WASHINGTON-Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, pamoja na Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila, wameshiriki Mkutano wa Mawaziri wa Fedha na Magavana wa Benki Kuu za Afrika, uliofanyika katika Ofisi za Kamisheni ya Umoja wa Afrika, sambamba na mikutano ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), mjini Washington D.C., Marekani.
Mkutano huo ulikuwa na lengo la kujadili maeneo ya kipaumbele ambayo nchi za Afrika zinapaswa kuyasukuma kama ajenda maalum katika mikutano ya Kundi la Nchi 20 Tajiri Duniani (G20) kwa mwaka 2025, ambapo Afrika Kusini inahudumu kama Mwenyekiti wa G20.Aidha, mjadala katika mkutano huo uliangazia umuhimu wa Afrika kuwa na sauti moja katika kushawishi nchi za G20 kufanya mabadiliko yatakayorahisisha upatikanaji wa fedha na mikopo nafuu kwa nchi zinazoendelea.
Pia, walijadili namna ya kukabiliana na changamoto ya madeni, ambalo ni tatizo linalozikumba nchi nyingi za Afrika kutokana na mabadiliko ya kiuchumi, kijiografia, na kisiasa.


