Tanzania yaimarisha uwezo wa Burundi katika usimamizi wa ubora wa huduma za hali ya hewa

BUJUMBURA-Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), ikishirikiana na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) na Taasisi ya Hali ya Hewa ya Burundi (IGEBU), ilifanikiwa kufanya mafunzo ya kujenga uwezo wa Mfumo wa Udhibiti wa Ubora (QMS) kwa wafanyakazi zaidi ya arobaini (40) wa IGEBU,Bujumbura nchini Burundi, kuanzia tarehe 13 hadi 30 Oktoba,2025.
Mafunzo hayo yalitolewa na wataalamu wa TMA kupitia mfumo wa ushirikiano wa kimataifa wa huduma za hali ya hewa katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kupitia mpango wa WMO wa Athari za Hali ya Hewa na Mifumo ya Tahadhari ya Mapema Afrika Mashariki (CREWS), mafunzo hayo yalilenga kujenga uwezo wa kitaasisi wa IGEBU ili kuoanisha mifumo yake kwa kiwango cha udhibiti ubora cha ISO 9001:2015.
Wataalamu wa QMS kutoka TMA, walitoa mafunzo endelevu kwa wafanyakazi wa IGEBU, kuwaongoza kupitia ukaguzi wa ndani na mipango ya usimamizi.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo katika ukumbi wa Chandelier, Bujumbura, Burundi, Mkurugenzi wa Ofisi ya WMO Kanda ya Afrika, Dkt. Agnes Kijazi alipongeza dhamira ya IGEBU na mchango wa Tanzania katika kujenga uwezo wa kikanda.

"Dhamira hii ni ushuhuda wa kile kinachoweza kupatikana kupitia ushirikiano kwa kuwekeza katika mifumo bora, kuimarisha imani katika huduma za hali ya hewa, msingi wa ustahimilivu na maendeleo endelevu,"alisema Dkt.Kijazi.
Katika hatua nyingine, Mkurugenzi wa Taasisi ya Hali ya Hewa ya Burundi (IGEBU), Bw. Deogratius Babonwanayo, alitoa shukrani kwa mafunzo yaliyotolewa na kuthibitisha dhamira ya IGEBU ya kuelekea kwenye Mfumo wa Udhibiti Ubora (QMS).

Naye Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Mabadiliko ya Sayansi ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang’a alishiriki kwa njia ya mtandao, akithibitisha kuendelea kujitolea kwa TMA katika maendeleo ya kikanda kupitia ushirikiano na kubadilishana ujuzi.
Mafunzo ya QMS yalilenga kuimarisha mifumo ya ndani ya IGEBU na kuimarisha mshikamano wa kikanda katika kutoa huduma za hali ya hewa zenye ubora. Juhudi hizo zinaletwa na msukumo wa kimataifa wa WMO ili kuhakikisha nchi zote zinaweza kutoa taarifa za hali ya hewa zenye ubora kwa wakati, zitakazoaminika na zinazoweza kutekelezeka kwa ajili ya kufanya maamuzi sahihi katika shughuli zote za kijamii na kiuchumi na kulinda maisha ya watu na mali zao.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news