Simba ya Kimataifa

NA DR MOHAMED MAGUO

LEO Aprili 27,2025 timu ya Simba ya Tanzania imefuzu kuingia fainali ya Kombe la Shirikisho barani Afrika (CAF Confederation Cup) kwa kuiondosha timu ya Stellenbosch FC ya Afrika ya Kusini.
Ni kupitia mitanange ambayo imepigwa na kuitoa katika hatua ya Nusu fainali ya Kombe hilo baada ya kuifunga goli moja kwa nunge uwanja wa Amani Complex,Zanzibar wiki moja iliyopita.

Hakika Simba ni timu Bora fahari ya Tanzania. Mchezo wa marudiano umechezwa leo Moses Mabhida Stadium mjini Durban nchini Afrika Kusini na kutoka sare ya kutofungana. Endelea na utenzi huu hapa chini ujifunze jambo;

¹Kwa ukanda wa Afrika
Ya kati na masharika
Ni simba inayoshika
Namba moja kwa ubora

²Simba hii kwa hakika
Ni ngumu kukamatika
Kila siku yasifika
Magoli kutumbukiza

³Mashabiki wanacheka
Furaha isosemeka
Kwamba Simba imefika
Fainali kwa kishindo

⁴Simba i pamechimbika
Hata Sauzifrika
Steleboshi ametoka
Ubaya jama ubwela

⁵Steleboshi nyakanyaka
Kwa mnyama 'meshikika
Masare yamesambuka
Mnyama ametoboa

⁶Taifa kuheshimika
Ni Stele kuanguka
Na Simbaye' kusomeka
Fainali 'meingia

⁷Kongole nazipeleka
Msimbazi wakawaka
Heshima mmeiweka
Heko kwenu wana Simba

⁸Simba i twajivunia
Timu yetu Tanzania
Vijana wametimia
Soka la kimataifa

⁹Nguvu moja nakwambia
Ndugu yangu we sikia
Simbaye' tumainia
Kombe italifumbata

¹⁰Watu wote wafurahia
Kwa sana washabikia
Shwangwe wanashangilia
Simba ni mkali sana

MTUNZI
Dkt. Mohamed Omary Maguo
Mshairi wa Kisasa
Mhadhiri Mwandamizi
Mkuu wa Itifaki
Chuo Kikuu Huria cha Tanzania
27/04/2025

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news