Mheshimiwa Spika tusikubali, Serikali inaibiwa-Luhaga Mpina


MCHANGO WA MBUNGE WA JIMBO LA KISESA, MH.LUHAGA JOELSON MPINA AKICHANGIA TAARIFA YA KAMATI YA PAC, LAAC NA PIC KUHUSU TAARIFA YA CAG YA MWAKA 2021/2022 BUNGENI DODOMA TAREHE 3 NOVEMBA 2023

1: UTANGULIZI

Mheshimiwa Spika,huko nyuma niliwahi kusema na niliwaomba waheshimiwa wabunge na Mheshimiwa Spika tusikubali Bunge hili Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lililowekwa madarakani na wananchi wanyonge kutumika kama sehemu ya kusafisha viongozi na watendaji wa Serikali waliohusika na wizi, rushwa na ubadhirifu wa mali za umma.

Wahenga walisema lakuvunda halina ubani.Nichukue nafasi hii kumpongeza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa
Hesabu za Serikali (CAG), CPA Charles Kichere na timu yake yote ya watumishi wa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi (NAOT) kwa ukaguzi mlioufanya ni kielelezo kikubwa cha uzalendo mlionao kwa taifa letu la Tanzania, Mungu awabariki sana.

Na kipekee kabisa nimpongeze sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu mawanda mapana ya ukaguzi kufanyika na kukataa nchi yetu kugeuzwa kuwa pango la wezi, wala rushwa na mafisadi.

Pia niwapongeze Kamati za Bunge za PAC, LAAC na PIC kwa uchambuzi wa ripoti ya CAG na kuwasilisha mapendekezo kwa Bunge kwa hatua zake na kwa mujibu wa Sheria ya Ukaguzi wa Umma Na. 11 ya Mwaka 2008.

Kipekee niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Kisesa kwa namna mnavyoendelea kuniunga mkono katika kuhakikisha maendeleo ya kweli yanapatikana Jimbo la Kisesa na Taifa zima.

2:UCHAMBUZI WA TAARIFA ZA KAMATI YA PAC, LAAC NA PIC KUHUSU RIPOTI YA CAG 2021/2022

Mheshimiwa Spika, nimesoma taarifa ya CAG ya mwaka 2021/2022 pamoja na utekelezaji wa hoja za miaka ya nyuma, Taarifa ya Kamati za Ukaguzi za PAC na LAAC na Taarifa ya Majumuisho ya Majibu ya Serikali na Mpango kazi wa utekelezaji wa mapendekezo ya CAG mwaka 2021/2022 ambayo yana jumla ya kurasa 1,111.

Kwa kifupi katika majibu haya, hoja za CAG hazikujibiwa kikamilifu na haionyeshi hatua mahususi zilizochukuliwa na Serikali kwa watuhumiwa na wabadhirifu wa fedha za umma tangu ripoti ya CAG iwasilishwe Machi 2023.

Niliwahi kusema hapa bungeni kuwa, kwa mujibu wa uchambuzi wangu wa Taarifa ya CAG ya mwaka 2021/2022 inaonyesha tumepigwa zaidi ya shilingi Trilioni 30 na nikaweka jedwali kuonyesha maeneo tuliyopigwa. Leo pia naambatisha jedwali hilo.

Lakini pia kwa mujibu wa taarifa ya FIU miamala shuku inaonyesha kufikia shilingi Trilioni 280 ambapo shilingi Trilioni 56.65 ni fedha taslimu na shilingi Trilioni 222.81 zilisafirishwa kwa njia ya kielektroniki, pia kati ya fedha hizo zilihusu usafirishaji wa fedha taslimu na hati za malipo kupitia mipakani.

Hii ni kwa mujibu wa taarifa ya Kitengo cha Udhibiti wa Utakasishaji wa Fedha Haramu, Ufadhili wa ugaidi na Ufadhili wa silaha za maangamizi na siyo taarifa ya Mpina.

Katika hali hiyo, ni ishara tosha kuwa kuna tatizo kubwa la utoroshaji fedha nje ya nchi, wizi, ubadhirifu, rushwa na ufisadi nchini.

