NMB yapeleka tabasamu Shule ya Sekondari Sombetini

ARUSHA-Wakati shule ya sekondari Sombetini wakilia na uhaba wa madawati 363, Benki ya NMB imefanikiwa kuwakabidhi msaada wa viti na meza 100 vyenye thamani ya shilingi milioni 10.
Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Felician Mtahengerwa na viongozi mbalimbali wa elimu Kata ya Sombetini akipokea msaada wa madawati hayo kutoka kwa Meneja wa Kanda ya Kaskazini wa Benki ya NMB, Baraka Ladislausi.

Msaada huo umetajwa kuwasaidia wanafunzi 100 pa kukalia, huku wakiomba wadau wengine kujitokeza.

"Tunashukuru sana kutupunguzia pengo hili kubwa, hakika mmetusogeza sana, kwani tulikuwa na uhitaji wa viti 363 na sasa mmetupa 100 na kufanya idadi ya viti shuleni hapa kufikia 1362 ukiachana na zile 1262 zilizokuwa zinategemewa na wanafunzi wote 1625, msituchoke tukija kuomba vingine 263 zilizobaki," alisema Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sombetini, Bertha John.

Akizungumza wakati wa makabidhiano, Meneja Kanda ya Kaskazini wa Benki ya NMB, Baraka Ladislaus alisema msaada huo ni muendelezo wa utaratibu wao wa kurudisha faida kwa kuhudumia jamii wanaozidi kuiwezesha Benki hiyo kufanya vizuri nchini.
"Benki ya NMB mwaka huu tumetenga zaidi ya bilioni 6.2 kwa ajili ya kuhudumia jamii ambapo ukiachana na mazingira na Afya, pia Elimu ni moja ya kipaumbele chetu muhimu kutokana na kutambua ukweli kuwa ndio msingi sana kwa maendeleo ya Taifa lolote hapa duniani," alisema Baraka.

Aliongeza kuwa,msaada huo wa viti na madawati 100 vyenye thamani ya shilingi milioni 10, sio mwanzo na hautakuwa mwisho wa kusaidia serikali katika kutatua changamoto zinazoikabili sekta ya Elimu, Afya na mazingira lakini pia majanga mbali mbali yanayojitokeza nchini.

"Tunatambua juhudi kubwa za serikali chini ya Rais wetu Samia Suluhu za kusimamia upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi, hivyo sisi kama wadau tunao wajibu wa kuunga mkono, kusaidia na kuwa mstari wa mbele katika kuchagia utatuzi wa changamoto zinazojitokeza katika jamii," alisema Meneja huyo wa NMB.
Alisema kuwa,moja ya mafanikio makubwa waliyoyapata ni kufungua matawi 229 na kusambaza mashine za kutolea huduma zaidi ya 800 huku wakiwa na zaidi ya mawakala 20, 000 nchi nzima.

"Kwa sasa NMB tumefika mikoa na Wilaya zote nchini huku tukizindua kampeni mbali mbali za kutoa masuluhisho ya huduma za kifedha na mikopo kwa wateja wetu ikiwemo ',onja unogewe ' , 'hati fungani' na zinginezo nyingi."

Akipokea msaada huo, Mkuu wa Wilaya ya Arusha,,Felician Mtahengerwa aliipongeza Benki ya NMB kwa kuwa msaada mkubwa kwa jamii na serikali kupitia misaada yao katika sekta ya Afya na Elimu huku wakiwataka kutanuka zaidi kimataifa.
"Hakika nawapongeza sana kwa kuwa Benki namba moja nchini kutambua na kutatua changamoto zinazoikabili jamii zilizokuwa ziigharimu serikali, hivyo nawapa changamoto kubwa sasa mtanue matawi yenu nje ya nchi ili kuwahudumia na watanzania walioko nje lakini watalii wanaoingia nchini kutoka nje."

Zaidi aliwataka kuunga mkono pia juhudi za halmashauri za kuweka Jiji safi kwa kutoa msaada wa ndoo za kukusanyia taka (dustbin) ili zisambazwe mjini katika kuweka Arusha katika hali ya usafi na kuvutia watalii zaidi.

Akitokoa shukrani kwa msaada huo, mmoja wa wanafunzi Joan Mremi alisema, samani hizo zimekuja wakati muafaka wakielekea kufanya mitihani yao ya kidato cha nne ambapo wangelazimika kuwanyang'anya wanafunzi wenzao wa madarasa ya chini viti ili kufanya mitihani kwa uwiano wa mwanafunzi mmoja kiti kimoja.
"Tunasema asante sana kwa Benki ya NMB kuonyesha ukaribu wao kwetu kivitendo, na tunaahidi kutumia viti hivyo kuongeza ufaulu kwani wanafunzi wengi sasa watakuwa na viti vya kukalia sio kubebana wala kukaa kwa zamu."

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news