Askari Mhifadhi hatiani kwa rushwa ya shilingi 450,000 Morogoro

MOROGORO-Mahakama ya Wilaya ya Morogoro imemtia hatiani askari mhifadhi wa Hifadhi ya Asili ya Mlima Uluguru, Bernard Mwaituka kwa kosa la kujipatia fedha kwa njia ya rushwa kinyume na kifungu cha 15(1)(a) na (2) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCA), Sura ya 329 marejeo ya mwaka 2023.
Katika shauri la rushwa namba 23268/2025, Mahakama ilielezwa kuwa, mshtakiwa alipokea kiasi cha shilingi 450,000 kwa ahadi ya kuachilia mbao pamoja na mashine za kukatia mbao (chain saw) ambazo alikuwa amezikamata kwa madai kuwa hazikuwa na vibali halali.

Hakimu Mheshimiwa Victor Kitauka, baada ya kupitia ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka, alimtia hatiani Mwaituka na kumhukumu kulipa faini ya shilingi 500,000 au kifungo cha miaka mitatu jela, pamoja na kurejesha shilingi 450,000 alizokuwa amepokea kwa njia ya hongo.

Mshtakiwa aliamua kulipa faini pamoja na kurejesha fedha hizo ili kuepuka kifungo cha jela.

Shauri hilo liliendeshwa na waendesha mashtaka kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Bi. Husna Kiboko na Bi. Felister Chamba.

Hukumu hiyo ni ushahidi kuwa,vyombo vya dola havitasita kuchukua hatua kali kwa watu au watumishi wa umma wanaojihusisha na vitendo vya rushwa, hasa vinavyohatarisha rasilimali za taifa kama misitu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news