2.1 Hoja ya Kamati ya PAC kipengele cha 2.2.3.2 kuhusu ongezeko la gharama za mradi kwa kipande cha 3 na 4 cha SGR kwa wastani wa dola za Marekani milioni 1.3 na milioni 1.6 mtawalia na kuisababishia hasara Serikali ya shilingi Trilioni 1.7.

Ukaguzi kuhusu Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mradi wa SGR Lot. 3 na Lot. 4 kuacha bei ya ushindani na kutumia Single Source na kuisababishia hasara Serikali ya shilingi Trilioni 1.7

(i) Kamati inathibitisha kuwa kwa kutumia njia ya ushindani (Competitive Tender) gharama ya ujenzi wa kilomita 1 katika Lot 1, Lot 2 na Lot 5 ilikuwa ni wastani wa dola za Marekani Milioni 4.2 ikilinganishwa na njia ya mzabuni mmoja (Single Source) ambayo ni wastani wa dola za Marekani milioni 5.35 sawa na ongezeko la dola za Marekani milioni 1.15 sawa na ongezeko la shilingi bilioni 3 kwa kila kilomita ya SGR.

(ii) Kamati inakiri kuwa bei zilizotolewa kwa njia ya ushindani hazikutofautiana kwa mbali licha ya kupita miaka mitano yaani Lot. 1 ya mwaka 2017 ilikuwa na wastani wa shilingi Bilioni 9 kwa kilomita 1 ya SGR wakati Lot. 5 ya mwaka 2020 ilikuwa ni wastani wa shilingi Bilioni 9.15.

Kwa kilomita ya SGR hili ni ongezeko la dola za Marekani 0.15 kwa kilomita sawa na ongezeko la shilingi Bilioni 0.4 kwa kilomita 1 ya SGR kwa miaka 5.

Hivyo, kwa njia ya ulinganifu Serikali ilipotumia njia ya ushindani bei iliongezeka kwa shilingi Bilioni 0.4 kwa kilomita 1 ya SGR katika kipindi cha miaka 5, lakini Serikali ilipoacha njia ya ushindani na kutumia njia ya Single Source gharama iliongezeka kwa shilingi Bilioni 3 kwa kilomita 1 ya SGR kwa mwaka mmoja.

Pia, siyo sahihi kusema kuwa gharama zimeongeka kwa kuwa ilikuwa imepita miaka sita kupatikana kwa mzabuni wa Lot.3 na Lot.4 mwaka 2021/2022, Kamati imesahau kuwa Lot. 5 iliyopatikana kwa njia ya ushindani ilitolewa mwaka 2020/2021, mwaka mmoja tu baadaye, hivyo CAG yuko sahihi.

(iii) Kamati katika kipengele cha 2.2.3.3 ukurasa wa 48 na kipengele cha 2.2.3.5 ukurasa wa 53 Kamati inakiri kuwa suala la kutumia mzabuni mmoja (Single Source) katika zabuni ya Lot. 3 na Lot. 4 lilikataliwa na PPRA(Mamlaka ya mwisho katika Usimamizi wa Manunuzi ya Umma) na Bodi ya Zabuni ya TRC kwa kuwa haikuwa rahisi kupata bei ya ushindani ili kupata thamani ya fedha (Value for Money).

Pia ni kinyume cha Sheria ya Manunuzi ya Umma Namba 7 ya Mwaka 2011 na kanuni zake Na. 161 (1) (2) (3) (4) (Single source Procurement for works) ya Kanuni za Manunuzi ya Umma ya Mwaka 2013 na Marekebisho yake (Mwaka 2016) na PPRA Guidelines.

Aidha, inaelezwa kuwa yalitolewa maelekezo ya kusainiwa mkataba huo kati ya TRC na Yapi Merkezi kutoka kwa Wizara ya Fedha kwa barua yenye Kumb. Na. PST/GEN/2021/01/55 ambayo pia ilikuwa ni mwendelezo wa kuvunja sheria za nchi kwa maslahi binafsi.

