DAR-Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limetangaza kukosekana kwa umeme leo Septemba 7, 2025 kwa zaidi ya saa 10 kutokana na matengenezo katika kituo cha kupoza umeme cha Gongolamboto.
Hayo ni kwa mujibu taarifa iliyotolewa Septemba 6, 2025 ambapo imefafanua kuwa, umeme utakosekana kuanzia saa 1 asubuhi hadi saa 11 jioni, hatua inayolenga kuimarisha huduma kwa wateja wake wa Mkoa wa Ilala na vitongoji jirani.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, maeneo yatakayoathirika na kukatika kwa umeme ni Kisarawe, Chanika yote, Moshi Bar, baadhi ya maeneo ya Mombasa na Gongolamboto.
Vilevile Kivule, Kitunda, Majohe, Chuo Kikuu cha Kampala, Mbondole, Magole, Siraly Msongola, Pugu na Ulongoni.
Pia,TANESCO imesema inatambua usumbufu utakaowakumba wateja wake na kuomba radhi kwa changamoto hiyo.
Aidha,imewataka wananchi kuwa makini na kuepuka kugusa nyaya zilizokatika au zilizo chini kwa usalama wao, na iwapo kuna tatizo lolote wawasiliane kupitia namba 180 muda wowote.
