DAR-Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rush wa (TAKUKURU), Mkoa wa Temeke imemfIkisha mahakamani Askofu wa Kanisa la Hosanna Assemblies of God Tanzania (HAOGT), Renatus Nyalali kwa tuhuma za kughushi nyaraka.
Naibu Mkuu wa Takukuru, Mkoa wa Temeke, Ismail Bukuku alisema askofu huyo anadaiwa kughushi nyaraka na kutoa nyaraka za uongo zinazohusiana na umiliki wa ardhi ili aweze kujipatia kiwanja chenye thamani ya Sh 60,000,000.
Ameyasema hayo Machi 5,2026 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari, ambapo hatua hiyo imechukuliwa baada ya uchunguzi wa kina uliofanywa na Takukuru baada ya kupokea taarifa kutoka kwa mmoja wa warithi na msimamizi wa mirathi ya Ally Hillal.
“Kutokana na ushahidi uliokusanywa na kufanyiwa uchambuzi wa kitaalamu, Takukuru imefungua kesi ya jinai dhidi ya Askofu Renatus Nyalali, katika Mahakama ya Wilaya ya Kigamboni."
Alisema kwa mujibu wa hati ya mashitaka, inadaiwa kati ya mwaka 2021 hadi 2022, mshitakiwa alighushi nyaraka na sahihi za wanafamilia wa Ally kwa lengo la kujipatia umiliki wa eneo la ardhi lililopo Mtaa wa Kizani, Geza Ulole, Wilaya ya Kigamboni ambapo eneo hilo lilinunuliwa mwaka 2008 kwa shilingi milioni sitini na kuachwa kama urithi kwa watoto wa Ally.
Pia, ilidaiwa kuwa mshitakiwa alitumia mwanya wa kuaminiwa na familia ya marehemu kuandaa nyaraka za uwakilishi (Power of Attorney) kwa njia isiyo halali ambapo nyaraka hizo zilidaiwa kutumika kupima eneo hilo na kuligawa katika viwanja tisa, ambavyo baadaye vilikuwa vikiuzwa kwa watu mbalimbali kwa kutumia majina na sahihi za kughushi za wanafamilia.
Tags
Askofu Renatus Nyalali
Habari
Mahakamani Leo
PCCB Tanzania
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)