(iv) Maelezo kwamba kutumia njia ya single source katika kipande cha Lot. 3 (Makutupora- Tabora) Km 368 na Lot. 4 (Tabora-Isaka) Km 165 ya Reli ya SGR yalitokana na masharti ya mkopo kutoka Benki ya Standard Chartered kuwa ni lazima Kampuni ya Yapi Markezi iteuliwe kuwa mkandarasi hayana mantiki yoyote.

Kwani, ni kinyume cha Katiba kwa kuwa yanaingilia mamlaka ya nchi yetu kujiamulia mambo yetu wenyewe na ni kinyume cha Kifungu cha 64 (1) cha Sheria ya Manunuzi ya Umma ya Mwaka 2011 na Kanuni ya 149 (1) ya Kanuni ya Manunuzi ya Umma ya Mwaka 2013 ambayo inataka njia ya ushindani wa zabuni kupewa kipaumbele ili kupata bei ya ushindani kutoka kwa wazabuni na hivyo kupata thamani ya fedha (Value for Money).

Hata hivyo, Wizara ya Fedha ilipaswa kukabidhi Financing Agreement kwa bodi ya zabuni ya TRC na kwa CAG kuthibitisha sharti hilo la mkopo kutoka Benki ya Standard Chartered, Mikopo yote inayotafutwa na kukopwa nchini ni kwa mujibu wa Sheria na hivyo huwezi kuvunja Sheria za nchi kupata mikopo. Nchi yetu haiwezi kukubali kupokea masharti yasiyofaa eti kwa sababu za kupewa mkopo.

(v) Manunuzi haya ni makubwa na hayakuwa na dharura yoyote, Yapi Markezi sio kampuni pekee duniani inayojenga reli, lakini pia wakati inapewa zabuni ya Lot 3 na Lot 4 haikuwa imekamilisha vipande vya Lot 1 na Lot 2 na hivyo haikuwa na sifa ya kupewa zabuni kwa njia ya Single Source.

Hivi sasa miradi yote inayotekelezwa na Kampuni ya Yapi Markezi inaripotiwa kutokukamilika kwa wakati Lot.1 (98.14%), Lot.2 (93.83%), Lot. 3 (7%), Lot. 4 (2.39%).

Hii ni kwa mujibu wa Hotuba ya Bajeti ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi ya Mwaka 2023/2024 na kuna Malalamiko mengi ya ucheleweshaji wa mradi na madai ya kuwepo dhuluma dhidi ya maslahi ya wafanyakazi wazawa.

Hapa utaona licha ya mkataba huu kusainiwa miaka miwili iliyopita utekelezaji wa Lot 3 ni 7% tu na utekelezaji wa Lot 4 ni 2.39% tu.

(vi) Maelezo ya TRC kuwa sio sahihi kufanya ulinganishaji wa gharama na kipande kingine kwa kuwa kuna tofauti ya muda na mazingira siyo kweli kwa kuwa katika uchambuzi wa kihasibu na mambo ya fedha (Financial Analysis) inaruhusiwa kufanya ulinganifu huo.

Lakini, pia TRC wanasahau kuwa Lot. 2 ina maeneo mengi oevu na milima ambayo ilibidi hadi kuchimba mahandaki na uchorongaji wa miamba Lakini pia CAG hakupewa uthibitisho na vielelezo vya mabadiliko ya bei na makisio ya kihandisi (Engineering Estimates).

Kwa kuwa, TRC, Wizara ya Fedha, Wizara ya Uchukuzi zimeshindwa kutoa majibu ya kina ya nini kilichowasukuma kuacha njia ya ushindani na kutumia njia ya Single Source na kuisababishia hasara Serikali ya shilingi Trilioni 1.7,na kwa kuwa, kila wanapopewa muda na nafasi wanashindwa kujibu tuhuma hizo.

