Haya hapa maagizo ya Waziri Mchengerwa kwa wakuu wote wa mikoa nchini

DODOMA-Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI), Mhe. Mohamed Mchengerwa amewaagiza wakuu wa mikoa kutekeleza maagizo mbalimbali ili mchakato wa kuwapokea wanafunzi wapya shule za awali, msingi na sekondari uende kwa ufanisi kuanzia Januari 6,2024.
Mhe. Mchengerwa, ametoa agizo hilo leo Jumamosi Desemba 30,2023 wakati akizungumza na wakuu wa mikoa katika kikao kazi kilichofanyika kwa njia ya mtandao ambapo viongozi hao walieleza hatua zilizofikiwa katika miradi ya elimu na walivyojipanga kuwapokea wanafunzi wapya.

Hata hivyo, wakuu wa mikoa hao kwa nyakati tofauti wakiwasilisha maelezo yao kuhusu utekelezaji wa miradi ya elimu walimhakikishia Waziri Mchengerwa kuwa hakuna mwanafunzi atakayekaa chini au kukosa darasa na kuwa wote walioandikishwa na kufaulu wataanza masomo kwa wakati mmoja.

Aidha, Waziri Mchengerwa ameagiza kuwa wakuu wa mikoa ambao bado hawajakamilisha ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya elimu kuhakikisha wanakamilisha baadhi ya majengo ya vyumba vya madarasa ifikapo Januari 15 kama walivyoahidi wakati wanatoa taarifa ya utekelezaji wa miradi ya elimu katika mikoa yao.

“Mimi na wasaidizi wangu tutapita kila mkoa, halmashauri na wilaya kukagua miradi mbalimbali ya elimu kama ambavyo mlimewekq ahadi za utekelezaji,” amesema.

Maagizo mengine aliyoyatoa ni pamoja na shule zote mpya zinazojengwa zisajiliwe hususan ni zile za wasichana na baada ya mchakato huo kukamilika zianze kazi mara moja ya kupokea wanafunzi. Amesema baadhi ya mikoa ukiwamo wa Pwani wameanza mchakato huo.

Amesema, kuna mikoa wamekamilisha ujenzi wa shule mpya kati ya asilimia 75 hadi 80, lakini bado shule hizo hazijasajiliwa wala kupokea wanafunzi, maelekezo yangu kwa wakuu wa mikoa shule zote zisajiliwe.

“Naomba msimamie usajili na mapokezi kwa wanafunzi wanaojiunga na elimu ya awali na darasa la kwanza na kidato cha kwanza. Hakikisheni wanafunzi wanasajiliwa bila masharti,” amesema Mchengerwa.

Waziri huyo amewataka wakuu wa mikoa kusimamia vema bajeti ya chakula kwa wanafunzi katika shule zote za bweni ili kuhakikisha wanapata chakula hicho

Mhe.Mchengerwa amesema, kwa kuwa Januari mwaka 2024, Serikali inaanza kutekeleza mtaala mpya wa darasa la kwanza na darasa la tatu, "Wakuu wote wa Mikoa mnatakiwa kusimamia maelekezo yaliyoanishwa katika sera mpya ya elimu."

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila amesema, katika mradi wa kuimarisha elimu ya sekondari walipokea Sh 13.0 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa shule za sekondari 15 kati ya hizo 13 zimekamilika huku zingine zikiendelea na ukiendelea.

“Tulipokea pia shule 15 za msingi kati ya hizo 13 zimekamilika, katika taarifa yetu Dar es SWalaam, kuna shule nne ambazo hazijamilika. Lakini mkoa wa Dar es Salaam una changamoto ya ardhi, ndio maana kuna shule tunajenga shule kwa mfumo wa maghorofa,” amesema Chalamila.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news