Mwinjilisti Temba aiangukia Serikali ujenzi Bandari Kavu Migombani Ilala

DAR ES SALAAM-Muhubiri na Mwinjilisti wa Kimataifa, Alphonce Temba ameiomba Serikali kupitia Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Kassim kutoa ufafanuzi kuhusu ujenzi wa Bandari Kavu Migombani, Ilala jijini Dar es Salaam.

Temba ametoa ombi hilo leo Agosti 20, 2023 ikiwa ni siku chache zimepita baada ya wakazi wa Mtaa wa Migombani Kata ya Minazi Mirefu katika Manispaa ya Ilala, ambao wanatakiwa kuondoka katika eneo hilo kupisha mwekezaji anayejenga bandari kavu kuonesha kutoridhika na aina ya fidia wanayotakiwa kulipwa.

Wakazi wa hao ambao wanatakiwa kuondoka katika eneo hilo kupisha mwekezaji anayejenga bandari kavu wanaiomba Serikali kuingilia kati suala lao la kutaka walipwe fidia inayoendana na uhalisia wa nyumba zao tofauti na fedha anazotaka kuwalipa mwekezaji ambazo wamesema, haziendani na thamani ya nyumba zao.

Hatua hiyo inakuja baada ya kudai kwamba baadhi ya viongozi ambao walikabidhiwa jukumu la kuwasimamia wananchi hao ili waweze kuzungumza na mwekezaji huyo na wananchi wameshindwa kulisimamia jukumu hilo.

"Tunamuomba Rais Samia (Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan) atusaidie katika hili, kwani viongozi ambao walikuwa wanatusimamia katika hili hawaoneshi jitihada zote na kujikuta tukiendelea kuteseka.

"Kwani hapa kuna mavumbi mengi yanayotokana na mwekezaji kuanza ujenzi wa bandari kavu,''amesema Solomoni Mushi mkazi wa Mtaa wa Migombani.

Mwenyekiti wa kamati ya kutetea haki za wananchi kwenye eneo hilo, Chumu Samweli Chumu amesema, kinachowakwamisha viongozi kuwasaidia wananchi hao kulipwa stahiki zao ni siasa licha ya kwamba mwekezaji anao uwezo wa kuwalipa kwa haki.

"Mimi ninajua mwekezaji huyu si kwamba anashindwa kutulipa, lakini wapo baadhi ya viongozi anashirikiana nao katika hili,"amedai Mwenyekiti huyo.

Diwani wa Kata ya Miti Mirefu ambaye alifika kwenye eneo hilo kusikiliza kilio cha wananchi hao, Godlisen Malisa amesema, mtaji wa wafanyabiashara ni fedha, lakini mtaji wa wanasiasa ni watu, hivyo viongozi waoneshe ushirikiano ambao utawasaidia wananchi hao kuondokana na kero wanazozipata kwa sasa kutoka kwa mwekezaji huyo.

"Unajua hawa wananchi tunaposhindwa kuwasaidia kwa sasa na kuamua kuwaacha tu ni hatari, kwani hapa walipo wanaishi kwenye mazingira hatarishi sana kiafya na usalama wa maisha yao kutokana na ujenzi huu wa bandari kavu,"alibainisha Diwani huyo.

Mwinjilisti Temba

Kutokana na kadhia hiyo, Muhubiri na Mwinjilisti wa Kimataifa, Alphonce Temba amebainisha kuwa, "Tunamuomba Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mheshimiwa Kassim Majaliwa Kassim kutoa ufafanuzi juu ya masuala ya ujenzi wa Bandari Kavu Migombani Ilala (Dar es Salaam).

"Eneo ambalo mwekezaji anaoneonekana kabisa kushindwa hata kulipa gharama za nyumba za wananchi wa maeneo yale.

"Akijikita kuwapa fedha chini ya shilingi milioni 20,kwanza kabisa tungependa kupata ufafanuzi wa Waziri Mkuu kwa sababu, Serikali imeshajenga kwa gharama kubwa, eneo la Kwala bandari kavu.

"Na tayari wapo baadhi ya viongozi mbalimbali waliotoka nje za nchi ambao walipelekwa na kuelekezwa na kuoneshwa maeneo akiwemo Rais wa Jamhuri ya Burundi.

"Viongozi wa Rwanda, viongozi wa Congo (Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo) na baadhi ya taasisi zimeoneshwa maeneo yao na pia, na pia vipo viwanda vingine vinajengwa kule.

"Huko kutakuwemo na mjumuisho mkubwa wa maeneo ambayo yameorodheshwa kwa kuwa mji wa kibiashara ikiwemo Kwala yenyewe kata, Mpriramumbi Kijiji, Magindu, Mshua Kitongoji,Gwata, Ngwera, Chaua, Chalinze, Pingo,

"Mbala, Chamakweza, Vigwaza Kambini, Vigwaza kwa Zoka, Ruvu Darajani, Vishezi, Mlandizi, Vijingo,Mzenga na baadhi ya vijiji na vitongoji mbalimbali ambavyo tayari vimekwishapitishwa kama mji wa kibiashara na bandari kavu.