Ni dhahiri kuwa, zabuni hii ilitolewa kwa misingi ya rushwa na ufisadi. Hivyo basi, ninaomba kuongezea maazimio mawili katika Taarifa ya Kamati ya PAC kwamba Bunge liiagize Serikali kufanya yafuatayo:-

(a) Kufanya tathmini na Kuvunja Mkataba wa TRC na Yapi Markezi wa Lot. 3 na Lot.4 na kutangaza upya zabuni hiyo.

(b) Waziri wa Fedha (Mhe. Dk. Mwigulu Lameck Nchemba), Waziri wa Uchukuzi (Mhe. Prof. Makame Mbarawa Mnyaa), Mkurugenzi Mkuu wa TRC (Ndg. Masanja Kungu Kadogosa), Mkurugenzi wa Yapi Markezi na wengine wote waliohusika wakamatwe na washtakiwe kwa makosa ya uhujumu uchumi na kuhakikisha kuwa hasara walioisababishia taifa ya shilingi Trilioni 1.7 wanaifidia.

3.2 Hoja za ukaguzi kuhusu Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO)

3.2.1 Hoja ya kutoweka tozo ya fidia ya ucheleweshaji wa mkataba wa shilingi Bilioni 327.93

Hoja hii sijaiona kwenye taarifa ya Kamati lakini katika Taarifa ya Majumuisho ya majibu ya Serikali na Mpango kazi wa utekelezaji wa Mapendekezo ya CAG ukurasa wa 606 hoja namba 8 katika aya ya 4.3 ambapo Serikali inaeleza kwamba Menejimenti ya TANESCO ilitoa nyongeza ya muda bila mazingatio ya kisheria na kimkataba (ex gratia time) kukamilisha mradi kwa mkandarasi, hivyo faini itaanza kutozwa kuanzia Juni 15,2023.

Uchambuzi na Maswali ya kujiuliza

(i) Wakati wa ukaguzi CAG hakukuta jitihada zozote zinazofanywa na Management ya TANESCO kudai tozo ya fidia ya ucheleweshaji wa mwaka mmoja wa mradi, Ex Gratia time ilitolewa wakati gani?.

(ii) Tozo ya fidia ya ucheleweshaji ya 5% ya thamani ya Mradi imewekwa katika kifungu cha 8.7 kifungu kidogo cha 2.5, Menejimenti ya TANESCO ilipata wapi nguvu ya kisheria na kimkataba kutoa ex gratia time? Katika jambo ambalo limeamuliwa kimkataba na pande zote kusaini.

TANESCO imekuwa ikilipa faini na adhabu zote kampuni ya Arab Contractors inapokiuka mkataba mfano kukosekana kwa umeme eneo la ujenzi wa mradi na mambo mengine.

(iii) Waziri wa Nishati na Menejimenti ya TANESCO hawana mamlaka kisheria kufuta mapato ya nchi kiasi cha shilingi Bilioni 327.93?.

(iv) Wabunge tulihoji hapa bungeni sababu za kutotozwa faini hii, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti na Kamati ya Nishati kwa nyakati tofauti tofauti zililiripoti bungeni kuwa ucheleweshaji wa mradi ulisababishwa na uzembe wa mkandarasi.

Nini kilichowasukuma Waziri wa Nishati na Menejimenti ya TANESCO kutoa ex gratia time? Kwa kampuni iliyozembea.

(v) Aliyekuwa Waziri wa Nishati, Mhe. Januari Makamba katika jitihada za kumlinda Mkandarasi Kampuni ya Arab Contractors isilipe faini hiyo kwa nyakati tofauti,ndani ya Bunge (ushahidi wa hansard) alieleza kuwa ucheleweshaji huo ulisababishwa na Uviko-19, kuchelewa kufika kwa Crane na kupinga hadharani muda aliyopewa mkandarasi katika mkataba akisema ulikuwa mfupi mno asingeweza kukamilisha ujenzi.

Maelezo ambayo yalikinzana na taarifa ya kitaalamu iliyotolewa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Leonard Masanja aliyoitoa katika Kamati ya Bajeti. Pia, maelezo hayo yalipingwa vikali na wabunge, lakini bado Waziri akaenda kutoa Ex Gratia time kwa mkandarasi. Uamuzi huu ulifanywa na Waziri kwa manufaa ya nani?.

