ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi amewasihi waumini wa Dini ya Kiislamu pamoja na wananchi wote kuendelea kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema ya amani iliyopo nchini.
Rais Mwinyi ametoa wito huo leo Disemba 19, 2025, alipojumuika na waumini wa Dini ya Kiislamu katika ibada ya Sala ya Ijumaa iliyosaliwa katika Msikiti wa Miembeni, Mkoa wa Mjini Magharibi.
Aidha, Rais Dkt.Mwinyi amesema kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu kwa amani ni tukio la kihistoria linalopaswa kuenziwa kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, akisisitiza kuwa ni wajibu wa kila mmoja kuendelea kumuomba Mungu aijalie nchi amani zaidi ili Serikali iweze kutekeleza kwa ufanisi mipango mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi.

Halikadhalika, Rais Dkt. Mwinyi amempongeza mfadhili aliyejitokeza kujenga msikiti mpya mkubwa na wa kisasa katika eneo la Miembeni, na kuwataka waumini kumuombea dua ili ujenzi huo uweze kukamilika kwa mafanikio.
Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar, Sheikh Khalid Ali Mfaume, amewahimiza waumini wa Dini ya Kiislamu kutumia vyema muda wao wa maisha hapa duniani kwa kutenda mema yatakayompendezesha Mwenyezi Mungu.










