Muswada wa Bima ya Afya kwa Wote kutinga bungeni

DODOMA-Serikali kupitia Wizara ya Afya inatarajia kupeleka tena Muswada wa Bima ya Afya kwa Wote bungeni leo Novemba 1,2023 ambao ulikwama mwezi Februari mwaka huu baada ya hoja iliyotolewa na Bunge ya kutokuwepo kwa chanzo endelevu cha fedha kutekeleza mpango huo.
Muswada huu ni ndoto ya Serikali ya miaka mingi ambapo Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amehakikisha uboreshaji wa huduma bora za afya kuanzia ngazi ya Taifa hadi ya msingi ili wananchi watakapojiunga na Bima ya Afya waweze kupata huduma karibu na maeneo yao.

Akielezea utayari wa muswada huo kuwasilishwa bungeni, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Afya, Bw. Englibert Kayombo amesema, Serikali kupitia Wizara ya Afya, Wadau wa Sekta na Wataalam wengine tayari wamefanyia kazi hoja zote zilizoibuliwa na Bunge.

Sambamba na wadau, hata hivyo semina elekezi zimefanyika kwa makundi mbalimbali ndani ya jamii kuhusu umuhimu wa Bima ya Afya kwa wote na maoni yaliyopatikana yalifanyiwa kazi, hivyo wananchi kesho watege macho na masikio yao Bungeni kujua nini ambacho Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu atawasilisha Bungeni.

Amesema kuwa kupitishwa kwa muswada huo kutawezesha kila Mtanzania kuwa ndani ya Mfumo wa Bima ya Afya hatua itakayoboresha zaidi upatikanaji wa huduma za matibabu bila kuwa na kikwazo cha fedha.

“Serikali yetu ni sikivu na imefanyia kazi hoja zote zilizoibuliwa na Waheshimiwa Wabunge ambao ndio wawakilishi wa wananchi hivyo yaliyomo ndani ya muswada huo yamelenga kuwasaidia wananchi kupata huduma bora za afya bila ya kikwazo cha fedha,"amesema Bw. Kayombo.

Kuhusu gharama za vifurushi, Kayombo amesema kuwa mara baada ya Muswada huo kupita na kuwa Sheria, kanuni zitatungwa ili kuratibu suala ya gharama za vifurushi na kusema kuwa uchambuzi utafanyika ili vifurushi viwe vya gharama nafuu na kila mwananchi aweze kuwa na bima ya afya.

Ameongeza kuwa, kwa upande wa Serikali imeshakamilisha maandalizi ya kutoa huduma kwa wananchi kupitia mfumo wa bima ya afya kwa wote ambapo imeboresha ubora wa huduma katika vituo vyake vya kutolea huduma ikiwemo upatikanaji wa dawa, ununuzi na usimikaji wa vifaa na vifaa tiba pamoja na ajira za watumishi.

“Kwa sasa nchi yetu iko mbali sana katika utoaji wa huduma, tuna vifaa vya kisasa vya uchunguzi wa magonjwa, huduma nyingi za kibingwa zinapatikana hapa nchini lakini pia huduma za afya zimesogezwa sana kwa wananchi hivyo kama nchi tupo tayari kutekeleza hili, nia na uwezo wa kufanya hivyo tunao”. Amesema Bw. Kayombo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news