Waelezeni wananchi mafanikio Sekta ya Afya-Dkt.Dugange

DODOMA-Viongozi katika sekta ya afya wametakiwa kuyasema kwa wananchi mafanikio yanayopatikana katika sekta ya afya ili wafahamu kazi nzuri inayofanywa na serikali katika kuboresha huduma za afya nchini.

Maagizo hayo yametolewa leo Novemba 27, 2023 na Naibu Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Festo Dugange wakati akifungua kikao kazi cha kujadili utekelezaji wa Mpango wa Afua za Takwimu za Bidhaa za Afya (IMPACT) jijini Dodoma.

Dkt.Dugange amesema kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya.

Ni kwa kujenga vituo vya kutolea huduma za afya,ununuzi wa dawa na vifaa tiba pamoja na kuajiri wahudumu wa afya, hivyo ni jukumu la kila kiongozi kuyasemea mafanikio hayo kwa wananchi.

“Serikali imefanya makubwa sana na nyie wote ni mashahidi, lakini kasi ya kuyasemea hayo ni ndogo. Wananchi wengine hawafamu kama kuna huduma bora zinapatikana, hivyo ni jukumu la viongozi wote kuyasemea haya.

"Tumeanzisha utaratibu kwa kushirikiana na Wizara ya Habari na Teknolojia kwa kila mkoa kuelezea mafanikio haya kwenye vyombo vya habari na nyinyi waganga wakuu wa mikoa na wilaya mnatakiwa kuisemea sekta ya afya. Tusiwe wanyonge na kujiona duni wakati mambo mazuri yapo,‘’amesema Dkt.Dugange.

Akizungumzia kuhusu vifaa tiba vilivyonunuliwa na Serikali,Dkt.Dugange amewaagiza wahudumu wote kuvitunza vifaa hivyo ili viweze kudumu kwa muda mrefu.

“Vifaa hivi ni gharama sana,hivyo mnatakiwa kuvitunza na kuvifanyia matengenezo mara kwa mara. Pia mtunze miundombinu ya majengo pamoja na magari mliyopewa hivi karibuni.Tutawachukulia hatua viongozi wote wazembe mtakaozembea kutekeleza maagizo haya.”

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI anayeshughulikia Afya,Ustawi wa Jamii na Lishe, Dkt.Charles Mahera amewaagiza waganga wakuu wa mikoa kudhibiti wizi wa vifaa tiba na dawa unaotokea sehemu mbalimbali nchini.

“Tumekuwa tukipokea taarifa za wizi wa madawa na vifaa tiba,nendeni mkasimamie hilo hasa mikoa ya mipakani ambako dawa zinaibiwa sana.

"Jana tumeona Hospitali ya Mkoa wa Njombe kuna seti za televisheni zimeibiwa. Msipodhibiti hilo mnahujumu juhudi zinazofanywa na serikali katika kuboresha huduma za afya nchini,”amesema Dkt.Mahera.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news