"Na Serikali imekuwa ikitoa matamko mbalimbali kupitia Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), kupitia Serikali yenyewe kwa maana ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kuwa, wameichagua Kwala kuwa bandari kavu.

"Ili mizigo yote itakayoingia kwa sasa hasa inayokwenda nje kupitia Bandari ya Dar es Salaam itasafirishwa moja kwa moja kwenda Kwala ambako kutakuwa na unafuu kutoka kule kwenda safari mbalimbali za nje ya nchi.

"Sasa,mwekezaji huyu anakwenda kuweka bandari kavu Dar es Salaam (Ilala),na bandari kavu nyingine inakuwa ipo Kwala,na bandari kavu lazima iwe ya Serikali, wawekezaji wanaweza kuwa na mayadi, magodauni, hivyo baada ya mizigo kutoka bandari kavu basi wao wakawa wanahifadhi mizigo kwa muda wakawa wanaisafrisha.

"Sasa, haya mambo ya bandari kavu kuendelea kuweko Ilala huku Serikali ikiendelea kufanya juhudi kubwa za kupunguza malori, ikizingatiwa kwamba Ilala ni sehemu ambayo imekuwa na shughuli nyingi za kiuchumi.

"Shughuli ambazo zinasababisha kuwa na njia kuu, mfano kuna njia kuu ya kwenda Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere.

"Njia kuu ya kwenda uwanja wa Taifa, njia kuu ya kwenda Kariakoo na njia nyingine nyingi ambazo ni muhimu na kiunganishi kikubwa kwa Taifa letu katika shughuli za kiuchumi,

"Kama vile kwenda viwanda vya Pugu, njia ya kwenda Kigamboni na Mbagala kwenda Kusini,kitendo cha bandari kavu kuendelea kujengwa Ilala Migombani, kitasaidiaje kupunguza msongamano wa malori ambao unatakiwa kuondolewa jijini Dar es Salaam?,

"Miji yote mikubwa, hususani yenye bahari huwa hakuna bandari kavu, Serikali inapaswa ijue kuwa Serikali yoyote yenye bahari inakuwa inajenga bandari kavu nje ya jiji, huwa haijengwi katikati ya jiji, huwa zinajengwa nje ya miji,kwa nini bado hatuna mikakati mizuri, kwa nini hatuna mwelekeo.

"Tunamuomba Waziri Mkuu atusaidie tuwe na mwelekeo wa kupunguza msongamano wa malori katikati ya jiji na si kuendeleza bandari kavu katikati ya jiji.

"Na ndiyo sababu,Serikali ikaona ni lazima itengeneze bandari kavu huko nje,angalau hayo malori yaishie huko nje,kumekuwa na mtapakanyo wa malori mbalimbali na saa nyingine unakuta kuna michezo ya Kimataifa.

"Michezo ya mipira, au michezo ya watani wa jadi Simba na Yanga au Taifa Stars inaendelea unakuta kunakuwa na mrundikano wa foleni, inayosababisha watu kushindwa kusafiri, watu wengine washindwe au wagonjwa washindwe kutoka.

"Leo hii, Ilala inajengwa bandari kavu, hali ya nchi itakuwaje wakati barabara haziongezwi badala yake kumekuwa na foleni kubwa, tunaiomba Serikali ije itueleze, itasaidiaje kupunguza malori jijini Dar es Salaam hususani katikati ya Jiji la Ilala.

"Huku mwekezaji akiendelea kutafuta eneo la kuweka bandari kavu ambayo itaweza kusababisha malori mengi yakawa pale pale, kuna umuhimu gani sasa wa kujengwa Bandari Kavu Kwala? Wakati bandari kavu inataka kujengwa Ilala?.

"Serikali iingilie kati na iwe na mwelekeo mzuri ili sisi Watanzania hasa tuliopo Dar es Salaam, ambao tunapoteza mabilioni ya fedha kila siku kwa sababu ya malori kujaa katikati ya jiji tuweze kuziokoa hizo fedha.

"Tunashuhudia maeneo kama vile Tabata,maeneo kama vile Buguruni, Chang'ombe, Sabasaba, Ubungo, Kimara, Mbezi malori yanavyozuia watu mbalimbali kwenda katika shughuli zao.

"Zaidi ya yote ni malori ya mafuta pia ambayo yanaelekea Kigamboni na sehemu zingine za mafuta kuweka mafuta yanavyokuwa yamechotwa mafuta na baadhi ya vijana wanaotumia plastic bags kuchukua mafuta yaliyokuwa yamebaki, jambo ambalo ni hatari na linaweza kusababisha mlipuko mkubwa wa moto kwa wavuta sigara wanaopita pembezoni mwa barabara.

