliyokuwa ndani ya kibuyu hicho, damu yenyewe ilikuwa nyeusi tii ikinuka huku ikiwa imechanganywa na vinyama nyama.

Yule abiria aliangaza huku na huku akitafua upenyo wa kuruka ili aepukane na suruba hiyo, mbaya zaidi madilisha na milango ya gari hilo ilikuwa imefungwa.

Hapakuwa na eneo la kutoroka ikabidi abiria huyo apokee kibuyu hicho, mikono yake ilikuwa ikitetemeka mithili ya mawimbi ya bahari.

Wakati huo mchawi huyo alikuwa kamsimamia mithili ya askari mnyampara, yule abiria alijikuta akidondosha kibuyu hicho. Damu hiyo ilimwagika garini humo na kutapakaa eneo lote la chini, yule mchawi alimtandika kofi abiria huyo akadondoka chini.

Wakati haya yakitendeka mtoto THE BOMBOM na kundi lake walikuwa ndani ya gari hilo wakishuhudia kila jambo lililokuwa likitendeka hatua kwa hatua.

Hawakutaka kuingilia ugomvi huo kwa kuwa walikuwa na mzozo mkubwa dhidi ya wale Wazungu, kutoonekana machoni mwa wa wachawi hao ndani ya gari lao ulidhihirisha uwezo mkubwa wa madawa waliokuwa nao kundi la mtoto THE BOMBOM na watu wake.

Yule mchawi aliendelea kumshikisha adabu yule abiria aliyemwaga damu, alinyanyua mguu wake na kumkanyaga tumboni abiria huyo akatapika chakula chote alichokula usiku wa kuamkia siku hiyo.

Kipigo kiliendelea kwa abiria huyo mbele ya macho ya wale abiria wengine saba waliokuwa wamesalia, abiria huyo alipigwa mpaka akabaki nyakanyaka yaani hakujitambua hata kidogo.

Wakati huo gari lilikuwa limevuka soko dogo la Igoma na Igoma By Night likielekea soko la juu. Punde si punde lilifika soko la juu likasimama, eneo hilo walipanda wachawi watano kisha likaendelea na safari yake.

Hakukuwa na abiria wa kawaida aliyepanda kituoni hapo, wale abiria waliokuwa ndani ya gari hilo walijilaumu sana kupanda gari hilo.

Siku zote wamekuwa wakiamka mapema kwa ajili ya kufuata bidhaa yao, hawakuwahi kukutana na maswahibu kama haya.

Hakika siku hiyo walikuwa wamepatikana tena sana, walijikuta wakiamini msemo usemao "ndege mjanja..." Yule mchawi alipotosheka na kipigo alichotoa kwa abiria huyo, alikwenda eneo la mbele la gari hilo karibu na dereva.
Baada ya kufika huko alifungua kitambaa cheusi kilichokuwa kimefunika jungu kuu jeusi. Alitumbukiza kibuyu chake ndani ya jungu hilo akachota kitu kilichokuwa ndani yake, sekunde kadhaa alikitoa kibuyu hicho kikiwa kimejaa damu nyingine.

Damu hiyo ilikuwa nyeusi tii kuliko ile ya awali, ilichanganyikana na vinyama nyama vingi zaidi ya ile ya awali. Damu hiyo ilikuwa nzito mithili ya asali mbichi, yule mchawi alitumbukiza mdomo wake na kuilamba kisha alioneka kurudi eneo walilokuwa wale abiria.

Wakati huo yule abiria aliyechezea kipigo hakuwa akijitambua, woga ulikuwa umetamalaki kwa wale abiria saba waliokuwa wamesalia.

Hakika walikuwa wamedandia gari la vibwengo, hakukuwa na namna yeyote ya kutoroka zaidi ya kumuomba Mungu wao.

Wakati huo gari lilikuwa limevuka eneo linaloitwa stendi ya Magu kwa pale Igoma, hapo halikusimama badala yake lilikwenda kusimama stendi ya Maramara. Pale pia walipanda wachawi wengine watano, mikononi mwao walishikilia vitu.

Baada ya muda vitu hivyo vilibainika vilikuwa ni makondo, mifuko ambayo hutumika kubebea watoto wangalipo tumboni.

Kila mchawi alikuwa amebebelea mikononi mwake, yalikuwa yakinuka mithili ya panya aliyefia ndani ya chungu. Lakini wachawi hawakuwa na wasiwasi wao waliiona yalikuwa mazuri, mbaya zaidi hata wenzao waliokuwa ndani ya gari hawakujali kabisa.

Yule mchawi mwenye kibuyu kilichojaa damu alimkabidhi kibuyu hicho abiria mwingine. Yule abiria alionekana kutetemeka mithili ya tetemeko la ardhi, aliendelea kukishikilia kikombe hicho chenye damu akisubiria amri toka kwa mchawi huyo.

Wakati huo yule mchawi alikuwa akimkata jicho la hasira, hakuonesha kuwa na chembe ya mzaa hata kidogo. Lilo jicho aliliona abiria huyo aliyekuwa kakabidhiwa kibuyu hicho, ikabidi aangalie pembeni maana jicho la mchawi huyo lilitisha.

Ghafla mchawi mwingine alisimama na kujongea eneo walilokuwa wamesimama wale abiria na yule mchawi. Mchawi huyo alikuwa aneshika ziwa bichi la mwanamke alilokuwa akiling'ata na kutafuna mithili ya mshikaki wa mbuzi.

Ziwa hilo lilikuwa limeoza tena lilikuwa likinuka kuliko maelezo, lakini mchawi huyo hakujali hata kidogo. Alipowasogelea abiria hao walionekana kutetemeka zaidi, aling'ata kidogo ziwa lile kisha aka...

LYANGOSHA

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news