OBADIA Mpenzu (22), mkazi wa Kitongoji cha Majimoto, Kijiji cha Nanyala, Wilaya ya Mbozi, anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kumbaka na kumjeruhi bibi yake, Tabia Sengo (80).


Akizungumza kwa njia ya simu, Mwenyekiti wa Kijiji cha Nanyala, Maneno Mwambunga, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa lililotokea usiku wa Desemba 8, 2025.
Alisema mtuhumiwa alitekeleza tukio hilo la ukatili baada ya kufika nyumbani kwa bibi yake majira ya saa nne usiku ya Desemba 8,mwaka huu wakati mume wa bibi huyo akiwa kilabuni.

Mwambunga alisema,mara baada ya tukio hilo, mtuhumiwa alikimbilia kusikojulikana ndipo uongozi wa kijiji ulianzisha msako uliodumu hadi asubuhi ya Desemba 9,2025. Ambapo majira ya saa tano walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa akiwa amejificha porini.“Mtuhumiwa alikutwa akiwa amejificha porini na afya yake ilionekana kuwa dhaifu, akitapika na inadaiwa alikuwa amekunywa sumu kwa lengo la kujitoa uhai kwa kujutia kitendo alichofanya,”alisema Mwambunga.
Baada ya kumkuta na hali hiyo mtuhumiwa alikimbizwa katika Kituo cha Afya Nanyala kwa huduma ya dharura kabla ya kukabidhiwa polisi kwa ajili ya hatua zaidi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Augostino Senga, alikiri kumshikiria mtuhumiwa huyo na kwamba hali yake inaendelea vizuri baada ya kupatiwa matibabu na uchunguzi utakapokamilika atafikishwa kwenye vyombo vya sheria.














Tags
Kurasa za Magazeti
Kurasa za Mbele na Nyuma za Magazeti
Magazeti
Magazeti ya Leo
Magazetini
Magazetini leo
Yaliyojiri Magazetini Leo





