MUYONYO-Mkutano wa dharura wa Mawaziri Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR ) wahimiza jitihada za pamoja za nchi za Afrika kutatua changamoto za Waafrika na Kikanda.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe.Dkt.Ngwaru Maghembe ameiwakilisha Tanzania katika Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na ICGLR ngazi ya Mawaziri na Nchi Wanachama wa Mkataba wa Amani, Usalama na Ushirikiano kwa DRC na Eneo la Maziwa Makuu.
Mhe. Dkt. Maghembe amemwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje naUshirikiano wa Afrika Mashariki katika kikao kilichofanyika Munyonyo, Uganda ambacho kimejadili na kupitisha ajenda za uwezeshaji wa mazungumzo ya wazi, jumuishi, yenye kujenga na kuleta suluhu za kikanda zilizoratibiwa na endelevu katika kudhibiti vyanzo vya migogoro, katika kurejesha amani ya kudumu na utulivu mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na eneo la Maziwa Makuu.
Katika mkutano huo, Tanzania kama kinara katika kukuza majadiliano, maridhiano na maendeleo endelevu, imeungana na nchi wanachama na taasisi za kimataifa kusisitiza dhamira yake thabiti ya kuendeleza amani na usalama katika Ukanda wa Maziwa Makuu. 

Kwa pamoja wametilia mkazo umuhimu wa suluhu zinazoendeshwa na michakato ya kikanda na kuongozwa na Waafrika katika kukabiliana na changamoto za kikanda.
Mkutano huo umetangulina na Mkutano wa Dharura wa Waratibu wa Kitaifa, ambapo Mkurugenzi Msaidizi, Idara ya Afrika, Bi. Ellen Maduhu aliongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo.
Kwa upande mwingine, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi atamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kikao cha Wakuu wa Nchi na Serikali wa ICGLR na PSC kitakachofanyika Desemba21,2025 kufuatia mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Uganda Mheshimiwa Yoweri Museveni.

















