DAR-Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imeonya uwepo wa mvua na radi kwa kipindi cha Januari 1 hadi 10, 2026 huku vipindi vya mvua vikitarajiwa katika baadhi ya maeneo ya Tanzania.
Maeneo yanayotajwa kupata mvua zinazoambatana na ngurumo za radi ni mikoa ya ukanda wa ziwa Viktoria abayo ni Kagera, Geita, Shinyanga, Mwanza, Simiyu na Mara.
Kwa upande wa nyanda za juu Kaskazini-Mashariki mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro itapata vipindi vya mvua machache, hasa katika siku tano za mwanzo za Januari.
Aidha,Pwani ya Kaskazini inayojumuisha mikoa ya Tanga, maeneo ya kaskazini mwa Morogoro, Pwani ya Dar es Salaam pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba vinatarajiwa kupata mvua.
Magharibi mwa Nchi, mikoa ya Kigoma, Katavi na Tabora inatarajiwa kupata mvua zinazoambatana na ngurumo za radi katika baadhi ya maeneo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Kanda ya Kati yaani mikoa ya Dodoma na Singida itapata mvua zinazoambatana na radi, hususan katika siku tano za mwanzo za Januari.
Nyanda za juu Kusini-Magharibi mikoa ya Rukwa, Songwe, Mbeya, Njombe na Iringa inatarajiwa kupata mvua zinazoambatana na ngurumo za radi katika baadhi ya maeneo.
Vilevile mikoa ya Pwani ya Kusini inayojumuisha Mtwara na Lindi kulingana na taarifa ya TMA itapata vipindi vya mvua chache.
Kanda ya Kusini mikoa wa Ruvuma na maeneo ya kusini mwa Morogoro yanatarajiwa kupata mvua zinazoambatana na ngurumo za radi katika baadhi ya maeneo.
Mbali na hayo,wakulima wanashauriwa kuzingatia ratiba za mvua ili kuepuka hasara ya mazao.
Tags
Habari
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA)
Mvua Kubwa
Mvua za Radi
Tanzania Meteorological Agency (TMA)
Utabiri wa Hali ya Hewa Tanzania
