Waziri Mkuu atoa agizo kwa wakuu wa mikoa yote

NA MWANDISHI WETU

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewaelekeza wakuu wa mikoa yote ya Tanzania Bara, wakae na Mabaraza ya Biashara na Wamiliki wa kumbi za Starehe katika mikoa yao kwa madhumuni ya kutafuta muafaka wa pamoja katika utekelezaji wa sheria, kanuni, mwongozo kuhusu udhibiti wa athari zitokanazo na sauti zilizozidi viwango.
Waziri Mkuu amezielekeza Idara za Mipangomiji katika halmashauri za wilaya zote nchini zitenge maeneo ya ujenzi wa nyumba za ibada kama wanavyotenga maeneo ya taasisi nyingine. 

Ametoa maelekezo hayo leo Jumatatu, Juni 12, 2023 wakati akizindua Kongamano la Kujengewa Uelewa kuhusu madhara yatokanayo na sauti zilizozidi viwango katika nyumba za ibada. Kongamano hilo liloandaliwa na Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) limefanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Amesema ipo miongozo inayosimamiwa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi inayohusu masuala ya usimamizi wa mipango miji. “Nasisitiza toeni miongozo mahsusi ya mipango ya matumizi ya ardhi .” 
“Kwa upande wa udhibiti wa sauti zilizozidi, kila mamlaka iliyotoa vibali au leseni ya shughuli au biashara, zifuatilie mwenendo wa matumizi ya leseni hizo. Nasisitiza kuwa kila mamlaka itimize wajibu wake kulingana na maelekezo yaliyimo katika Mwongozo wa Uthibiti wa Uchafuzi wa Mazingira Utokanao na Kelele na Mitetemo uliotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais.”

“Leo kuna kongamano la kitaifa linaloratibiwa na JMAT, NEMC wekeni mpango wa kufanya makongamano kama haya hadi katika ngazi ya mikoa ili jamii iwe na uelewa wa pamoja kuhusu athari za viwango vya sauti vinavyozidi. Aidha, toeni elimu kwa umma ili wajue viwango halisi vya sauti vinavyostahili wakati wa mchana na wakati wa usiku.”

Akizungumzia kuhusu wamiliki wa majengo, Waziri Mkuu amewataka wafanye tathmini ya athari ya mazingira kwa watu wanaotumia majengo hayo pamoja na wakazi wa jirani na majengo hayo kwa lengo la kubaini madhara kwa watumiaji wa majengo hayo na jamii inayozunguka. 
Kadhalika, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwasisitiza viongozi wa dini, wanaoshiriki katika kongamano hilo waendelee kuwa vielelezo na mabalozi wazuri wa kufikisha yale mambo mazuri yanayowasilishwa katika kongamano hilo. 

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Samuel Gwamaka amesema madhumuni ya kongamano hilo ni kuwakutanisha pamoja viongozi wa dini na mila ili kutoa elimu ya athari za sauti zilizozidi viwango kutoka kwenye nyumba za ibada na jamii. 

Amesema kanuni za udhibiti wa kelele na mitetemo za mwaka 2015 zimeainisha viwango vinavyoruhusiwa katika maeneo ya makazi, nyumba za ibada, biashara, viwanda na hospitali kwa ajili ya jamii, mfano viwango vya sauti vinavyoruhusiwa katika nyumba za ibada zilizopo maeneo ya makazi ni dBA 60 wakati wa mchana na usiku dBA 40. 

Amesema sauti zinazozidi viwango katika nyumba za ibada zinaweza kuathiri afya za waumini waliopo kwenye nyumba za ibada na maeneo ya jirani na kusababisha matatizo ya kusikia, usingizi na kuathiri uwezo wa kufanya kazi pamoja na kusababisha migogoro kati ya wakazi na viongozi au waumini. 
Dkt. Gwamaka amesema NEMC itaendelea kusimamia kwa ukamilifu uzingatiaji na utekelezaji wa sheria na kanuni zake kwa kuandaa semina, warsha na mikutano ili kujenga uelewa mpana zaidi kwa jamii na wadau kadiri inavyohitajika. “Nitoe wito kwa viongozi wa dini tushirikiane katika utekelezaji wa sheria hizi ili kuboresha ustawi wa mazingira yetu.” 

Awali, Katibu Mkuu wa JMAT Askofu Dkt. Israel Maasa alitumia fursa hiyo kuwashukuru viongozi wenzake wa dini mbalimbali nchini kwa kuendelea kushirikiana hali inayolifanya Taifa liendelee kuwa kitovu cha amani na utulivu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news