Serikali kuziwezesha mamlaka za Serikali za mitaa kusimamia taka

DODOMA-Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis amesema Serikali kwa kushirikiana na Washirika wa Maendeleo imeibua miradi ya kuziwezesha Mamlaka za Serikali za Mitaa kusimamia taka nchini.
Amesema hayo wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mikakati ya kukabiliana na uchafuzi wa mazingira kwenye mito na mifereji katika jiji la Dar es Salaam, mafanikio na changamoto kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira jijini Dodoma, Oktoba 23, 2023.

Mhe. Khamis amesema Serikali ilitoa mwongozo wa usafishaji mito kwa lengo la kuondoa taka ngumu, mchanga na tope kwa mito ya Dar es Salaam kwa lengo la kupunguza madhara yanayoweza kutokea kutokana na uchimbaji holela wa mchanga katika mito hiyo.

Amesema katika utekelezaji wa Mwongozo, usafishaji ulianza katika mito mitano na hadi sasa jumla ya mito tisa mkoani humo ikiwemo Msimbazi, Mbezi, Tegeta, Nyakasangwa, Mpiji Luhanga, Kibangu, Kibwegere na Kigori imeanza kusafishwa.

Aidha, Naibu Waziri Khamis ametaja mafanikio yaliyopatikana kutokana na utekelezaji wa mikakati ya kukabiliana na uchafuzi wa mito na mifereji kuwa ni pamoja na kuongezeka kwa usafi wa mito katika maeneo ya jiji ambapo jumla ya urefu wa eneo la mito lililosafishwa ni takribani mita 99,677 ambapo wakandarasi wamesafisha mita 41,150 na vikundi vya machepe mita 58,527.

Pia, amesema uimarishaji wa kingo za mito ambapo miti rafiki kwa mazingira 24,000 imepandwa katika maeneo mbalimbali kama vile mto Msimbazi eneo la Pugu Station, Mto Mpiji maeneo ya Mgemuzi, Mabwepande Mitiki na Mbweni.

Dar es Salaam ni mojawapo ya majiji makubwa likiwa na jumla ya watu milioni tano kwa mujibu wa Sensa mwaka 2022, ongezeko likiambatana na shughuli nyingi za kiuchumi na kijamii ambazo zinachangia kwa kiasi kikubwa changamoto za kimazingira ikiwemo uchafuzi unaotokana na taka ngumu na taka maji.

Kwa mujibu wa takwimu za hivi karibuni uzalishaji wa taka ngumu ni wastani wa tani 4,161 kwa siku ambapo kati ya hizo, uwezo wa Halmashauri kukusanya taka ni asilimia kati ya 45 hadi 50 tu, ambapo zaidi ya asilimia 50 ya taka hubakia kwenye mazingira na kuzagaa hadi kwenye mito na mifereji ya maji taka na mitaro ya maji ya mvua.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news