Design ya mradi ilitaka mkandarasi ajenge matuta matatu ya kuchepushia maji, lakini mkandarasi alikataa na kujenga tuta moja, hali iliyopelekea maji kujaa na kazi kusimama kwa muda mrefu.

(vi) Waziri wa Nishati aliwahi kutoa maelezo kinzani hapa bungeni na kwamba alikuwa hajui mradi utakamilika lini hadi Spika uliingilia kati na kutoa maelekezo kwa Serikali ukimtaka Waziri Mkuu atoe taarifa sahihi bungeni ni lini mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere utakamilika. Leo mambo ya ex gratia time yanatoka wapi?.

Kwa kuwa, Serikali haina majibu ya msingi kuhusu hoja hiyo ya CAG kutoza faini ya ucheleweshaji kiasi cha Tsh. Bilioni 327.93 kwa Mkandarasi Arab Contractors,na kwa kuwa, Bunge lilishaiagiza Serikali kutoza faini hiyo muda mrefu, lakini Waziri amekaidi maagizo ya Bunge (ushahidi wa hansard) hali inayoonyesha kuna njama baina ya watumishi wa umma na mkandarasi kuwaibia watanzania.

Hivyo basi, kwa kuwa hoja hii haikuletwa na kamati naomba kuongeza mapendekezo mapya mawili kwamba Bunge liiagize Serikali kufanya yafuatayo:-

(i) Aliyekuwa Waziri wa Nishati, Mhe. January Makamba na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO, Maharage Chande na iliyokuwa Bodi ya TANESCO na Mkurugenzi wa Kampuni ya Arab Contractors wakamatwe na washtakiwe kwa makosa ya kula njama ya kuiibia Serikali na makosa ya uhujumu uchumi.

(ii) Serikali ihakikishe kuwa fedha za umma kiasi cha Bilioni 327.93 zinalipwa na Kampuni ya Arab Contractors na si vinginevyo.

3.2.2 Hoja ya kuchelewa kutekeleza miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) katika mradi wa JNHPP kwa kipindi cha miaka mitatu na miezi 11 na sasa ni karibu miaka mitano.

Pia, suala hili halipo kwenye taarifa ya kamati, lakini katika Taarifa ya Majumuisho ya majibu ya Serikali na Mpango kazi wa utekelezaji wa Mapendekezo ya CAG ukurasa wa 607, hoja ya 10 aya ya 4.5 ambapo Serikali inaeleza kuwa majadiliano yanaendelea ya kukubaliana miradi ya kutekelezwa kwa utaratibu wa CSR na kwa kuanzia wataanza kujenga mradi wa Chuo cha Ufundi cha umeme na gesi huko mkoani Lindi.

Uchambuzi na Maswali ya kujiuliza

(i) Suala hili ni la kimkataba ambapo Mkandarasi anapaswa kutoa 4% ya thamani ya mradi kama CSR, hivyo katika mradi huo ni jumla ya shilingi Bilioni 270, ni mazungumzo gani yasiyo na mwisho hadi yachukue miaka 5?.

(ii) Mradi huu uko hatua za mwisho kukamilika zaidi ya 90%, je miradi hiyo ya kijamii itatekelezwa wakati gani? Kwani mkandarasi atakamilisha mradi na kuondoka kabla miradi ya kijamii haijatekezwa.

(iii) Bunge lilishaigiza Serikali kuitaka Kampuni la Arab Contractor kutekeleza miradi ya SGR kwa mujibu wa Mkataba. kwanini agizo hili halitekelezwi? Na Je mradi wa chuo cha umeme na gesi unaotarajiwa kujengwa una thamani gani? Ikilinganishwa na fedha za CSR tunazodai mkandarasi.