"Tunaiomba Serikali ije pia kutueleza, je? Ujenzi wa bandari kavu ya Ilala (Migombani) itaenda sambamba vipi na kupunguzwa kwa malori kujaa Dar es Salaam.

"Hivi karibuni tumeona TANROADS wakitengeneza eneo la kuegesha magari yasiingie kwa fujo mjini, pale eneo la Mbezi Kibanda cha Mkaa ambako yamekuwa yakizuiwa mpaka mchana kuruhusiwa kuingia jijini.

"Hata hivyo, bado msongamano ni mkubwa, wakati wa jioni kuanzia saa kumi, kuanzia maeneo ya Ubungo mpaka Kimara kumekuwa na vurugu kubwa ya malori, na mengi yamekuwa yakifa njiani wakati watu wakitoka makazini na kurudi majumbani hiyo foleni imesababisha shida kubwa kwa Watanzania hata wagonjwa hasa wanaokwenda hospitali mbalimbali.

"Mfano kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili, Ocean Road,Aga Khan, Tumbi na nyinginezo, hivyo muda mwingi kutumika barabarani kutokana na kukosa mahali pa kupenya kwa sababu malori mengi yamekufa barabarani, na msongamano ni mkubwa, huu ujenzi wa banadari kavu Ilala, utasaidiaje Watanzania kuondokana na malori kujaa jijini Dar es Salaam?.

"Ikumbukwe kwamba kuna malori ya mizigo na matenki nchini, yanayozidi 35,000 ambayo yanaingia Dar es Salaam karibu asilimia 90.

"Sasa leo hii kuruhusiwa kujengwa kwa bandari kavu kutaondoaje haya malori 35,000 yanayojaa jijini Dar es Salaam yapungue ili kuwe na utaratibu mwingine mzuri wa kuwasaidia Watanzania wanaokwenda kwenye kazi zao na Watanzania wanaokwenda kwenye shughuli zingine nje ya masuala ya banadari?.

"Tunamuomba Waziri Mkuu aje atuelimishe Watanzania na atusaidie tuweze kupata uelewa kuhusu ujenzi huu wa bandari kavu kwa sababu watanzania wengi wamepigwa na butwaa kuhusu ujenzi wa bandari kavu katikati ya jiji,Tanzania itakuwa ndiyo nchi pekee duniani inayojenga bandari kavu sasa.

"Kwa nini watu hawa, mwekezaji huyu asielelezwe eneo la Serikali la NARCO lililoko Kwala akapewa kwa ajili ya ujenzi wa bandari kavu?. Inawezekana akatumia robo tatu tu ya gharama ambazo alikuwa anunue nyumba hapo akapewa lile eneo la Serikali kwa ajili ya bandari kavu.

"Na akatumia reli, kwa sababu mizigo hiyo kuwepo Ilala siyo kwamba itakusababishia kupata hasara akikaa Kwala kwa sababu mizigo hiyo inatoka Japan, China, Ulaya na inakuja kutoka mbali hivyo kuisubiri Kwala ni rahisi kuliko kuisubiri Ilala, anaweza kufanikiwa kujenga bandari kavu, lakini ule mzunguko wa kutoka na kuingia na ule mzunguko wa kuwawekea watu hifadhi pale,

"Ukawa ni gharama sana na matokeo yake Bandari Kavu ya Kwala ikamsababishia hasara kubwa, hivyo pia, Serikali imlinde mwekezaji huyu anayeweka bandari kavu.

"Kwa sababu asije akawa amekopa kwenye mabenki mbalimbali akashindwa kurudisha kwa sababu hakuna atakayekubali mizigo yake ifikie pale ambako kutakuwa na charges kubwa sana.

"Na, kule Kwala charges zake zaka ziko chini kwa sababu ya gharama ya ardhi kule ipo chini, lakini suala la bandari kavu lazima liwe kwenye ulinzi wa Serikali, ulinzi wa Serikali ijengwe na Serikali kwa sababu ya kukwepa kuwa na vitu ambavyo ni hatarishi na visivyo na usalama kwa nchi na usalama wa nchi pia kwa ujumla,

"Kwa hiyo, Serikali itusaidie kwa sababu tafsri ya ujenzi wa bandari kavu ni kubwa, kama ni yadi au bandari kavu au ni stoo au ni magodauni, yajulikane ni magodauni.

"Lakini, bandari kavu inapaswa ijengwe na Serikali na si kujengwa na watu binafsi,"amefafanua kwa kina Muhubiri na Mwinjilisti wa Kimataifa, Alphonce Temba.
 
Bandari kavu kwa maana ya Inland Container Deport (ICD) ni maeneo mahsusi yaliyotengwa kwa ajili ya kuhifadhi makontena mpaka yatakalipiwa ushuru. Hii ni kusaidia kupunguza msongomano bandarini na kurahisisha utoaji wa mizigo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news