ARUSHA-Taasisi nunuzi nchini zimeshauriwa kuzingatia sheria, kanuni, miongozo iliyowekwa kwa mujibu wa sheria na kuwa na maadili ili kukomesha mambo ambayo ni kinyume na matarajio ya Serikali.
Hayo yameelezwa na Kamishna wa Sera ya Ununuzi wa Umma, Dkt. Frederick Mwakibinga wakati wa Kongamano la tisa la Ununuzi wa Umma la mwaka 2025 linaloendelea katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa AICC jijini Arusha.Alisema kuwa uzingatiwaji wa Sheria utaweza kupunguza kiwango cha upotevu wa mali na kuchukua hatua ambazo zimewekwa katika Sheria ili kukomesha mambo ambayo ni kinyume na matarajio ya Serikali na kuhakikisha kwamba fedha za umma zinalindwa kadiri inavyowezekana.
“Kama mnavyofahamu ununuzi wa umma ni moja kati ya nyenzo zinazotumika kwa manufaa mbalimbali ikiwemo kuutumia ununuzi wa umma kwa kuzinufaisha kampuni za wazawa ili ziweze kukua na kuwa na mchango katika maendeleo ya nchi, kuyajali makundi mbalimbali ya jamii ambayo yakiachwa bila kusaidiwa au kuwezeshwa yanapata ugumu katika ushindani wa soko la ununuzi wa umma,”amesema Dkt. Mwakibinga
Dkt. Mwakibinga alisema, kongamano hilo muhimu limekutanisha, Wadau wa Ununuzi wa Umma kwa maana ya Watendaji wa Umma, Makampuni, Viongozi, Wafanyabiashara na watu mbalimbali ili kufanya majadiliano ya kujenga himaya ya Ununuzi wa Umma iliyo thabiti.


