ZANZIBAR-Kamisheni ya Utalii Zanzibar (ZCT) imetoa tangazo kwa wadau wote wa sekta ya utalii kuhusu uendeshaji wa shughuli za utalii katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani 2026, kwa lengo la kuheshimu maadili ya kidini na tamaduni za jamii ya Zanzibar.
Katika tangazo hilo, ZCT imeeleza kuwa, Ramadhani ni kipindi kitukufu kinachoadhimishwa na Waislamu wengi Zanzibar, kinachohusisha kufunga, sala, tafakari na kuheshimu misingi ya dini na utamaduni.
Ili kudumisha amani ya kijamii na kuhakikisha utalii unaowajibika, waendeshaji wa biashara za utalii, wahudumu na wageni wametakiwa kuzingatia miongozo ifuatayo:
■Migahawa na maduka ya vyakula nje ya hoteli yafungwe wakati wa mchana na kufunguliwa baada ya machweo (Iftar).
■Huduma za chakula na vinywaji ndani ya hoteli zitolewe kwa wageni wa hoteli pekee na ndani ya majengo ya hoteli.
■Kula, kunywa au kuvuta sigara hadharani wakati wa mchana hakuruhusiwi.
■Vazi la heshima liheshimiwe katika maeneo ya umma.

