NA DIRAMAKINI
SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) limewataarifu wateja wake kuwa litafanya maboresho ya mfumo wa manunuzi ya umeme wa kulipia kabla (LUKU), hatua inayolenga kuboresha ufanisi na upatikanaji wa huduma hiyo kwa watumiaji.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na shirika hilo leo Machi 10,2026 maboresho hayo yanatarajiwa kufanyika kesho Jumatano usiku kuamkia Alhamisi kuanzia saa 6:00 usiku hadi saa 8:00 usiku, sawa na muda wa masaa mawili.
Kutokana na zoezi hilo la kiufundi, huduma ya kununua umeme kupitia mfumo wa LUKU haitapatikana katika kipindi chote cha maboresho hayo.
Aidha, TANESCO imewashauri wateja wake kununua umeme mapema kabla ya muda uliopangwa wa maboresho ili kuepusha usumbufu wowote unaoweza kujitokeza wakati huduma hiyo itakapokuwa imesitishwa kwa muda.
Shirika hilo limeeleza kuwa, maboresho hayo ni sehemu ya juhudi zake za kuimarisha mifumo ya utoaji huduma kwa wateja na kuhakikisha upatikanaji wa huduma za umeme unakuwa bora na wa kuaminika zaidi.
