NGOJA TUISHANGILIE, HII SERENGETI YETU

NA LWAGA MWAMBANDE

USIKU wa Oktoba 15, 2023 Hifadhi ya Taifa Serengeti imeibuka kidedea kwa kuwa mshindi wa kinyang’anyiro cha Tuzo ya Hifadhi bora barani Afrika kwa mwaka 2023.

Tuzo hii ambayo ufahamika kwa jina la kitaalamu Africa’s Leading National Park 2023 inakuwa ni mara ya tano mfululizo kwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kushinda.

Ni baada ya kuwagaragaza washindani wa tuzo hiyo wakiwemo Central Kalahari Game Reserve- Botwswana, Etosha National Park -Namibia, Kidepo Valley National Park -Uganda, Kruger National Park -South Africa, mapoja na Masai Mara National Reserve - Kenya.

Tanzania imekabidhiwa tuzo hiyo na World Travel Awards katika Hoteli ya Atlantis The Royal iliyopo Dubai katika nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu na kupokelewa na Mkuu wa Kanda ya Magharibi, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Izumbe Msindai kwa niaba ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA).

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande licha ya kupongeza juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuimarisha Sekta ya Utalii nchini, pia amesema ushindi wa Hifadhi ya Taifa wa Serengeti unaendelea kuwapa heshima Watanzania kote duniani, Endelea;


1. Ngoja tuishangilie, hii Serengeti yetu,
Ushindi tufurahie, ubora kwa bara letu,
Mitano na itimie, kilele kile cha kwetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora kwa Afrika.

2. Kwa miaka mitano, ya mfululizo kwetu,
Imeandikwa kwa wino, ushindi wote ni wetu,
Vitendo siyo maneno, inashinda mbuga yetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora kwa Afrika.

3. Huko tunao wanyama, ni maliasili yetu,
Mbuga inatunzwa vyema, kwani ni urithi wetu,
Duniani inavuma, safari za nyumbu wetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora Afrika.

4. Kwa huu mfululizo, ushindi kwa mbuga yetu,
Acha zijazane tuzo, hiyo ni faida kwetu,
Izidi kuwa gumzo, katika sayari yetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora Afrika.

5. Kura hatujipigii, kupata ushindi wetu,
Ni wale wanaotii, ubora wa mbuga yetu,
Hao hawasubirii, kupaisha mbuga yetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora Afrika.

6. Wito wetu tunatoa, uongozi mbuga zetu,
Endelea kujitoa, kuzitunza mbuga zetu,
Kila siku ziwe poa, zilete faida kwetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora Afrika.

7. Serengeti kwa ushindi, hiyo ni faida kwetu,
Wazungu hata Wahindi, watafika wengi kwetu,
Tutapata nyingi Randi, tujenge uchumi wetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora Afrika.

8. Pongezi ziweze fika, kwao wahifadhi wetu,
Ambao wachakarika, kuzitunza mbuga zetu,
Hata zinatambulika, kama Serengeti yetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora Afrika.

9.Mambo yanayofanyika, huu utalii wetu,
Wageni waongezeka, faida yabaki kwetu,
Tuendako tutafika, sawa na malengo yetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora Afrika.

10. Royal Tour twakumbuka, ile ya Rais wetu,
Nchi inavyofunguka, hizi nyingi sera zetu,
Nchi yetu yasomeka, katika dunia yetu,
Hii Serengeti yetu, ni Mbuga Bora Afrika.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news