TANGA-Bodi ya Bima ya Amana (DIB) imeendelea kutoa elimu kwa wananchi katika Maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa yanayoendelea katika viwanja vya Usagara jijini Tanga.
Pichani ni Mwanasheria wa DIB, Bi. Esther Mpendaamani, akitoa elimu kuhusu majukumu ya DIB kwa wananchi katika darasa maalum lililoandaliwa kwa ajili kutoa elimu kwa wananchi katika viwanja hivyo.
Bi. Mpendaamani amewahamasisha wananchi kutumia huduma za kibenki akiwahakikishia kwamba wanapofungua akaunti katika benki na taasisi za fedha zenye leseni kutoka Benki Kuu ya Tanzania, wanakuwa wamekingwa dhidi ya upotevu wa fedha zao endapo benki au taasisi ya fedha itafilisika.
Aidha, amewahimiza kuweka fedha benki badala ya kwenye vibubu ili kuepuka hasara ambazo zinaweza kuwapata kwa fedha kuibiwa au majanga mengine yanapotokea nyumbani.
“Unapokuwa na akaunti yako katika benki au taasisi ya fedha, una uhakika kwamba fedha yako iko salama kwa sababu Bodi ya Bima ya Amana tunakinga amana yako,” amesema Bi. Mpendaamani katika maelezo yake.
Washiriki wa elimu hiyo kutoka Makorora, Tanga walishukuru kwa maelezo yaliyotolewa na kupata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali ya ufahamu kuhusu Bodi ya Bima ya Amana ambayo yalijibiwa kwa ufasaha na Bi. Mpendaamani.
Tags
Bodi ya Bima ya Amana (DIB)
Deposit Insurance Board
(DIB)
Habari
Maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Fedha


