BoT yaendelea kusimamia uthabiti wa sekta ya fedha kuchochea ukuaji endelevu wa uchumi na maendeleo ya taifa

DAR-Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dkt.Yamungu Kayandabila amesema, kuwa Benki Kuu inaendelea kusimamia uthabiti wa sekta ya fedha ili kuchochea ukuaji endelevu wa uchumi na maendeleo ya taifa kwa ujumla.
Dkt.Kayandabila ameyasema hayo leo Agosti 27,2025 aliposhiriki katika mjadala wa Jukwaa la Biashara la Maafisa Watendaji Wakuu, lililofanyika jijini Dar es Salaam.

Amesema kuwa, sekta ya fedha nchini inaendelea kukua na kuimarika, hivyo ni lazima iwe ya ushindani, jumuishi, yenye ufanisi na gharama nafuu.
Aidha, amebainisha kuwa Benki Kuu imeendelea kuweka mazingira rafiki kwa sekta mbalimbali nchini, ikiwemo kilimo, ambapo shilingi trilioni moja imetengwa kwa ajili ya kusaidia mikopo ya kilimo. Kupitia Mfuko huo, benki zinazoshiriki zinatoa mikopo kwa riba isiyozidi asilimia 10.

Aliongeza kuwa, BoT inaendelea kufanya mapitio ya mfuko huo ili kusaidia upatikanaji wa mikopo kwa sekta nyingine muhimu kama vile uzalishaji na nishati.
Dkt. Kayandabila pia alisema kuwa, Benki Kuu inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa, ikiwemo kudhibiti mfumuko wa bei, kusimamia uthabiti wa thamani ya shilingi, na kuhakikisha upatikanaji wa kutosha wa fedha za kigeni nchini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news