NEC kufanya zoezi la uboreshaji wa majaribio daftari la kudumu la wapiga kura

DODOMA-Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) inatarajia kufanya zoezi la uboreshaji wa majaribio wa daftari la kudumu la wapiga kura katika Kata ya Ng’ambo iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, Mkoa wa Tabora na Kata ya Ikoma iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Rorya, Mkoa wa Mara kuanzia tarehe 24 hadi 30 Novemba, 2023.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa yua Uchaguzi, Ramadhan Kailima (kushoto) na Mkurugenzi wa Idara ya Uandikishaji wa Daftari la Kudumu la Mpiga Kura na Tehama, Geofrey Mpangala (kulia) wakionesha BVR Kits zenye vifaa mbalimbali vinavyowasiliana ili kuchukua na kutunza taarifa za wapiga kura.

Akitangaza uboreshaji huo leo Novemba 10,2023 wakati akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Bw. Ramadhani Kailima amesema zoezi hilo litafanyika katika vituo 16 vya kuandikisha wapiga kura kati ya hivyo vituo 10 ni katika kata ya Ng'ambo na 6 vipo kata ya Ikoma.

“Uboreshaji wa majaribio utahusisha kuandikisha raia wa Tanzania mwenye umri wa miaka 18 au zaidi na atakayetimiza umri wa miaka 18 kabla au ifikapo tarehe ya uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 , wapiga kura wanaoboresha taarifa zao ambao wamehama kutoka eneo moja la uchaguzi kwenda eneo jingine, wapiga kura waliopoteza sifa za kuwemo daftarini,”amesema Bw. Kailima.

Kailima amesema lengo la kufanya majaribio hayo ni kupima uwezo wa vifaa na mifumo ya uandikishaji itakayotumika wakati wa uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura unaotarajiwa kufanyika nchi nzima kwa tarehe na ratiba itakayopangwa na tume.

Mkurugenzi wa Habari na Elimu ya Mpiga Kura, Bi. Giveness Aswile akizungumza jambo katika mkutano huo.

“Katika zoezi hili tume itatumia BVR Kits zenye vifaa mbalimbali vinavyowasiliana ili kuchukua na kutunza taarifa za wapiga kura, BVR Kits hizo zimeboreshwa na ni tofauti na zile zilizotumika katika zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura mwaka 2015 na 2019,”amesema Kailima.

Aidha, Kailima amesema Tume imesanifu na kuboresha mfumo wa uandikishaji wa Wapiga Kura (Voters Registration System-VRS) ili kukidhi muundo na BVR Kits za sasa ambazo zinatumia programu ya android tofauti na BVR Kits za awali ambazo zilikuwa zinatumia programu ya Microsoft Windows.

“Mfumo wa uandikishaji ulioboreshwa utawawezesha wapiga kura ambao wameshaandikishwa na wapo kwenye daftari la wapiga kura, kuanzisha mchakato wa kuboresha taarifa zao ama kwa kubadilisha kituo cha kupigia kura iwapo amehama Mkoa au Wilaya nyingine au kurekebisha taarifa zao kwa njia ya mtandao kwa kutumia simu zao za mkononi au kompyuta,”amesema Kailima.

Amesema kuanzisha mchakato mtandaoni, mpiga kura ataingia kwenye tovuti ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi www.nec.go.tz kwa kutumia kompyuta au simu janja kisha atabonyeza kiunganishi (link) kilichoandikwa “Boresha Taarifa za Mpiga Kura” au atatumia anuani ya ovrs.nec.go.tz itakayompeleka moja kwa moja kuanzisha mchakato. Baada ya kufuata utaratibu huo, mfumo utamletea ukurasa wenye vipengele vitakavyomruhusu kuweka taarifa zake kulingana na mahitaji.

“Baada ya kukamilisha taratibu zote na kuwasilisha taarifa kwenye mfumo, mpiga kura atapokea ujumbe mfupi wenye kumbukumbu namba kupitia namba yake ya simu aliyoitumia wakati wa kuboresha taarifa zake kwenye mtandao. Kumbukumbu namba hiyo atakwenda nayo kwenye kituo cha kuandikisha wapiga kura kwa ajili ya kumalizia hatua zilizobaki na kupatiwa kadi,”amesema Kailima.

Katika hatua nyingine Bw.Kailima amesema kuwa uboreshaji huo utahusisha vyama vya siasa kwa kuweka wakala mmoja katika kila kituo cha kuandikisha wapiga kura lengo likiwa ni kushuhudia na kujiridhisha kuhusu taratibu zitakazotumika wakati wa uboreshaji wa majaribio wa daftari.

Amesema utaratibu huo wa uboreshaji wa taarifa kwa njia ya mtandao hautawahusisha wapiga kura wapya wanaotaka kuandikishwa kwa mara ya kwanza na waliopoteza kadi zao au kuharibika.

“Hawa wanashauriwa wafike kwenye kituo cha kuandikisha wapiga kura na kufuata taratibu watakazo elekezwa na maafisa wa Tume watakaokuwepo kwenye kituo,”amesema.

Pia, Kailima amesema Tume inatoa wito kwa wananchi wenye sifa zilizotajwa wa Kata ya Ng’ambo iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora na Kata ya Ikoma iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Rorya, kujitokeza kwa wingi kushiriki katika uboreshaji wa majaribio wa Daftari na kutoa ushirikiano kwa Tume wakati wote wa utekelezaji wa jukumu hili muhimu kwa mustakabali wa Taifa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news