Kwa kuwa, danadana zinazopigwa na Serikali zinalenga kumuokoa mkandarasi asitekeleze miradi ya CSR iliyowekwa kwa mujibu wa mkataba na kwa kuwa, mradi huo uko hatua za mwisho na kwamba mkandarasi hatakuwa na muda wala nafasi ya kutekeleza miradi ya CSR na kwamba hata mradi wa ujenzi wa Chuo cha Umeme na Gesi huko Lindi haujaelezwa una thamani gani na utaanza lini.

Hivyo basi, naomba niongezee maazimio mawili katika Taarifa ya Kamati ya PAC kwamba Bunge liamue yafuatayo:-

(i) Mkandarasi Arab Contractors akatwe fedha kiasi cha shilingi Bilioni 270 za CSR na utekelezaji wa miradi hiyo uanze mara moja,

(ii) Hatua kali zichukuliwe kwa aliyekuwa Waziri wa Nishati, January Makamba na aliyekuwa Mkurugenzi wa TANESCO, Maharage Chande na iliyokuwa Bodi ya TANESCO na Mkandarasi Kampuni ya Arab Contractor washtakiwe kwa kosa la kula njama kuiibia Serikali na makosa ya uhujumu uchumi.

3.2.3 Hoja ya TANESCO kushindwa kuidai IPTL kiasi cha dola Milioni 148.4 sawa na shilingi Bilioni 370


Kamati imelieleza suala hili kwa kina katika ukurasa wa 30 kipengele cha 2.2.1,kwa mujibu wa taarifa ya CAG 2021/2022,TANESCO kushindwa kudai malipo ya shilingi Bilioni 370 kutoka Kampuni ya IPTL baada ya Serikali kushinda kesi Machi 2021,fedha hizi zinatakiwa kupatikana ili kulipa deni Benki ya Standard Chartered Hong Kong dola za Marekani milioni 148.4 pamoja na riba kama ilivyoamuriwa na Kituo cha Kimataifa cha kutatua migogoro ya uwekezaji.

Kitendo cha kushindwa kukusanya fedha hizi kutaifanya Serikali ilipe mkopo pamoja na riba kwa Benki ya Standard Chartered Hong Kong. Nini kilichofanya Wizara ya Nishati, Wizara ya Fedha na TANESCO washindwe kudai IPTL madai hayo halali kwa amri ya Mahakama.

Kufuatia uamuzi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Tarehe 1 Machi 2021 iliitaka IPTL iilipe TANESCO Dola za Marekani Milioni 148.4 ili kutekeleza hati ya fidia iliyotiwa saini tarehe 27 Oktoba 2013 ambayo inalinda hatua ya Serikali kutoa fedha kwenye Akaunti ya Escrow kutokana na madai ya wahusika wa nje.

Hata hivyo, hadi Disemba 2022 IPTL hawakuwa wamelipa kiasi kinachodaiwa na kwa mujibu wa majumuisho ya majibu ya Serikali ukurasa wa 614 hoja namba 17 aya ya 2.11.12/5.2.5 hakuna utekelezaji wa aina yoyote hadi leo hii tunapo ongea hapa Bungeni.

Nilikuwepo Bungeni wakati Fedha zinatolewa kwenye akaunti ya Escrow na kupewa IPTL, wabunge tulikataa lakini tulibishiwa na viongozi wakuu wa Serikali kwamba fedha hizo sio za umma na akakabidhiwa mabilioni ya fedha IPTL, Bunge likatoa maazimio chini ya Spika Mhe. Anna Semamba Makinda ya kutaka fedha hizo zirudishwe na mitambo ya IPTL itaifishwe na Serikali jambo ambalo halijatekelezwa na Serikali hadi leo.

Mmiliki wa IPTL, Habinder Sigh Seth na mwenzake Rugemalila walishakamatwa na kufikishwa mahakamani kwa makosa ya uhujumu uchumi na baadaye wameachiliwa huru bila maelezo yoyote.

Waziri wa Fedha, Waziri wa Nishati na Mwanasheria Mkuu wa Serikali walioruhusu fedha hizo zitoke wapo na wana nafasi kubwa serikalini, leo zinapigwa danadana tena katika kudai fedha hizo.

