ASILIMIA 70 YA MAPATO YA VITUO VYOTE NCHINI INATEGEMEA NHIF-DKT.MOLLEL

NA MWANDISHI WETU

NAIBU Waziri wa Afya,Dkt. Godwin Mollel amebainisha kuwa, asilimia 70 ya Mapato ya vituo vya huduma za Afya vya Serikali pamoja na binafsi vinategemea Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) ili kuendesha vituo hivyo.
Dkt. Mollel ametoa maelekezo hayo leo Juni 6, 2023 wakati akijibu swali la Mbunge wa Nkasi Kaskazini Mhe. Aida Joseph Khenani katika Bunge la kumi na mbili Mkutano wa kumi na moja kikao cha 41 jijini Dodoma. 

Amesema, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umekuwa ni nguzo muhimu katika uboreshaji wa huduma za Afya Nchini ambapo taasisi binafsi za Afya pamoja na vituo vya huduma za Afya vya Serikali vimeonekana kutoweza kujiendesha bila uwepo wa Mfuko huo kutokana na Watanzania wenye uwezo wa kulipa fedha taslimu kuwa wachache. 

Ameendelea kusema kuwa, Serikali imefanya maboresho kwa kuongeza idadi ya dawa, vitendanishi na vifaa tiba ambapo kwa ngazi ya zahanati imeongeza kutoka aina 254 hadi 451 na kwa ngazi ya vituo vya Afya toka aina 414 hadi 828.

Sambamba na hilo, Dkt. Mollel amesema Serikali kupitia Wizara ya Afya inaendelea kutoa hamasa kwa viongozi wote ikiwemo Wabunge kuunga mkono Bima ya Afya kwa wote pindi mswada huo utapoletwa Bungeni ili wananchi wanufaike na huduma za afya katika ngazi zote kuanzia zahanati mpaka hospitali ya Taifa bila kikwazo chochote. 

Ameendelea kusema, katika kipindi ambacho Wizara inaendelea kufanya maboresho kwenye Bima ya Afya kwa wote, Wizara inaendelea kushirikiana na OR TAMISEMI na Wadau wa CHF kuboresha Bima ya Afya ya CHF ili kukidhi mahitaji ya kupata huduma bora kwa wananchi hasa wenye kipato kwa chini. 

Aidha, Dkt. Mollel amemwelekeza Mkurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ndani ya siku tatu hospitali ya Wilaya ya Biharamuro ipate huduma za NHIF ili wananchi wa Wilaya hiyo waanze kunufaika na huduma hiyo. 

Pamoja na hayo Dkt. Mollel amesema, Dkt. Mollel amesema, Serikali inaendelea kuboresha utoaji huduma katika maeneo yote ya utoaji huduma ikiwemo upatikanaji wa dawa, vifaa na vifaa tiba pamoja na kuendelea kutoa ajira kwa Wataalamu mbalimbali wa afya.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news