NJOMBE-Askofu wa Jimbo Katoliki Njombe, Mhashamu Eusebio Kyando, ameonya kuwa Waumini wa Kanisa Katoliki hawagawanyiki, akieleza kuwa katika siku za karibuni kumejitokeza jitihada za baadhi ya watu wanaolenga kuwagawa waumini hao, akisisitiza kuwa juhudi hizo hazitafua dafu.
Askofu Kyando amesema hayo Januari 1, 2026 wakati wa adhimisho la Misa Takatifu ya kuukaribisha Mwaka Mpya, akisema Kanisa Katoliki limejengwa juu ya misingi imara ya umoja ambayo haiwezi kuvunjwa wala kugawanyika.
“Sisi hatugawiki. Sisi ni kama namba witiri; huwezi kugawa namba witiri ukapata matokeo sahihi. Kanisa Katoliki si namba shufwa. Namba yetu haigawanyiki kirahisi,” alisema Askofu Kyando akitumia lugha ya mfano kufafanua msimamo wa Kanisa.
Aliongeza kuwa,Kanisa Katoliki ni Kanisa Moja, Takatifu, Katoliki na la Kitume, akionya kwamba mtu yeyote anayejihusisha au kutumiwa katika njama za kuwagawa waumini hujiingiza katika matatizo ya kiroho na laana ya bure.
Aidha, Askofu Kyando aliwahimiza waumini kuendelea kudumisha umoja na mshikamano, akisisitiza kuwa Mkatoliki wa kweli anayelipenda Kanisa lake hawezi kufikiria kuligawa, bali hufikiria namna ya kulijenga na kuimarisha umoja uliowekwa na Yesu Kristo mwenyewe.
“Hatugawanyiki. Mtu akisema amefanikiwa kuligawa Kanisa Katoliki, ukweli ni kwamba amejitenga mwenyewe na kuasi. Hajagawanya Kanisa, bali ameanzisha mwelekeo wake binafsi. Wanaodhani wanaweza kutugawa wanapoteza muda, kwa sababu Kanisa Katoliki haligawanyiki wala haliwezi kugawanyika,” alisisitiza.
Tags
Habari
Kanisa Katoliki Duniani
Kanisa Katoliki Njombe
Kanisa Katoliki Tanzania
Mhashamu Eusebio Kyando