Kwa kuwa, hakuna sababu zozote za msingi za Serikali kushindwa kudai fedha hizo kwa IPTL,na kwa kuwa, Mahakama Kuu ya Tanzania ilishatoa maamuzi ambayo yameshindwa kutekelezwa na Serikali kwa miaka 3 sasa hali inayoonyesha kuwa kuna njama baina ya watumishi wa Serikali na Mmiliki wa IPTL kupoteza mapato ya Serikali.

Hivyo basi, naomba niongezee maamizio mawili kwenye Taarifa ya Kamati ya PAC kwamba Bunge liiagize Serikali kufanya yafuatayo:-

(i) Hatua kali za kiutawala na za kisheria zichukuliwe ikiwemo kukamatwa na kushtakiwa kwa makosa ya kula njama na kuiibia nchi na makosa ya uhujumu uchumi kwa aliyekuwa Waziri wa Nishati, Mhe. January Makamba na aliyekuwa Mkurugenzi wa TANESCO,Maharage Chande na Mmiliki wa IPTL, Habinder Sigh Seth wote waliohusika na kuisababishia Serikali hasara ya shilingi Bilioni 370.

(ii) Serikali iitake IPTL kwa haraka kulipa fedha kiasi cha Dola za Marekani Milioni 148.4 pamoja na riba kama Mahakama Kuu ya Tanzania ilivyoamuru.

3.3. Hoja ya CAG kuhusu mikopo na Deni la Serikali

Hoja hii haikuelezwa na Kamati na haimo katika majumuisho ya majibu ya Serikali. Kwa mujibu wa taarifa ya CAG 2021/2022 Serikali Kuu jedwali na 17 ukurasa wa 56 linaonyesha kuwa Serikali imekopa nje ya bajeti iliyoidhinishwa na Bunge na bila ridhaa ya Bunge kiasi cha shilingi Trilioni 1.285.

Pia jedwali hilo linaonyesha kuwa kiasi cha shilingi Trilioni 2.531 fedha za mikopo hazikupokelewa katika Mfuko Mkuu wa Serikali kwani fedha hizo zilipokelewa kwenye akaunti za wafadhili na zingine zilipokelewa moja kwa moja kwenye miradi.

Waziri wa Fedha alikopa fedha hizi kiasi cha shilingi Trilioni 1.285 kwa ajili ya shughuli gani na kwa ridhaa ya nani? Fedha na kazi zilizopangwa katika bajeti ya mwaka 2021/2022 zilipitishwa na kuidhinishwa na Bunge tena kwa kupigiwa kura ya NDIYO,

Fedha za ziada alizokopa Waziri wa Fedha ni kwa ajili ya shughuli gani na kwa ridhaa ya nani?. Waziri wa Fedha alipata wapi mamlaka ya kukopa fedha na kupeleka moja kwa moja kwenye miradi kiasi cha shilingi Trilioni 2.531 badala ya fedha hizo kupokelewa Mfuko Mkuu wa Serikali kwanza kabla ya matumizi kama Katiba na Sheria za nchi zinavyotaka ili kuwepo na uwazi na usimamizi makini wa fedha za umma.

Waziri wa Fedha alilenga kuficha nini na je fedha hizo zilipelekwa kwenye miradi gani mbona nayo imefichwa.


Kwa mujibu wa Sheria ya mikopo ‘Government Loans,Guarantees and Grants Act’ ambapo mamlaka ya kukopa mikopo amepewa Waziri wa Fedha kwa niaba ya Serikali na atafanya hivyo kwa kuzingatia ukomo uliowekwa na Bunge kupitia Bajeti iliyoidhinishwa na endapo katika utekelezaji wa bajeti kutakuwa na mahitaji mapya atapata kibali cha Bunge.

Katika mwaka wa fedha 2021/2022 ilipotokea ongezeko la mikopo la shilingi Trilioni 1.31 kutoka IMF kwa ajili ya kutekeleza mpango wa kukabiliana na hali ya uchumi baada ya kupungua kwa ugonjwa wa Covid 19 bajeti ilifanyiwa marekebisho kupitia Bunge kutoka Trilioni 36.68 hadi Trilioni 37.99.

Hapa Waziri wa Fedha alizingatia matakwa ya Sheria ya Mikopo inavyotaka ambapo Bunge liliridhia kwa kauli moja na hakukuwepo malalamiko.

Swali la kujiuliza kwa nini Waziri wa Fedha aukwepe Mfuko Mkuu wa Serikali na kwa nini akope zaidi ya kiwango kilichoruhusiwa na Bunge.

Maamuzi ya Waziri wa Fedha yamekwenda kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sheria ya Bajeti,Sheria ya Fedha na Sheria ya Mikopo lakini pia ni matumizi mabaya ya ofisi kwenye Sheria ya Kanuni ya Adhabu.

Kwa kuwa, Waziri wa Fedha hana majibu kuhusu hoja ya ukopaji nje ya bajeti na mikopo kutopitia mfuko mkuu wa Serikali na kwa kuwa, wabunge kwa niaba ya wananchi wameomba kupewa majibu ya kina juu ya suala hili bila mafanikio.

Hivyo basi, naomba kuongeza maazimio mawili katika taarifa ya Kamati ya PAC kwamba Bunge liiagize Serikali kufanya yafuatayo:-

(i) CAG na TAKUKURU wafanye uchunguzi na ukaguzi maalum ili kubaini sababu zilizomsukuma Waziri wa Fedha kukopa na kutumia fedha za mikopo nje ya bajeti iliyopitishwa na Bunge pamoja na kuthibitisha uhalali wa matumizi yaliyofanywa.

(ii) Hatua kali za kiutawala na kisheria zichukuliwe kwa Waziri wa Fedha, Mhe. Dk. Mwigulu Nchemba na aliyekuwa Mlipaji Mkuu wa Serikali, Ndg. Emmanuel Tutuba na wahusika wengine wote kukamatwa na kushtakiwa kwa makosa ya uhujumu uchumi ambao umepelekea kuliingiza taifa kwenye hasara na mzigo mkubwa wa madeni.

HITIMISHO

Kwa hoja 5 tu nilizozitaja hapo juu za SGR, Bwawa la Mwalimu Nyerere, IPTL na Mikopo inafikia Tsh. Trilioni 6.5 kati ya Trilioni 30 ambazo zipo kwenye Jedwali la Ubadhirifu na Upotevu wa Fedha za Umma.

Kwa mwenendo huu nchi yetu itaendelea kufilisika na hatutuweza kufikia malengo ya kuleta na kutoa huduma bora kwa watanzania.

Ukipitia taarifa ya Kamati na majumuisho ya majibu ya Serikali huoni hatua mahususi zilizochukuliwa na Serikali tangu taarifa ya CAG iwasilishwe Machi 2023 mbele ya Mhe. Rais na Bunge Tukufu.

Katika taarifa ya CAG kuna maeneo ambayo Mawaziri wamehusika moja kwa moja na maeneo mengine wameshindwa kuchukua hatua stahiki kwa watuhumiwa wa ubadhirifu wa fedha za umma.

Kwa fursa hii ni wajibu wetu waheshimiwa wabunge kuisimamia Serikali kikamilifu ili kuhakikisha kuwa fedha na raslimali za umma zinalindwa kwa nguvu zote na kuhakikisha kuwa wabadhirifu,wezi, wala rushwa na mafisadi wote wanakamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria lakini pia kuhakikisha kuwa fedha za umma zinafidiwa.


Hivyo, niwaombe waheshimiwa wabunge mniunge mkono mapendekezo yangu ili tutokomeze wizi na ufisadi katika taifa letu. Pia nimembatisha Jedwali la Ubadhirifu na Upotevu wa Fedha za Umma kiasi cha shilingi Trilioni 30;
Nawasilisha,
…………………………………….
Luhaga Joelson Mpina (Mb)
Mbunge wa Jimbo la Kisesa

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news